1 1 Neno la Bwana ambalo lilimjia Yoeli mwana wa Pethueli.
2 Sikilizeni hili, enyi wazee;
sikilizeni, ninyi nyote mnaoishi katika nchi.
Je, jambo kama hili lilishawahi kutokea
katika siku zenu au katika siku za babu zenu?
3 Waelezeni watoto wenu,
na watoto wenu wawaambie watoto wao,
na watoto wao kwa kizazi kitakachofuata.
4 Kilichosazwa na kundi la tunutu
nzige wakubwa wamekula,
kilichosazwa na nzige wakubwa
parare wamekula,
kilichosazwa na parare
madumadu wamekula.
5 Amkeni, enyi walevi, mlie!
Pigeni yowe enyi wanywaji wote wa mvinyo,
pigeni yowe kwa sababu ya mvinyo mpya,
kwa kuwa mmenyangʼanywa
kutoka midomoni mwenu.
6 Taifa limevamia nchi yangu,
lenye nguvu tena lisilo na idadi;
lina meno ya simba,
magego ya simba jike.
7 Limeharibu mizabibu yangu
na kuangamiza mitini yangu.
Limebambua magome yake
na kuyatupilia mbali,
likayaacha matawi yake yakiwa meupe.
8 Omboleza kama bikira aliyevaa nguo ya gunia
anayehuzunika kwa ajili ya mume wa ujana wake.
9 Sadaka za nafaka na sadaka za kinywaji
zimekatiliwa mbali kutoka nyumba ya Bwana.
Makuhani wanaomboleza,
wale wanaohudumu mbele za Bwana.
10 Mashamba yameharibiwa,
ardhi imekauka;
nafaka imeharibiwa,
mvinyo mpya umekauka,
mafuta yamekoma.
11 Kateni tamaa, enyi wakulima,
lieni, enyi mlimao mizabibu;
huzunikeni kwa ajili ya ngano na shayiri,
kwa sababu mavuno ya shambani yameharibiwa.
12 Mzabibu umekauka
na mtini umenyauka;
mkomamanga, mtende na mtofaa,
miti yote shambani, imekauka.
Hakika furaha yote ya mwanadamu
imeondoka.
13 Vaeni nguo ya gunia, enyi makuhani, muomboleze;
pigeni yowe, enyi mnaohudumu madhabahuni.
Njooni, vaeni nguo ya gunia usiku kucha,
enyi mnaohudumu mbele za Mungu wangu;
kwa kuwa sadaka za nafaka na sadaka za kinywaji
zimezuiliwa kufika katika nyumba ya Mungu wenu.
14 Tangazeni saumu takatifu;
liiteni kusanyiko takatifu.
Iteni wazee
na wote waishio katika nchi
waende katika nyumba ya Bwana Mungu wenu,
wakamlilie Bwana.
15 Ole kwa siku hiyo!
Kwa kuwa siku ya Bwana iko karibu;
itakuja kama uharibifu
kutoka kwa Mwenyezi.[fn]
16 Je, chakula hakikukatiliwa mbali
mbele ya macho yetu:
furaha na shangwe
kutoka nyumba ya Mungu wetu?
17 Mbegu zinakauka
chini ya mabonge ya udongo.
Ghala zimeachwa katika uharibifu,
ghala za nafaka zimebomolewa,
kwa maana hakuna nafaka.
18 Jinsi gani ngʼombe wanavyolia!
Makundi ya mifugo yanahangaika
kwa sababu hawana malisho;
hata makundi ya kondoo yanateseka.
19 Kwako, Ee Bwana, naita,
kwa kuwa moto umeteketeza
malisho ya mbugani
na miali ya moto imeunguza
miti yote shambani.
20 Hata wanyama wa porini wanakuonea shauku;
vijito vya maji vimekauka,
na moto umeteketeza
malisho yote ya mbugani.
2 1 Pigeni tarumbeta katika Sayuni;
pigeni mbiu katika mlima wangu mtakatifu.
Wote waishio katika nchi na watetemeke,
kwa kuwa siku ya Bwana inakuja. Iko karibu,
2 siku ya giza na huzuni,
siku ya mawingu na utusitusi.
Kama mapambazuko yasambaavyo
toka upande huu wa milima
hata upande mwingine
jeshi kubwa na lenye nguvu linakuja.
Jambo kama hili halijakuwepo tangu zamani
wala halitakuwepo tena kamwe
kwa vizazi vijavyo.
3 Mbele yao moto unateketeza,
nyuma yao miali ya moto
inawaka kwa nguvu.
Mbele yao nchi iko kama bustani ya Edeni,
nyuma yao ni jangwa lisilofaa:
hakuna kitu kinachowaepuka.
4 Wanaonekana kama farasi;
wanakwenda mbio
kama askari wapanda farasi.
5 Wanatoa sauti kama magari ya vita,
wanaporukaruka juu ya vilele vya milima,
kama mlio wa miali ya moto ilayo mabua,
kama jeshi kubwa lililojipanga kwa ajili ya vita.
6 Wanapoonekana, mataifa yanakuwa katika maumivu makuu;
kila uso unabadilika rangi.
7 Wanashambulia kama wapiganaji wa vita;
wanapanda kuta kama askari.
Wote wanatembea katika safu,
hawapotoshi safu zao.
8 Hakuna anayemsukuma mwenzake;
kila mmoja anakwenda mbele moja kwa moja.
Wanapita katika vizuizi
bila kuharibu safu zao.
9 Wanaenda kasi kuingia mjini;
wanakimbia ukutani.
Wanaingia ndani ya nyumba;
kwa kuingilia madirishani kama wevi.
10 Mbele yao dunia inatikisika,
anga linatetemeka,
jua na mwezi vinatiwa giza,
na nyota hazitoi mwanga wake tena.
11 Bwana anatoa mshindo wa ngurumo
mbele ya jeshi lake;
majeshi yake hayana idadi,
ni wenye nguvu nyingi
wale ambao hutii agizo lake.
Siku ya Bwana ni kuu,
ni ya kutisha.
Ni nani anayeweza kuistahimili?
12 “Hata sasa,” asema Bwana,
“nirudieni kwa mioyo yenu yote,
kwa kufunga, kwa kulia na kuomboleza.”
13 Rarueni mioyo yenu
na siyo mavazi yenu.
Mrudieni Bwana, Mungu wenu,
kwa maana yeye ndiye mwenye neema
na mwingi wa huruma,
si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa upendo,
huona huruma, hujizuia kuleta maafa.
14 Ni nani ajuaye? Yeye aweza kugeuka na kuwa na huruma
na kuacha baraka nyuma yake:
sadaka za nafaka na sadaka za vinywaji
kwa ajili ya Bwana Mungu wenu.
15 Pigeni tarumbeta katika Sayuni,
tangazeni saumu takatifu,
liiteni kusanyiko takatifu.
16 Wakusanyeni watu,
wekeni wakfu kusanyiko;
waleteni pamoja wazee,
wakusanyeni watoto,
wale wanyonyao maziwa.
Bwana arusi na atoke chumbani mwake
na bibi arusi naye atoke katika chumba chake.
17 Makuhani, ambao wanahudumu mbele za Bwana,
na walie katikati ya ukumbi
wa Hekalu na madhabahu.
Waseme, “Wahurumie watu wako, Ee Bwana.
Usifanye urithi wako kitu cha kudharauliwa,
neno la dhihaka kati ya mataifa.
Kwa nini wasemezane miongoni mwao,
‘Yuko wapi Mungu wao?’ ”
18 Kisha Bwana atakuwa na wivu kwa ajili ya nchi yake
na kuwa na huruma juu ya watu wake.
19 Bwana atawajibu:
“Ninawapelekea nafaka,
mvinyo mpya na mafuta,
vya kuwatosha ninyi
hadi mridhike kabisa;
kamwe sitawafanya tena
kitu cha kudharauliwa na mataifa.
20 “Nitafukuza jeshi la kaskazini likae mbali nanyi,
nikilisukuma ndani ya jangwa,
askari wa safu za mbele wakienda
ndani ya bahari ya mashariki
na wale wa safu za nyuma
katika bahari ya magharibi.
Uvundo wake utapaa juu;
harufu yake itapanda juu.”
Hakika ametenda mambo makubwa.
21 Usiogope, ee nchi;
furahi na kushangilia.
Hakika Bwana ametenda mambo makubwa.
22 Msiogope, enyi wanyama pori,
kwa kuwa mbuga za malisho yenu
zinarudia ubichi.
Miti nayo inazaa matunda,
mtini na mzabibu inatoa utajiri wake.
23 Furahini, enyi watu wa Sayuni,
shangilieni katika Bwana Mungu wenu,
kwa kuwa amewapa mvua za vuli
kwa kipimo cha haki.
Anawapelekea mvua nyingi,
mvua ya vuli na ya masika, kama mwanzoni.
24 Sakafu za kupuria zitajaa nafaka,
mapipa yatafurika mvinyo mpya na mafuta.
25 “Nitawalipa kwa ajili ya miaka ile iliyoliwa na nzige:
parare, madumadu na tunutu,
jeshi langu kubwa ambalo
nililituma katikati yenu.
26 Mtakuwa na wingi wa vyakula mpaka mshibe,
na mtalisifu jina la Bwana Mungu wenu,
ambaye amefanya maajabu kwa ajili yenu;
kamwe watu wangu hawataaibishwa tena.
27 Ndipo mtakapojua kwamba mimi niko katika Israeli
kwamba mimi ndimi Bwana Mungu wenu,
na kwamba hakuna mwingine;
kamwe watu wangu hawataaibika tena.
28 “Hata itakuwa, baada ya hayo,
nitamimina Roho wangu juu ya wote wenye mwili.
Wana wenu na binti zenu watatabiri,
wazee wenu wataota ndoto,
na vijana wenu wataona maono.
29 Hata juu ya watumishi wangu, wanaume kwa wanawake,
katika siku zile nitamimina Roho wangu.
30 Nami nitaonyesha maajabu katika mbingu
na duniani:
damu, moto na mawimbi ya moshi.
31 Jua litageuzwa kuwa giza
na mwezi kuwa mwekundu kama damu,
kabla ya kuja siku ya Bwana
ile kuu na ya kutisha.
32 Na kila mtu atakayeliitia
jina la Bwana ataokolewa.
Kwa maana juu ya Mlima Sayuni na katika Yerusalemu
kutakuwepo wokovu,
kama Bwana alivyosema,
miongoni mwa walionusurika
ambao Bwana awaita.
3 1 “Katika siku hizo na wakati huo,
nitakaporejesha neema ya Yuda na Yerusalemu,
2 nitayakusanya mataifa yote na kuyaleta
katika Bonde la Yehoshafati[fn]
Hapo nitaingia kwenye hukumu dhidi yao
kuhusu urithi wangu, watu wangu Israeli,
kwa kuwa waliwatawanya watu wangu
miongoni mwa mataifa
na kuigawa nchi yangu.
3 Wanawapigia kura watu wangu
na kuwauza wavulana ili kupata makahaba;
waliwauza wasichana
ili wapate kunywa mvinyo.
4 “Sasa una nini dhidi yangu, ee Tiro na Sidoni, nanyi nchi zote za Ufilisti? Je, mnanilipiza kwa yale niliyoyafanya? Kama mnalipa, mimi nitalipiza juu ya vichwa vyenu kwa kasi na kwa haraka yale mliyoyatenda. 5 Kwa kuwa mlichukua fedha na dhahabu yangu pia mkabeba hazina zangu nzuri sana mkapeleka kwenye mahekalu yenu. 6 Mliwauza watu wa Yuda na Yerusalemu kwa Wayunani, ili kwamba mpate kuwapeleka mbali na nchi yao.
7 “Tazama nitawaamsha kutoka zile sehemu mlizowauza, nami nitawalipiza juu ya vichwa vyenu kile mlichofanya. 8 Nitawauza wana wenu na binti zenu kwa watu wa Yuda, nao watawauza kwa Waseba, taifa lililo mbali.” Bwana amesema.
9 Tangazeni hili miongoni mwa mataifa:
Jiandaeni kwa vita!
Amsha askari!
Wanaume wote wapiganaji
wasogee karibu na kushambulia.
10 Majembe yenu yafueni yawe panga
na miundu yenu ya kukatia iwe mikuki.
Aliye dhaifu na aseme,
“Mimi nina nguvu!”
11 Njooni haraka, ninyi mataifa yote kutoka pande zote,
kusanyikeni huko.
Shusha wapiganaji wako, Ee Bwana!
12 “Mataifa na yaamshwe;
na yasonge mbele kuelekea Bonde la Yehoshafati,
kwa kuwa nitaketi mahali pale
kuhukumu mataifa yote yaliyoko kila upande.
13 Tia mundu,
kwa kuwa mavuno yamekomaa.
Njooni, mkanyage zabibu,
kwa kuwa shinikizo la kukamua zabibu limejaa
na mapipa yanafurika:
kwa kuwa uovu wao ni mkubwa!”
14 Umati mkubwa, umati mkubwa
katika bonde la uamuzi!
Kwa kuwa siku ya Bwana ni karibu
katika bonde la uamuzi.
15 Jua na mwezi vitatiwa giza,
na nyota hazitatoa mwanga wake tena.
16 Bwana atanguruma kutoka Sayuni
na mshindo wa ngurumo kutoka Yerusalemu;
dunia na mbingu vitatikisika.
Lakini Bwana atakuwa kimbilio la watu wake,
ngome imara kwa ajili ya watu wa Israeli.
17 “Ndipo mtakapojua kwamba Mimi, Bwana Mungu wenu,
nakaa Sayuni, mlima wangu mtakatifu.
Yerusalemu utakuwa mtakatifu;
kamwe wageni hawatavamia tena.
18 “Katika siku hiyo milima itadondosha divai mpya,
na vilima vitatiririka maziwa;
mabonde yote ya Yuda yatatiririka maji.
Chemchemi itatiririka kutoka kwenye nyumba ya Bwana
na kunywesha Bonde la Shitimu.[fn]
19 Lakini Misri itakuwa ukiwa,
Edomu itakuwa jangwa tupu,
kwa sababu ya jeuri waliofanya kwa watu wa Yuda,
ambao katika nchi yao
walimwaga damu isiyo na hatia.
20 Yuda itakaliwa na watu milele
na Yerusalemu itadumu vizazi vyote.
21 Hatia yao ya damu, ambayo sijasamehe,
nitasamehe.”