Mhubiri
1
Kila Kitu Ni Ubatili Mtupu
Maneno ya Mhubiri, mwana wa Daudi, mfalme huko Yerusalemu:
“Ubatili mtupu! Ubatili mtupu!”
Mhubiri anasema.
“Ubatili mtupu!
Kila kitu ni ubatili.”
 
Mwanadamu anafaidi nini kutokana na kazi yake yote
anayotaabikia chini ya jua?
Vizazi huja na vizazi hupita,
lakini dunia inadumu milele.
Jua huchomoza na jua huzama,
nalo huharakisha kurudi mawioni.
Upepo huvuma kuelekea kusini
na kugeukia kaskazini,
hurudia mzunguko huo huo,
daima ukirudia njia yake.
Mito yote hutiririka baharini,
hata hivyo bahari kamwe haijai.
Mahali mito inapotoka,
huko hurudi tena.
Vitu vyote vinachosha,
zaidi kuliko mtu anavyoweza kusema.
Jicho kamwe halitosheki kutazama,
wala sikio halishibi kusikia.
Kile kilichokuwepo kitakuwepo tena,
kile kilichofanyika kitafanyika tena,
hakuna kilicho kipya chini ya jua.
10 Kuna kitu chochote ambacho mtu anaweza kusema,
“Tazama! Kitu hiki ni kipya”?
Kilikuwepo tangu zamani za kale,
kilikuwepo kabla ya wakati wetu.
11 Hakuna kumbukumbu ya watu wa zamani,
hata na wale ambao hawajaja bado
hawatakumbukwa
na wale watakaofuata baadaye.
Hekima Ni Ubatili
12 Mimi, Mhubiri, nilikuwa mfalme wa Israeli katika Yerusalemu. 13 Nilitumia muda wangu wote kujifunza na kuvumbua kwa hekima yote yanayofanyika chini ya mbingu. Jinsi gani Mungu ameweka mzigo mzito juu ya wanadamu! 14 Nimeshaona mambo yote yanayotendeka chini ya jua, hayo yote ni ubatili, hii ni kukimbiza upepo.
15 Kilichopindika hakiwezi kunyooshwa,
kile ambacho hakipo haiwezekani kukihesabu.
16 Niliwaza mwenyewe, “Tazama, nimekua na kuongezeka katika hekima kuliko yeyote aliyewahi kutawala Yerusalemu kabla yangu. Nimekuwa na uzoefu mkubwa wa hekima na maarifa.” 17 Ndipo nilipojitahidi kufahamu kutofautisha hekima, wazimu na upumbavu, lakini nikatambua hata hili nalo ni kukimbiza upepo.
18 Kwa kuwa hekima nyingi huleta huzuni kubwa;
maarifa yanapoongezeka, masikitiko yanaongezeka.