Zaburi. 19. Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi. Mbingu zinatangaza utukufu wa Mungu, anga zahubiri kazi ya mikono yake. Siku baada ya siku zinatoa habari, usiku baada ya usiku zinatangaza maarifa. Hakuna msemo wala lugha, ambapo sauti zao hazisikiki. Sauti yao imeenea duniani pote, nayo maneno yao yameenea hadi miisho ya ulimwengu. Katika mbingu amepiga hema kwa ajili ya jua, linafanana na bwana arusi akitoka chumbani mwake, kama shujaa afurahiavyo kukamilisha kushindana kwake. Huchomoza upande mmoja wa mbingu, na kufanya mzunguko wake hadi upande mwingine. Hakuna kilichojificha joto lake. Sheria ya Bwana ni kamilifu, ikihuisha nafsi. Shuhuda za Bwana ni za kuaminika, zikimpa mjinga hekima. Maagizo ya Bwana ni kamili, nayo hufurahisha moyo. Amri za Bwana huangaza, zatia nuru machoni. Kumcha Bwana ni utakatifu, nako kwadumu milele. Amri za Bwana ni za hakika, nazo zina haki. Ni za thamani kuliko dhahabu, kuliko dhahabu iliyo safi sana, ni tamu kuliko asali, kuliko asali kutoka kwenye sega. Kwa hizo mtumishi wako anaonywa, katika kuzishika kuna thawabu kubwa. Ni nani awezaye kutambua makosa yake? Nisamehe makosa yangu nisiyoyajua. Mlinde mtumishi wako na dhambi za makusudi, nazo zisinitawale. Ndipo nitakapokuwa sina lawama, wala sitakuwa na hatia ya kosa kubwa. Maneno ya kinywa changu na mawazo ya moyo wangu, yapate kibali mbele zako, Ee Bwana, Mwamba wangu na Mkombozi wangu.