Zaburi. 74. Utenzi wa Asafu. Ee Mungu, mbona umetukataa milele? Mbona hasira yako inatoka moshi juu ya kondoo wa malisho yako? Kumbuka watu uliowanunua zamani, kabila la urithi wako, ambao uliwakomboa: Mlima Sayuni, ambamo uliishi. Geuza hatua zako kuelekea magofu haya ya kudumu, uharibifu wote huu ambao adui ameuleta pale patakatifu. Adui zako wamenguruma pale ulipokutana nasi, wanaweka bendera zao kama alama. Walifanya kama watu wanaotumia mashoka kukata kichaka cha miti. Walivunjavunja milango yote iliyonakshiwa kwa mashoka na vishoka vyao. Waliteketeza kabisa mahali pako patakatifu, wakayanajisi makao ya Jina lako. Walisema mioyoni mwao, “Tutawaponda kabisa!” Walichoma kila mahali ambapo Mungu aliabudiwa katika nchi. Hatukupewa ishara za miujiza; hakuna manabii waliobaki, hakuna yeyote kati yetu ajuaye hali hii itachukua muda gani. Ee Mungu, mtesi atakudhihaki mpaka lini? Je, adui watalitukana jina lako milele? Kwa nini unazuia mkono wako, mkono wako wa kuume? Uutoe kutoka makunjo ya vazi lako na uwaangamize! Lakini wewe, Ee Mungu, ni mfalme wangu tangu zamani, unaleta wokovu duniani. Ni wewe uliyeigawanya bahari kwa uweza wako; ulivunja vichwa vya wanyama wakubwa wa kutisha katika maji. Ni wewe uliyeponda vichwa vya Lewiathani nawe ukamtoa kama chakula kwa viumbe vya jangwani. Ni wewe uliyefungua chemchemi na vijito, ulikausha mito ambayo ilikuwa ikitiririka daima. Mchana ni wako, nao usiku ni wako pia, uliziweka jua na mwezi. Ni wewe uliyeiweka mipaka yote ya dunia, ulifanya kiangazi na masika. Ee Bwana, kumbuka jinsi mtesi alivyokudhihaki, jinsi watu wapumbavu walivyolitukana jina lako. Usiukabidhi uhai wa njiwa wako kwa wanyama wakali wa mwitu; usisahau kabisa uhai wa watu wako wanaoteseka milele. Likumbuke agano lako, maana mara kwa mara mambo ya jeuri yamejaa katika sehemu za giza nchini. Usiruhusu walioonewa warudi nyuma kwa aibu; maskini na wahitaji hebu walisifu jina lako. Inuka, Ee Mungu, ujitetee; kumbuka jinsi wapumbavu wanavyokudhihaki mchana kutwa. Usipuuze makelele ya watesi wako, ghasia za adui zako, zinazoinuka mfululizo.