Zaburi. 146. Msifuni Bwana! Ee nafsi yangu, umsifu Bwana, Nitamsifu Bwana maisha yangu yote; nitamwimbia Mungu wangu sifa wakati wote niishipo. Usiweke tumaini lako kwa wakuu, kwa wanadamu ambao hufa, ambao hawawezi kuokoa. Roho yao itokapo hurudi mavumbini, siku hiyo hiyo mipango yao yote hukoma. Heri yeye ambaye Mungu wa Yakobo ni msaada wake, ambaye tumaini lake ni katika Bwana, Mungu wake, Muumba wa mbingu na nchi, na bahari na vyote vilivyomo ndani yake: Bwana anayedumu kuwa mwaminifu milele na milele. Naye huwapatia haki walioonewa na kuwapa wenye njaa chakula. Bwana huwaweka wafungwa huru, Bwana huwafumbua vipofu macho, Bwana huwainua waliolemewa na mizigo yao, Bwana huwapenda wenye haki. Bwana huwalinda wageni na kuwategemeza yatima na wajane, lakini hupinga njia za waovu. Bwana atamiliki milele, Mungu wako, ee Sayuni, kwa vizazi vyote. Msifuni Bwana.