Wimbo Ulio Bora. 1. Wimbo ulio bora wa Solomoni. Unibusu kwa busu la kinywa chako, kwa maana upendo wako unafurahisha kuliko divai. Manukato yako yananukia vizuri, jina lako ni kama manukato yaliyomiminwa. Ndiyo sababu wanawali wanakupenda! Nichukue twende nawe, na tufanye haraka! Mfalme na anilete ndani ya vyumba vyake. Marafiki Tunakushangilia na kukufurahia, tutasifu upendo wako zaidi kuliko divai. Mpendwa Tazama jinsi ilivyo bora wakupende! Mimi ni mweusi, lakini napendeza, enyi binti za Yerusalemu, mweusi kama mahema ya Kedari, kama mapazia ya hema la Solomoni. Usinikazie macho kwa sababu mimi ni mweusi, kwa sababu nimefanywa mweusi na jua. Wana wa mama yangu walinikasirikia na kunifanya niwe mtunza mashamba ya mizabibu. Shamba langu mwenyewe la mizabibu nimeliacha. Niambie, wewe ambaye ninakupenda, unalisha wapi kundi lako la kondoo na ni wapi unapowapumzisha kondoo wako adhuhuri. Kwa nini niwe kama mwanamke aliyefunikwa shela karibu na makundi ya rafiki zako? Kama hujui, ewe mwanamke mzuri kuliko wote, fuata nyayo za kondoo, na kulisha wana-mbuzi wako karibu na hema za wachungaji. Mpenzi wangu, ninakufananisha na farasi jike aliyefungwa katika mojawapo ya magari ya vita ya Farao. Mashavu yako yanapendeza yakiwa na vipuli, shingo yako ikiwa na mikufu ya vito. Tutakufanyia vipuli vya dhahabu, vyenye kupambwa kwa fedha. Wakati mfalme alipokuwa mezani pake, manukato yangu yalisambaza harufu yake nzuri. Mpenzi wangu kwangu mimi ni kifuko cha manemane kati ya matiti yangu. Mpenzi wangu kwangu mimi ni kama kishada cha maua ya mhina kutoka mashamba ya mizabibu ya En-Gedi. Tazama jinsi ulivyo mzuri, mpenzi wangu! Tazama jinsi ulivyo mzuri! Macho yako ni kama ya hua. Tazama jinsi ulivyo mzuri, mpenzi wangu! Ee, tazama jinsi unavyopendeza! Na kitanda chetu ni cha majani mazuri. Nguzo za nyumba yetu ni mierezi, na mapao yetu ni miberoshi.