Hosea. 5. “Sikieni hili, enyi makuhani! Kuweni wasikivu, enyi Waisraeli! Sikieni, ee nyumba ya mfalme! Hukumu hii ni dhidi yenu: Mmekuwa mtego huko Mispa, wavu uliotandwa juu ya Tabori. Waasi wamezidisha sana mauaji. Mimi nitawatiisha wote. Ninajua yote kuhusu Efraimu, Israeli hukufichika kwangu. Efraimu, sasa umegeukia ukahaba, Israeli amenajisika. “Matendo yao hayawaachii kurudi kwa Mungu wao. Roho ya ukahaba imo ndani ya mioyo yao, hawamkubali Bwana. Kiburi cha Israeli kinashuhudia dhidi yao; Waisraeli, hata Efraimu, wanajikwaa katika dhambi zao; pia Yuda atajikwaa pamoja nao. Wakati wanapokwenda na makundi yao ya kondoo na ngʼombe kumtafuta Bwana, hawatampata; yeye amejiondoa kutoka kwao. Wao si waaminifu kwa Bwana; wamezaa watoto haramu. Sasa sikukuu zao za Mwandamo wa Mwezi zitawaangamiza wao pamoja na mashamba yao. “Pigeni tarumbeta huko Gibea, baragumu huko Rama. Paza kilio cha vita huko Beth-Aveni, ongoza, ee Benyamini. Efraimu ataachwa ukiwa katika siku ya kuadhibiwa. Miongoni mwa makabila ya Israeli ninatangaza lile ambalo halina budi kutukia. Viongozi wa Yuda ni kama wale wanaosogeza mawe ya mpaka. Nitamwaga ghadhabu yangu juu yao kama mafuriko ya maji. Efraimu ameonewa, amekanyagwa katika hukumu kwa kuwa amekusudia kufuatia sanamu. Mimi ni kama nondo kwa Efraimu, na kama uozo kwa watu wa Yuda. “Wakati Efraimu alipoona ugonjwa wake, naye Yuda vidonda vyake, ndipo Efraimu alipogeukia Ashuru, na kuomba msaada kwa mfalme mkuu. Lakini hawezi kukuponya, wala hawezi kukuponya vidonda vyako. Kwa maana nitakuwa kama simba kwa Efraimu, kama simba mkubwa kwa Yuda. Nitawararua vipande vipande na kuondoka; nitawachukua mbali, na hakuna wa kuwaokoa. Kisha nitarudi mahali pangu mpaka watakapokubali kosa lao. Nao watautafuta uso wangu; katika taabu yao watanitafuta kwa bidii.”