Mwanzo 1MwanzoSiku Sita Za Uumbaji Na Sabato 1 1:1Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia. 2 1:2Wakati huu dunia ilikuwa haina umbo, tena ilikuwa tupu. Giza lilikuwa juu ya uso wa vilindi vya maji, naye Roho wa Mungu alikuwa ametulia juu ya maji.
  • 3 1:3Mungu akasema, “Iwepo nuru,” nayo nuru ikawepo. 4 1:4Mungu akaona ya kuwa nuru ni njema, ndipo Mungu akatenganisha nuru na giza. 5 1:5Mungu akaiita nuru “mchana,” na giza akaliita “usiku.” Ikawa jioni, ikawa asubuhi, siku ya kwanza.
  • 6 1:6Mungu akasema, “Iwepo nafasi kati ya maji igawe maji na maji.” 7 1:7Kwa hiyo Mungu akafanya nafasi, akatenganisha maji yaliyo chini ya hiyo nafasi na maji yaliyo juu yake. Ikawa hivyo. 8 1:8Mungu akaiita hiyo nafasi “anga.” Ikawa jioni, ikawa asubuhi, siku ya pili.
  • 9 1:9Mungu akasema, “Maji yaliyopo chini ya anga na yakusanyike mahali pamoja, pawepo na nchi kavu.” Ikawa hivyo. 10 1:10Mungu akaiita nchi kavu “ardhi,” nalo lile kusanyiko la maji akaliita “bahari.” Mungu akaona kuwa ni vyema.
  • 11 1:11Kisha Mungu akasema, “Ardhi na itoe mimea: miche itoayo mbegu, miti juu ya nchi itoayo matunda yenye mbegu ndani yake, kila mmea kulingana na aina zake mbalimbali.” Ikawa hivyo. 12 1:12Ardhi ikachipua mimea: Mimea itoayo mbegu kulingana na aina zake, na miti itoayo matunda yenye mbegu kulingana na aina zake. Mungu akaona ya kuwa hili ni jema. 13 1:13Ikawa jioni, ikawa asubuhi, siku ya tatu.
  • 14 1:14Mungu akasema, “Iwepo mianga kwenye nafasi ya anga ili itenganishe usiku na mchana, nayo iwe alama ya kutambulisha majira mbalimbali, siku na miaka, 15 1:15nayo iwe mianga kwenye nafasi ya anga ya kutia nuru juu ya dunia.” Ikawa hivyo. 16 1:16Mungu akafanya mianga miwili mikubwa: mwanga mkubwa utawale mchana, na mwanga mdogo utawale usiku. Pia Mungu akafanya nyota. 17 1:17Mungu akaiweka katika nafasi ya anga iangaze dunia, 18 1:18itawale usiku na mchana, na ikatenganishe nuru na giza. Mungu akaona kuwa hili ni jema. 19 1:19Ikawa jioni, ikawa asubuhi, siku ya nne.
  • 20 1:20Mungu akasema, “Kuwepo na viumbe hai tele kwenye maji, nao ndege waruke juu ya dunia katika nafasi ya anga.” 21 1:21Kwa hiyo Mungu akaumba viumbe wakubwa wa baharini na kila kiumbe hai kiendacho majini kulingana na aina zake, na kila ndege mwenye mabawa kulingana na aina yake. Mungu akaona kuwa hili ni jema. 22 1:22Mungu akavibariki, akasema, “Zaeni mwongezeke, mkayajaze maji ya bahari, nao ndege waongezeke katika dunia.” 23 1:23Ikawa jioni, ikawa asubuhi, siku ya tano.
  • 24 1:24Mungu akasema, “Ardhi na itoe viumbe hai kulingana na aina zake: wanyama wa kufugwa, viumbe vitambaavyo ardhini na wanyama pori, kila mnyama kulingana na aina yake.” Ikawa hivyo. 25 1:25Mungu akafanya wanyama pori kulingana na aina zake, wanyama wa kufugwa kulingana na aina zake, na viumbe vyote vitambaavyo juu ya ardhi kulingana na aina zake. Mungu akaona kuwa hili ni jema.
  • 26 1:26Ndipo Mungu akasema, “Tufanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu, wakatawale juu ya samaki wa baharini na ndege wa angani, juu ya mifugo, juu ya dunia yote, na juu ya viumbe wote watambaao juu ya nchi.” 27 1:27Kwa hiyo Mungu akamuumba mtu kwa mfano wake mwenyewe, kwa mfano wa Mungu alimuumba; mwanaume na mwanamke aliwaumba. 28 1:28Mungu akawabariki na akawaambia, “Zaeni na mkaongezeke, mkaijaze tena dunia na kuitiisha. Mkatawale samaki wa baharini, ndege wa angani, na kila kiumbe hai kiendacho juu ya ardhi.” 29 1:29Kisha Mungu akasema, “Nimewapa kila mche utoao mbegu juu ya uso wa dunia yote, na kila mti wenye matunda yenye mbegu ndani yake. Vitakuwa chakula chenu. 30 1:30Nao wanyama wote wa dunia, ndege wote wa angani, na viumbe vyote viendavyo juu ya ardhi: yaani kila kiumbe chenye pumzi ya uhai, ninawapa kila mche wa kijani kuwa chakula.” Ikawa hivyo. 31 1:31Mungu akaona vyote alivyoumba, na tazama, ilikuwa vizuri sana. Ikawa jioni, ikawa asubuhi, siku ya sita. 21 2:1Kwa hiyo mbingu na dunia zikakamilika, pamoja na vyote vilivyomo.
  • 2 2:2Katika siku ya saba Mungu alikuwa amekamilisha kazi aliyokuwa akiifanya, hivyo siku ya saba akapumzika kutoka kazi zake zote. 3 2:3Mungu akaibariki siku ya saba akaifanya takatifu, kwa sababu katika siku hiyo alipumzika kutoka kazi zote za kuumba alizokuwa amefanya.
  • Adamu Na Eva

    4 2:4Haya ndiyo maelezo ya mbingu na dunia wakati zilipoumbwa.

    Bwana Mungu alipoziumba mbingu na dunia, 5 2:5hapakuwepo na mche wa shambani uliokuwa umejitokeza ardhini, wala hapakuwepo na mmea wa shamba uliokuwa umeota, kwa kuwa Bwana Mungu alikuwa hajanyeshea mvua juu ya nchi, na hapakuwepo mtu wa kuilima ardhi, 6 2:6lakini umande ulitokeza kutoka ardhini na kunyesha uso wote wa nchi: 7 2:7 Bwana Mungu alimuumba mtu kutoka mavumbi 2:7 Neno la Kiebrania la mavumbi ya ardhi ndilo kiini cha jina Adamu. ya ardhi, akampulizia pumzi ya uhai puani mwake, naye mtu akawa kiumbe hai.

    8 2:8Basi Bwana Mungu alikuwa ameotesha bustani upande wa mashariki, katika Edeni, huko akamweka huyo mtu aliyemuumba. 9 2:9 Bwana Mungu akafanya aina zote za miti ziote kutoka ardhini, miti yenye kupendeza macho na mizuri kwa chakula. Katikati ya bustani ulikuwepo mti wa uzima na mti wa kujua mema na mabaya.

    10 2:10Mto wa kunyeshea bustani ulitiririka toka Edeni, kuanzia hapa ukagawanyika kuwa mito minne. 11 2:11Mto wa kwanza uliitwa Pishoni, nao huzunguka nchi yote ya Havila ambako kuna dhahabu. 12 2:12(Dhahabu ya nchi hiyo ni nzuri, bedola na vito shohamu pia hupatikana huko.) 13 2:13Jina la mto wa pili ni Gihoni, ambao huzunguka nchi yote ya Kushi. 14 2:14Jina la mto wa tatu ni Tigrisi, unaopita mashariki ya Ashuru. Mto wa nne ni Frati.

    15 2:15 Bwana Mungu akamchukua huyo mtu, akamweka kwenye Bustani ya Edeni ailime na kuitunza. 16 2:16 Bwana Mungu akamwagiza huyo mtu, akamwambia, “Uko huru kula matunda ya mti wowote katika bustani, 17 2:17lakini kamwe usile matunda ya mti wa kujua mema na mabaya, kwa maana siku utakapokula matunda yake, hakika utakufa.”

    18 2:18 Bwana Mungu akasema, “Si vyema huyu mtu awe peke yake. Nitamfanyia msaidizi wa kumfaa.”

    19 2:19Basi Bwana Mungu alikuwa amefanyiza kutoka ardhi wanyama wote wa porini na ndege wote wa angani. Akawaleta kwa huyu mtu aone atawaitaje, nalo jina lolote alilokiita kila kiumbe hai, likawa ndilo jina lake. 20 2:20Hivyo Adamu akawapa majina wanyama wote wa kufugwa, ndege wa angani, na wanyama wote wa porini.

    Lakini kwa Adamu hakupatikana msaidizi wa kumfaa. 21 2:21Hivyo Bwana Mungu akamfanya Adamu kulala usingizi mzito, naye alipokuwa amelala akachukua moja ya mbavu zake, akapafunika mahali pale kwa nyama. 22 2:22Kisha Bwana Mungu akamfanya mwanamke kutoka kwenye ule ubavu aliouchukua kutoka kwa huyo mwanaume, akamleta huyo mwanamke kwa huyo mwanaume.

    23 2:23Huyo mwanaume akasema,

    “Huyu sasa ni mfupa wa mifupa yangu na nyama ya nyama yangu, ataitwa ‘mwanamke,’ 2:23 Jina la Kiebrania la mwanamke linafanana na lile la mwanaume. kwa kuwa alitolewa katika mwanaume.” 24 2:24Kwa sababu hii mwanaume atamwacha baba yake na mama yake na kuambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja.

    25 2:25Adamu na mkewe wote wawili walikuwa uchi, wala hawakuona aibu.

    3Kuanguka Kwa Mwanadamu

    1 3:1Basi nyoka alikuwa mwerevu kuliko wanyama wote wa porini ambao Bwana Mungu aliwafanya. Nyoka akamwambia mwanamke, “Ati kweli Mungu alisema, ‘Kamwe msile matunda ya mti wowote wa bustanini’?”

    2 3:2Mwanamke akamjibu nyoka, “Tunaweza kula matunda ya miti iliyoko bustanini, 3 3:3lakini Mungu alisema, ‘Kamwe msile tunda la mti ulio katikati ya bustani, wala kuugusa, la sivyo mtakufa.’ ”

    4 3:4Lakini nyoka akamwambia mwanamke, “Hakika hamtakufa. 5 3:5Kwa maana Mungu anajua ya kuwa wakati mtakapoyala, macho yenu yatafumbuliwa, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.”

    6 3:6Mwanamke alipoona ya kuwa tunda la mti huo lilikuwa zuri kwa chakula na la kupendeza macho, tena linatamanika kwa kujipatia hekima, basi akachuma katika matunda yake, akala, pia akampa mumewe, aliyekuwa pamoja naye, naye akala. 7 3:7Ndipo macho yao wote wawili yakafumbuliwa, wakajiona kwamba walikuwa uchi; hivyo wakashona majani ya mtini, wakajifunika.

    8 3:8Ndipo yule mwanaume na mkewe, waliposikia sauti ya Bwana Mungu alipokuwa akitembea bustanini jioni, wakajificha kutoka mbele za Bwana Mungu katikati ya miti ya bustani. 9 3:9Lakini Bwana Mungu akamwita Adamu, “Uko wapi?”

    10 3:10Naye akajibu, “Nilikusikia katika bustani nikaogopa kwa sababu nilikuwa uchi, hivyo nikajificha.”

    11 3:11Mungu akamuuliza, “Ni nani aliyekuambia ya kuwa ulikuwa uchi? Je, umekula matunda ya mti niliokuamuru usile?”

    12 3:12Adamu akasema, “Huyu mwanamke uliyenipa awe pamoja nami alinipa sehemu ya tunda kutoka kwenye huo mti, nami nikala.”

    13 3:13Ndipo Bwana Mungu akamuuliza mwanamke, “Ni nini hili ambalo umelifanya?” Mwanamke akajibu, “Nyoka alinidanganya, nami nikala.”

    14 3:14Hivyo Bwana Mungu akamwambia nyoka, “Kwa kuwa umefanya hili,

    “Umelaaniwa kuliko wanyama wote wa kufugwa na wa porini! Utatambaa kwa tumbo lako na kula mavumbi siku zote za maisha yako. 15 3:15Nami nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na wake, yeye atakuponda kichwa, nawe utamuuma kisigino.”

    16 3:16Kwa mwanamke akasema,

    “Nitakuzidishia sana utungu wakati wa kuzaa kwako; kwa utungu utazaa watoto. Tamaa yako itakuwa kwa mumeo naye atakutawala.”

    17 3:17Kwa Adamu akasema, “Kwa sababu umemsikiliza mke wako na ukala kutoka kwenye mti niliokuamuru, ‘Msile tunda lake,’

    “Ardhi imelaaniwa kwa sababu yako, kwa kazi ngumu utakula chakula kitokacho humo siku zote za maisha yako. 18 3:18Itazaa miiba na mibaruti kwa ajili yako, nawe utakula mimea ya shambani. 19 3:19Kwa jasho la uso wako utakula chakula chako hadi utakaporudi ardhini, kwa kuwa ulitwaliwa kutoka humo, kwa kuwa wewe u mavumbi na mavumbini wewe utarudi.”

    20 3:20Adamu akamwita mkewe Eva, kwa kuwa atakuwa mama wa wote walio hai.

    21 3:21 Bwana Mungu akawatengenezea Adamu na mkewe mavazi ya ngozi, akawavika. 22 3:22Kisha Bwana Mungu akasema, “Sasa mtu huyu amekuwa kama mmoja wetu, kwa kujua mema na mabaya. Sharti asiruhusiwe kunyoosha mkono wake na kuchuma pia kutoka mti wa uzima akala, naye akaishi milele.” 23 3:23Hivyo Bwana Mungu akamfukuzia mbali kutoka Bustani ya Edeni, akalime ardhi ambamo alitolewa. 24 3:24Baada ya kumfukuzia mbali Adamu, Mungu akaweka makerubi mashariki ya Bustani ya Edeni, pamoja na upanga wa moto ukimulika huku na huko kulinda njia ya kuuendea mti wa uzima.

    4Kaini Na Abeli

    1 4:1Adamu akakutana kimwili na mkewe Eva, naye akapata mimba, akamzaa Kaini. Eva akasema, “Kwa msaada wa Bwana nimemzaa mwanaume.” 2 4:2Baadaye akamzaa Abeli ndugu yake.

    Basi Abeli akawa mfugaji, na Kaini akawa mkulima. 3 4:3Baada ya muda Kaini akaleta baadhi ya mazao ya shamba kama sadaka kwa Bwana. 4 4:4Lakini Abeli akaleta fungu nono kutoka baadhi ya wazaliwa wa kwanza wa mifugo yake. Bwana akamkubali Abeli pamoja na sadaka yake, 5 4:5lakini Mungu hakumkubali Kaini pamoja na sadaka yake. Kwa hiyo Kaini akakasirika sana, uso wake ukawa na huzuni.

    6 4:6Kisha Bwana akamwambia Kaini, “Kwa nini umekasirika? Kwa nini uso wako una huzuni? 7 4:7Ukifanya lililo sawa, je, hutakubalika? Lakini usipofanya lililo sawa, dhambi inakuvizia mlangoni mwako, inakutamani wewe, lakini inakupasa uishinde.”

    8 4:8Basi Kaini akamwambia ndugu yake Abeli, “Twende shambani.” Walipokuwa shambani, Kaini akamshambulia Abeli ndugu yake, akamuua.

    9 4:9Kisha Bwana akamuuliza Kaini, “Ndugu yako Abeli yuko wapi?”

    Akamjibu, “Sijui, je, mimi ni mlinzi wa ndugu yangu?”

    10 4:10 Bwana akasema, “Umefanya nini? Sikiliza! Damu ya ndugu yako inanililia mimi kutoka ardhini. 11 4:11Sasa umelaaniwa na umehamishwa kutoka ardhi, ambayo imefungua kinywa chake na kupokea damu ya ndugu yako kutoka mkononi mwako. 12 4:12Utakapoilima ardhi, haitakupa tena mazao yake. Utakuwa mtu wa kutangatanga duniani asiye na utulivu.”

    13 4:13Kaini akamwambia Bwana, “Adhabu yangu ni zaidi ya niwezavyo kustahimili. 14 4:14Leo unanifukuza kutoka nchi, nami nitafichwa mbali na uwepo wako. Nitakuwa mtu wa kutangatanga asiyetulia duniani na yeyote anionaye ataniua.”

    15 4:15Lakini Bwana akamwambia, “La sivyo, ikiwa mtu yeyote atamuua Kaini atalipizwa kisasi mara saba zaidi.” Kisha Bwana akamwekea Kaini alama ili mtu yeyote ambaye angemwona asimuue. 16 4:16Kwa hiyo Kaini akaondoka mbele za Bwana akaenda kuishi katika nchi ya Nodi, iliyoko mashariki ya Edeni.

    17 4:17Kaini akakutana kimwili na mkewe, naye akapata mimba na akamzaa Enoki. Wakati huo Kaini alikuwa anajenga mji, akauita Enoki jina la mtoto wake. 18 4:18Enoki akamzaa Iradi, Iradi akamzaa Mehuyaeli, Mehuyaeli akamzaa Methushaeli, na Methushaeli akamzaa Lameki.

    19 4:19Lameki alioa wanawake wawili, mmoja aliitwa Ada, na mwingine Sila. 20 4:20Ada akamzaa Yabali ambaye ni baba wa wale walioishi katika mahema na kufuga wanyama. 21 4:21Kaka yake aliitwa Yubali, aliyekuwa baba wa wote wapigao zeze na filimbi. 22 4:22Pia Sila alikuwa na mtoto wa kiume aliyeitwa Tubali-Kaini ambaye alifua vifaa vya aina mbalimbali vya shaba na chuma. Naama alikuwa dada wa Tubali-Kaini.

    23 4:23Lameki akawaambia wake zake,

    “Ada na Sila nisikilizeni mimi; wake wa Lameki sikieni maneno yangu. Nimemuua mtu kwa kunijeruhi, kijana mdogo kwa kuniumiza. 24 4:24Kama Kaini atalipizwa kisasi mara saba, basi Lameki itakuwa mara sabini na saba.”

    25 4:25Adamu akakutana kimwili na mke wake tena, akamzaa mwana, akamwita Sethi, akisema, “Mungu amenijalia mwana mwingine badala ya Abeli, kwa kuwa Kaini alimuua.” 26 4:26Naye Sethi akamzaa mwana, akamwita Enoshi.

    Wakati huo watu wakaanza kuliitia jina la Bwana.

    5Kutoka Adamu Hadi Noa (1 Nyakati 1:1-4)

    1 5:1Hii ni orodha iliyoandikwa ya vizazi vya Adamu.

    Wakati Mungu alipomuumba Adamu, alimfanya kwa sura ya Mungu. 2 5:2Aliwaumba mwanaume na mwanamke, akawabariki. Walipokwisha kuumbwa, akawaita “mwanadamu.”

    3 5:3Adamu alipokuwa ameishi miaka 130, alikuwa na mwana aliyekuwa na sura yake, mwenye kufanana naye. Akamwita Sethi. 4 5:4Baada ya Sethi kuzaliwa, Adamu aliishi miaka 800, akawa na watoto wengine wa kiume na wa kike. 5 5:5Adamu aliishi jumla ya miaka 930, ndipo akafa.

    6 5:6Sethi alipokuwa ameishi miaka 105, akamzaa Enoshi. 7 5:7Baada ya kumzaa Enoshi, Sethi aliishi miaka 807, akawa na watoto wengine wa kiume na wa kike. 8 5:8Sethi aliishi jumla ya miaka 912, ndipo akafa.

    9 5:9Enoshi alipokuwa ameishi miaka tisini, akamzaa Kenani. 10 5:10Baada ya kumzaa Kenani, Enoshi aliishi miaka 815, naye alikuwa na watoto wengine wa kiume na wa kike. 11 5:11Enoshi aliishi jumla ya miaka 905, ndipo akafa.

    12 5:12Kenani alipokuwa ameishi miaka sabini, akamzaa Mahalaleli. 13 5:13Baada ya kumzaa Mahalaleli, Kenani aliishi miaka 840, akawa na watoto wengine wa kiume na wa kike. 14 5:14Kenani aliishi jumla ya miaka 910, ndipo akafa.

    15 5:15Mahalaleli alipokuwa ameishi miaka sitini na mitano, akamzaa Yaredi. 16 5:16Baada ya kumzaa Yaredi, Mahalaleli aliishi miaka 830, akawa na watoto wengine wa kiume na wa kike. 17 5:17Mahalaleli aliishi jumla ya miaka 895, ndipo akafa.

    18 5:18Yaredi alipokuwa ameishi miaka 162, akamzaa Enoki. 19 5:19Baada ya kumzaa Enoki, Yaredi aliishi miaka 800, naye akawa na watoto wengine wa kiume na wa kike. 20 5:20Yaredi aliishi jumla ya miaka 962, ndipo akafa.

    21 5:21Enoki alipokuwa ameishi miaka sitini na mitano, akamzaa Methusela. 22 5:22Baada ya kumzaa Methusela, Enoki alitembea na Mungu miaka 300, na akawa na watoto wengine wa kiume na wa kike. 23 5:23Enoki aliishi jumla ya miaka 365. 24 5:24Enoki akatembea na Mungu, kisha akatoweka, kwa sababu Mungu alimchukua.

    25 5:25Methusela alipokuwa ameishi miaka 187, akamzaa Lameki. 26 5:26Baada ya kumzaa Lameki, Methusela aliishi miaka 782, akawa na watoto wengine wa kiume na wa kike. 27 5:27Methusela aliishi jumla ya miaka 969, ndipo akafa.

    28 5:28Lameki alipokuwa ameishi miaka 182, alimzaa mwana. 29 5:29Akamwita jina lake Noa, akasema, “Yeye ndiye atakayetufariji katika kazi na maumivu makali ya mikono yetu yaliyosababishwa na ardhi iliyolaaniwa na Bwana.” 30 5:30Baada ya Noa kuzaliwa, Lameki aliishi miaka 595, akawa na watoto wengine wa kiume na wa kike. 31 5:31Lameki aliishi jumla ya miaka 777, ndipo akafa.

    32 5:32Baada ya Noa kuishi miaka 500, aliwazaa Shemu, Hamu na Yafethi.

    6Gharika Kuu

    1 6:1Watu walipoanza kuongezeka idadi katika uso wa dunia na watoto wa kike wakazaliwa kwao, 2 6:2wana wa Mungu wakawaona kuwa hao binti za wanadamu walikuwa wazuri wa sura, wakaoa yeyote miongoni mwao waliyemchagua. 3 6:3Ndipo Bwana akasema, “Roho yangu haitashindana na mwanadamu milele, kwa kuwa yeye ni wa kufa, siku zake zitakuwa miaka 120.”

    4 6:4Wanefili walikuwako duniani siku hizo, na baadaye, hao wana wa Mungu walipoingia kwa binti za wanadamu na kuzaa nao. Wanefili walikuwa mashujaa na watu waliojulikana wa zamani hizo.

    5 6:5 Bwana akaona jinsi uovu wa mwanadamu ulivyokuwa mkubwa duniani, na ya kuwa kila mwelekeo wa mawazo ya moyo wake wakati wote ulikuwa mbaya tu. 6 6:6 Bwana akasikitika kwamba alimuumba mwanadamu duniani, moyo wa Mungu ukajaa masikitiko. 7 6:7Kwa hiyo Bwana akasema, “Nitamfutilia mbali mwanadamu niliyemuumba kutoka kwenye uso wa dunia, wanadamu na wanyama, pamoja na viumbe vitambaavyo na ndege wa angani. Kwa maana nasikitika kuwaumba.” 8 6:8Lakini Noa akapata kibali machoni pa Bwana.

    9 6:9Hivi ndivyo vizazi vya Noa.

    Noa alikuwa mtu wa haki, na mkamilifu miongoni mwa watu wa wakati wake, tena alitembea na Mungu. 10 6:10Noa alikuwa na wana watatu: Shemu, Hamu na Yafethi.

    11 6:11Wakati huu dunia ilikuwa imejaa uharibifu na ukatili machoni pa Mungu. 12 6:12Mungu akaona jinsi dunia ilivyoharibika, kwa maana watu wote duniani walikuwa wameharibu njia zao. 13 6:13Kwa hiyo Mungu akamwambia Noa, “Nitawaangamiza watu wote, kwa kuwa dunia imejaa ukatili kwa sababu yao. Hakika mimi nitaangamiza watu pamoja na dunia. 14 6:14Kwa hiyo jitengenezee safina kubwa kwa mbao za mvinje, tengeneza vyumba ndani yake na uipake lami ndani na nje. 15 6:15Hivi ndivyo utakavyoitengeneza: Safina iwe na urefu wa dhiraa 300, 6:15 Dhiraa 300 ni sawa na mita 135. upana wake dhiraa hamsini 6:15 Dhiraa 50 ni sawa na mita 22:5. na kimo chake dhiraa thelathini. 6:15 Dhiraa 30 ni sawa na mita 13:5. 16 6:16Itengenezee paa na umalizie safina kwa kuacha nafasi ya dhiraa moja 6:16 Dhiraa moja ni sawa na sentimita 45. juu. Weka mlango ubavuni mwa safina, na uifanye ya ghorofa ya chini, ya kati na ya juu. 17 6:17Nitaleta gharika ya maji juu ya nchi ili kuangamiza uhai wote chini ya mbingu, kila kiumbe chenye pumzi ya uhai ndani yake. Kila kitu juu ya nchi kitaangamia. 18 6:18Lakini Mimi nitaweka Agano langu na wewe, nawe utaingia ndani ya Safina, wewe pamoja na mke wako, wanao na wake zao. 19 6:19Utaingiza ndani ya Safina kila aina ya kiumbe hai wawili wawili, wa kiume na wa kike, ili kuwahifadhi hai pamoja na wewe. 20 6:20Wawili wa kila aina ya ndege, wa kila aina ya mnyama na wa kila aina ya kitambaacho ardhini watakuja kwako ili wahifadhiwe hai. 21 6:21Utachukua kila aina ya chakula kitakacholiwa, na ukiweke akiba kama chakula kwa ajili yako na yao.”

    22 6:22Noa akafanya kila kitu kama vile Mungu alivyomwamuru.

    71 7:1Ndipo Bwana akamwambia Noa, “Ingia katika safina wewe na jamaa yako yote, kwa sababu katika kizazi hiki nimeona ya kuwa wewe ni mwenye haki. 2 7:2Uchukue wanyama saba walio safi wa kila aina, wa kiume na wa kike, na wanyama wawili wawili wa kila aina walio najisi wa kiume na wa kike. 3 7:3Pia uchukue ndege saba walio safi wa kila aina, wa kiume na wa kike, ili kuhifadhi aina zao mbalimbali katika dunia yote. 4 7:4Siku saba kuanzia sasa nitaleta mvua juu ya nchi kwa siku arobaini usiku na mchana, nami nitafutilia mbali kutoka uso wa nchi kila kiumbe hai nilichokiumba.”

    5 7:5Noa akafanya yote kama Bwana alivyomwamuru.

    6 7:6Noa alikuwa na miaka 600 gharika ilipokuja juu ya dunia. 7 7:7Noa na mkewe na wanawe na wake zao wakaingia katika safina ili waepuke ile gharika. 8 7:8Jozi ya wanyama walio safi na walio najisi, ndege na viumbe vitambaavyo, 9 7:9wa kiume na wa kike, walikuja kwa Noa wakaingia katika safina kama Mungu alivyomwamuru Noa. 10 7:10Baada ya siku saba, maji ya gharika yakaja juu ya dunia.

    11 7:11Katika siku ya kumi na saba ya mwezi wa pili mwaka wa 600 wa kuishi kwake Noa, siku hiyo ndipo chemchemi zote hata zilizo chini sana ya ardhi zilibubujika kwa nguvu, na malango ya mafuriko ya mbinguni yakafunguliwa. 12 7:12Mvua ikanyesha juu ya nchi siku arobaini usiku na mchana.

    13 7:13Siku hiyo Noa, na mkewe, na wanawe Shemu, Hamu na Yafethi pamoja na wake zao wakaingia katika ile safina. 14 7:14Nao walikuwa pamoja na kila mnyama wa mwituni kufuatana na aina yake, wanyama wote wafugwao kufuatana na aina zao, kila kiumbe kitambaacho juu ya ardhi kwa aina yake, na kila ndege kufuatana na aina yake, naam kila kiumbe chenye mabawa. 15 7:15Viumbe vyote vyenye pumzi ya uhai ndani yake vikaja kwa Noa viwili viwili, vikaingia katika safina. 16 7:16Wanyama walioingia katika safina walikuwa wa kiume na wa kike, wa kila kiumbe chenye uhai kama Mungu alivyomwamuru Noa, ndipo Bwana akamfungia ndani.

    17 7:17Kwa siku arobaini mafuriko yaliendelea kujaa duniani na maji yalivyozidi kuongezeka, yaliinua safina juu sana kutoka kwenye uso wa nchi. 18 7:18Maji yakajaa na kuongezeka sana juu ya nchi, na safina ikaelea juu ya uso wa maji. 19 7:19Maji yakazidi kujaa juu ya nchi, yakaifunika milima yote mirefu chini ya mbingu yote. 20 7:20Maji yakaendelea kujaa yakaifunika milima kwa kina cha zaidi ya dhiraa kumi na tano. 7:20 Dhiraa 15 ni sawa na mita 7. 21 7:21Kila kiumbe hai kitambaacho juu ya nchi kikaangamia: Ndege, wanyama wa kufugwa, wanyama pori, viumbe vyote juu ya nchi na wanadamu wote. 22 7:22Kila kiumbe juu ya nchi kavu chenye pumzi ya uhai kikafa. 23 7:23Kila kitu chenye uhai juu ya uso wa nchi kilifutiliwa mbali, watu, wanyama, viumbe vitambaavyo na ndege warukao angani wakafutiliwa mbali toka duniani. Waliobaki ni Noa peke yake na wale waliokuwa pamoja naye ndani ya safina.

    24 7:24Maji yakaifunika dunia kwa siku 150.

    8Mwisho Wa Gharika

    1 8:1Mungu akamkumbuka Noa na wanyama wote wa porini na wa kufugwa waliokuwa naye ndani ya safina, akatuma upepo ukavuma katika dunia, nayo maji yakaondoka. 2 8:2Zile chemchemi zilizo chini sana ya ardhi pamoja na malango ya mafuriko ya mbinguni yakawa yamefungwa nayo mvua ikawa imekoma kunyesha kutoka angani. 3 8:3Maji yakaendelea kupungua taratibu katika nchi. Kunako mwisho wa siku ya 150, maji yalikuwa yamepungua, 4 8:4katika siku ya kumi na saba ya mwezi wa saba, safina ikatua katika milima ya Ararati. 5 8:5Maji yakaendelea kupungua hadi mwezi wa kumi, na siku ya kwanza ya mwezi wa kumi, vilele vya milima vikaonekana.

    6 8:6Baada ya siku arobaini Noa akafungua dirisha alilokuwa amelifanya katika safina 7 8:7na akamtoa kunguru, akawa akiruka kwenda na kurudi mpaka maji yalipokwisha kukauka juu ya nchi. 8 8:8Kisha akamtoa hua ili aone kama maji yameondoka juu ya uso wa ardhi. 9 8:9Lakini hua hakupata mahali pa kutua kwa kuwa maji yalienea juu ya uso wa dunia yote, kwa hiyo akarudi kwa Noa ndani ya safina. Noa akanyoosha mkono akamchukua yule hua akamrudisha ndani ya safina. 10 8:10Noa akangojea siku saba zaidi kisha akamtoa tena hua kutoka safina. 11 8:11Wakati hua aliporejea kwa Noa jioni, alikuwa amechukua katika mdomo wake jani bichi la mzeituni, lililochumwa wakati ule ule! Ndipo Noa akajua ya kuwa maji yameondoka juu ya uso wa dunia. 12 8:12Akangojea siku saba zaidi na akamtuma tena hua, lakini wakati huu hua hakurudi tena kwa Noa.

    13 8:13Katika siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza ya mwaka 601, wa kuishi kwake Noa, maji yalikuwa yamekauka duniani. Kisha Noa akafungua mlango wa safina akaona ya kuwa uso wa ardhi ulikuwa umekauka. 14 8:14Katika siku ya ishirini na saba ya mwezi wa pili dunia ilikuwa imekauka kabisa.

    15 8:15Ndipo Mungu akamwambia Noa, 16 8:16“Toka ndani ya safina, wewe na mkeo na wanao na wake zao. 17 8:17Utoe nje kila aina ya kiumbe hai aliye pamoja nawe: Ndege, wanyama na viumbe vyote vitambaavyo juu ya ardhi, ili wakazae, na kuongezeka na kuijaza tena dunia.”

    18 8:18Kwa hiyo Noa akatoka nje pamoja na mkewe, wanawe na wake zao. 19 8:19Wanyama wote na viumbe vyote vitambaavyo juu ya ardhi na ndege wote, kila kitu kiendacho juu ya nchi, aina moja baada ya nyingine vikatoka katika safina, kila aina ya kiumbe, kimoja baada ya kingine.

    Noa Atoa Dhabihu

    20 8:20Kisha Noa akamjengea Bwana madhabahu, akachukua baadhi ya wale wanyama na ndege wote walio safi, akatoa sadaka za kuteketezwa juu ya madhabahu. 21 8:21 Bwana akasikia harufu nzuri ya kupendeza, naye akasema moyoni mwake, “Kamwe sitailaani tena ardhi kwa sababu ya mwanadamu, hata ingawa kila mwelekeo wa moyo wake ni mbaya tangu ujana. Kamwe sitaangamiza tena viumbe hai vyote kama nilivyofanya.

    22 8:22“Kwa muda dunia idumupo, wakati wa kupanda na wa kuvuna, wakati wa baridi na wa joto, wakati wa kiangazi na wa masika, usiku na mchana kamwe havitakoma.” 9Mungu Aweka Agano Na Noa

    1 9:1Ndipo Mungu akambariki Noa na wanawe, akiwaambia, “Zaeni mkaongezeke kwa idadi na mkaijaze tena dunia. 2 9:2Wanyama wote wa duniani, ndege wote wa angani, kila kiumbe kitambaacho juu ya ardhi, na samaki wote wa baharini wamekabidhiwa mikononi mwenu, nao watawaogopa na kuwahofu. 3 9:3Kila kitu chenye uhai kiendacho kitakuwa chakula chenu. Kama vile nilivyowapa mimea mbalimbali, sasa nawapa kila kitu.

    4 9:4“Lakini kamwe msile nyama ambayo bado ina damu ya uhai wake, kwa maana damu ni uhai. 5 9:5Hakika damu ya uhai wenu nitaidai. Nitaidai kutoka kwa kila mnyama. Kutoka kwa kila mwanadamu pia nitaidai kwa ajili ya uhai wa mtu mwenzake.

    6 9:6“Yeyote amwagaye damu ya mwanadamu, damu yake itamwagwa na mwanadamu, kwa kuwa katika mfano wa Mungu, Mungu alimuumba mwanadamu. 7 9:7Kuhusu ninyi, zaeni mwongezeke kwa wingi, mzidi katika dunia na kuijaza.”

    8 9:8Ndipo Mungu akamwambia Noa na wanawe pamoja naye: 9 9:9“Sasa mimi ninaweka Agano langu nanyi, pamoja na uzao wenu baada yenu, 10 9:10pia na kila kiumbe hai kilichokuwa pamoja nanyi: Ndege, wanyama wa kufugwa na wanyama wote wa porini, wale wote waliotoka katika safina pamoja nanyi, kila kiumbe hai duniani. 11 9:11Ninaweka Agano nanyi: Kamwe uhai hautafutwa tena kwa gharika, kamwe haitakuwepo tena gharika ya kuangamiza dunia.”

    12 9:12Mungu akasema, “Hii ni ishara ya Agano ninalofanya kati yangu na ninyi na kila kiumbe hai kilicho pamoja nanyi, Agano kwa vizazi vyote vijavyo: 13 9:13Nimeweka upinde wangu wa mvua mawinguni, nao utakuwa ishara ya Agano nifanyalo kati yangu na dunia. 14 9:14Wakati wowote ninapotanda mawingu juu ya dunia na upinde wa mvua ukijitokeza mawinguni, 15 9:15nitakumbuka Agano langu kati yangu na ninyi na viumbe vyote vilivyo hai vya kila aina. Kamwe maji hayatakuwa tena gharika ya kuangamiza uhai wote. 16 9:16Wakati wowote upinde wa mvua unapotokea mawinguni, nitauona na kukumbuka Agano la milele kati ya Mungu na viumbe vyote vilivyo hai vya kila aina duniani.”

    17 9:17Hivyo Mungu akamwambia Noa, “Hii ndiyo ishara ya Agano ambalo nimelifanya kati yangu na viumbe vyote vilivyo hai duniani.”

    Wana Wa Noa

    18 9:18Wana wa Noa waliotoka ndani ya safina ni: Shemu, Hamu na Yafethi. (Hamu ndiye alikuwa baba wa Kanaani.) 19 9:19Hawa ndio waliokuwa wana watatu wa Noa, kutokana nao watu walienea katika dunia.

    20 9:20Noa akawa mkulima, akawa mtu wa kwanza kupanda mizabibu. 21 9:21Alipokunywa huo mvinyo wake akalewa na akalala uchi kwenye hema lake. 22 9:22Hamu, baba wa Kanaani, akauona uchi wa baba yake na kuwaeleza ndugu zake wawili waliokuwa nje. 23 9:23Lakini Shemu na Yafethi wakachukua nguo wakaitanda mabegani mwao wote wawili, kisha wakaenda kinyumenyume, wakaufunika uchi wa baba yao. Nyuso zao zilielekea upande mwingine ili wasiuone uchi wa baba yao.

    24 9:24Noa alipolevuka kutoka kwenye mvinyo wake na kujua lile ambalo mwanawe mdogo kuliko wote alilokuwa amemtendea, 25 9:25akasema,

    “Alaaniwe Kanaani! Atakuwa mtumwa wa chini sana kuliko watumwa wote kwa ndugu zake.”

    26 9:26Pia akasema,

    “Abarikiwe Bwana, Mungu wa Shemu! Kanaani na awe mtumwa wa Shemu. 27 9:27Mungu na apanue mipaka ya Yafethi; Yafethi na aishi katika mahema ya Shemu, na Kanaani na awe mtumwa wake.”

    28 9:28Baada ya gharika Noa aliishi miaka 350. 29 9:29Noa alikuwa na jumla ya miaka 950, ndipo akafa.

    10Mataifa Yaliyotokana Na Noa (1 Nyakati 1:5-23)

    1 10:1Hawa ndio wazao wa Noa: Shemu, Hamu na Yafethi, ambao walizaa wana baada ya gharika.

    Wazao Wa Yafethi
  • 2 10:2Wana wa Yafethi walikuwa:
  • Gomeri, Magogu, Madai, Yavani, Tubali, Mesheki na Tirasi.
  • 3 10:3Wana wa Gomeri walikuwa:
  • Ashkenazi, Rifathi na Togarma.
  • 4 10:4Wana wa Yavani walikuwa:
  • Elisha, Tarshishi, Kitimu na Rodanimu. 5 10:5(Kutokana na hawa mataifa ya Pwani yalienea katika nchi zao, kwa koo zao katika mataifa yao, kila moja kwa lugha yake.) Wazao Wa Hamu
  • 6 10:6Wana wa Hamu walikuwa:
  • Kushi, Misraimu, 10:6 Yaani Misri. Putu na Kanaani.
  • 7 10:7Wana wa Kushi walikuwa:
  • Seba, Havila, Sabta, Raama na Sabteka.
  • Wana wa Raama walikuwa:
  • Sheba na Dedani.

    8 10:8Kushi akamzaa Nimrodi, ambaye alikua akawa mtu shujaa duniani. 9 10:9Alikuwa mwindaji hodari mbele za Bwana. Ndiyo sababu watu husema, “Kama Nimrodi, hodari wa kuwinda mbele za Bwana.” 10 10:10Vituo vyake vya kwanza katika ufalme wake vilikuwa Babeli, Ereki, Akadi na Kalne katika Shinari. 11 10:11Kutoka nchi ile alikwenda Ashuru, ambako alijenga Ninawi, Rehoboth-iri, Kala, 12 10:12na Reseni, iliyo kati ya Ninawi na Kala; huo ndio mji mkubwa.

  • 13 10:13Misraimu alikuwa baba wa:
  • Waludi, Waanami, Walehabi, Wanaftuhi, 14 10:14Wapathrusi, Wakasluhi (hao ndio asili ya Wafilisti), na Wakaftori.
  • 15 10:15Kanaani alikuwa baba wa:
  • Sidoni mzaliwa wake wa kwanza, Hethi, 16 10:16Wayebusi, Waamori, Wagirgashi, 17 10:17Wahivi, Waariki, Wasini, 18 10:18Waarvadi, Wasemari na Wahamathi.

    Baadaye koo za Wakanaani zilitawanyika, 19 10:19na mipaka ya Kanaani ilienea kutoka Sidoni kuelekea Gerari hadi Gaza, kisha kuelekea Sodoma, Gomora, Adma na Seboimu, hadi kufikia Lasha.

    20 10:20Hawa ni wana wa Hamu kwa koo zao na lugha zao, katika nchi zao na mataifa yao.

    Wazao Wa Shemu

    21 10:21Shemu ambaye ni ndugu mkubwa wa Yafethi, kwake kulizaliwa wana pia. Shemu alikuwa baba wa wana wote wa Eberi.

  • 22 10:22Wana wa Shemu walikuwa:
  • Elamu, Ashuru, Arfaksadi, Ludi na Aramu.
  • 23 10:23Wana wa Aramu walikuwa:
  • Usi, Huli, Getheri na Mesheki.
  • 24 10:24Arfaksadi alikuwa baba wa Shela,
  • naye Shela akamzaa Eberi.
  • 25 10:25Eberi akapata wana wawili:
  • Mmoja wao aliitwa Pelegi, kwa kuwa wakati wake ndipo dunia iligawanyika; nduguye aliitwa Yoktani.
  • 26 10:26Yoktani alikuwa baba wa:
  • Almodadi, Shelefu, Hasarmawethi, Yera, 27 10:27Hadoramu, Uzali, Dikla, 28 10:28Obali, Abimaeli, Sheba, 29 10:29Ofiri, Havila na Yobabu. Hawa wote walikuwa wana wa Yoktani. 30 10:30Nchi waliyoishi ilienea toka Mesha kuelekea Sefari kwenye nchi ya vilima iliyoko mashariki.

    31 10:31Hao ndio wana wa Shemu kwa koo zao na lugha zao, katika nchi zao na mataifa yao.

    32 10:32Hizi ndizo koo za wana wa Noa, kufuatana na vizazi vyao, katika mataifa yao. Kutokana na hawa mataifa yalienea duniani kote baada ya gharika.

    11Mnara Wa Babeli

    1 11:1Wakati huo dunia yote ilikuwa na lugha moja na msemo mmoja. 2 11:2Watu walipoelekea upande wa mashariki, wakafika kwenye tambarare katika nchi ya Shinari 11:2 Shinari ndio Babeli. nao wakaishi huko.

    3 11:3Wakasemezana wao kwa wao, “Njooni, tufyatue matofali na tuyachome vizuri kwa moto.” Walitumia matofali badala ya mawe, na lami kwa ajili ya kushikamanishia hayo matofali. 4 11:4Ndipo wakasema, “Njooni, tujijengee mji wenye mnara ambao utafika hadi mbinguni, ili tujipatie jina tusije tukatawanyika usoni pa dunia yote.”

    5 11:5Lakini Bwana akashuka ili auone mji na mnara ambao wanadamu waliokuwa wanaujenga. 6 11:6 Bwana akasema, “Ikiwa kama taifa moja wanaozungumza lugha moja wameanza kufanya hili, basi hakuna lolote watakalopanga kufanya ambalo halitawezekana kwao. 7 11:7Njooni, tushuke tuvuruge lugha yao ili wasielewane wao kwa wao.”

    8 11:8Hivyo Bwana akawatawanya kutoka mahali pale kwenda katika dunia yote, nao wakaacha kuujenga huo mji. 9 11:9Ndiyo maana pakaitwa Babeli, kwa sababu hapo ndipo Bwana alipoivuruga lugha ya dunia nzima. Kutoka hapo Bwana akawatawanya katika uso wa dunia yote.

    Shemu Hadi Abramu (1 Nyakati 1:24-27)

    10 11:10Hivi ndivyo vizazi vya Shemu.

    Miaka miwili baada ya gharika, Shemu alipokuwa na miaka 100, akamzaa Arfaksadi. 11 11:11Baada ya kumzaa Arfaksadi, Shemu aliishi miaka 500, akazaa watoto wengine wa kiume na wa kike.

    12 11:12Wakati Arfaksadi alipokuwa na miaka thelathini na mitano, akamzaa Shela. 13 11:13Baada ya Arfaksadi kumzaa Shela, aliishi miaka 403, akazaa watoto wengine wa kiume na wa kike.

    14 11:14Shela alipokuwa na miaka thelathini, akamzaa Eberi. 15 11:15Shela baada ya kumzaa Eberi, aliishi miaka 403, akazaa watoto wengine wa kiume na wa kike.

    16 11:16Eberi alipokuwa na miaka thelathini na minne, akamzaa Pelegi. 17 11:17Baada ya Eberi kumzaa Pelegi, aliishi miaka 430, akazaa watoto wengine wa kiume na wa kike.

    18 11:18Pelegi alipokuwa na miaka thelathini, akamzaa Reu. 19 11:19Baada ya Pelegi kumzaa Reu, aliishi miaka 209, akazaa watoto wengine wa kiume na wa kike.

    20 11:20Reu alipokuwa na miaka thelathini na miwili, akamzaa Serugi. 21 11:21Baada ya Reu kumzaa Serugi, aliishi miaka 207, akazaa watoto wengine wa kiume na wa kike.

    22 11:22Serugi alipokuwa na miaka thelathini, akamzaa Nahori. 23 11:23Baada ya Serugi kumzaa Nahori, aliishi miaka 200, akazaa watoto wengine wa kiume na wa kike.

    24 11:24Nahori alipokuwa na miaka ishirini na tisa, akamzaa Tera. 25 11:25Baada ya Nahori kumzaa Tera, aliishi miaka 119, akazaa watoto wengine wa kiume na wa kike.

    26 11:26Tera alipokuwa na miaka sabini, akamzaa Abramu, Nahori na Harani.

    Wazao Wa Tera

    27 11:27Hawa ndio wazao wa Tera.

    Tera aliwazaa Abramu, Nahori na Harani. Harani akamzaa Loti. 28 11:28Tera alipokuwa bado hai, Harani akafa huko Uru ya Wakaldayo, nchi alimozaliwa. 29 11:29Abramu na Nahori walioa. Mke wa Abramu aliitwa Sarai, na mke wa Nahori aliitwa Milka; Milka na Iska walikuwa watoto wa Harani. 30 11:30Sarai alikuwa tasa, hakuwa na watoto.

    31 11:31Tera akamchukua Abramu mwanawe, Loti mwana wa Harani mwanawe, na Sarai mkwewe, mke wa Abramu mwanawe, wakatoka kwa pamoja katika Uru ya Wakaldayo kwenda nchi ya Kanaani. Lakini walipofika Harani, wakaishi huko.

    32 11:32Tera alikufa huko Harani akiwa na miaka 205.

    12Wito Wa Abramu

    1 12:1 Bwana akawa amemwambia Abramu, “Ondoka kutoka nchi yako, uache jamii yako na nyumba ya baba yako, uende hadi nchi nitakayokuonyesha.

    2 12:2“Mimi nitakufanya taifa kubwa na nitakubariki, Nitalikuza jina lako, nawe utakuwa baraka. 3 12:3Nitawabariki wale wanaokubariki, na yeyote akulaaniye nitamlaani; na kupitia kwako mataifa yote duniani yatabarikiwa.”

    4 12:4Hivyo Abramu akaondoka kama Bwana alivyokuwa amemwambia; naye Loti akaondoka pamoja naye. Wakati Abramu alipoitwa aondoke Harani, alikuwa na miaka sabini na mitano. 5 12:5Abramu akamchukua Sarai mkewe pamoja na Loti mwana wa ndugu yake, mali zote walizokuwa nazo pamoja na watu aliokuwa amewapata huko Harani, wakasafiri mpaka nchi ya Kanaani, wakafika huko.

    6 12:6Abramu akasafiri katika nchi hiyo akafika huko Shekemu, mahali penye mti wa mwaloni ulioko More. Wakati huo Wakanaani walikuwa wanaishi katika nchi hiyo. 7 12:7 Bwana akamtokea Abramu, akamwambia, “Nitawapa uzao wako nchi hii.” Hivyo hapa akamjengea madhabahu Bwana aliyekuwa amemtokea.

    8 12:8Kutoka huko Abramu akasafiri kuelekea kwenye vilima mashariki ya Betheli, naye akapiga hema huko, Betheli ikiwa upande wa magharibi na Ai upande wa mashariki. Huko alimjengea Bwana madhabahu na akaliitia jina la Bwana. 9 12:9Kisha Abramu akasafiri kuelekea upande wa Negebu.

    Abramu Katika Nchi Ya Misri

    10 12:10Basi kulikuwako na njaa katika nchi, naye Abramu akashuka kwenda Misri kukaa huko kwa muda, kwa maana njaa ilikuwa kali. 11 12:11Alipokuwa karibu kuingia Misri, akamwambia Sarai mkewe, “Ninajua ya kwamba wewe ni mwanamke mzuri wa sura. 12 12:12Wakati Wamisri watakapokuona, watasema, ‘Huyu ni mke wake.’ Ndipo wataniua, lakini wewe watakuacha hai. 13 12:13Sema wewe ni dada yangu, ili nitendewe mema kwa ajili yako, na maisha yangu yatahifadhiwa kwa sababu yako.”

    14 12:14Abramu alipoingia Misri, Wamisri wakamwona Sarai kuwa ni mwanamke mzuri sana wa sura. 15 12:15Maafisa wa Farao walipomwona, wakamsifia kwa Farao; ndipo Sarai akapelekwa kwa nyumba ya mfalme. 16 12:16Kwa ajili ya Sarai, Farao akamtendea Abramu mema, naye Abramu akapata kondoo, ngʼombe, punda, ngamia na watumishi wa kiume na wa kike.

    17 12:17Lakini Bwana akamwadhibu Farao na nyumba yake kwa maradhi ya kufisha kwa sababu ya kumchukua Sarai, mke wa Abramu. 18 12:18Ndipo Farao akamwita Abramu, akamuuliza, “Umenifanyia nini? Kwa nini hukuniambia ni mke wako? 19 12:19Kwa nini ulisema, ‘Yeye ni dada yangu,’ hata nikamchukua kuwa mke wangu? Sasa basi, mke wako huyu hapa. Mchukue uende zako!” 20 12:20Kisha Farao akawapa watu wake amri kuhusu Abramu, wakamsindikiza pamoja na mke wake na kila alichokuwa nacho.

    13Abramu Na Loti Watengana

    1 13:1Hivyo Abramu akakwea kutoka Misri kwenda Negebu, yeye na mkewe na kila kitu alichokuwa nacho, pia Loti akaenda pamoja naye. 2 13:2Wakati huo Abramu alikuwa tajiri sana wa mifugo, fedha na dhahabu.

    3 13:3Kutoka Negebu, akapita mahali hadi mahali, hadi akafika Betheli, mahali hapo ambapo mwanzoni alipiga hema lake kati ya Betheli na Ai 4 13:4hapo ambapo alikuwa amejenga madhabahu ya kwanza. Huko Abramu akaliitia jina la Bwana.

    5 13:5Basi Loti, ambaye alikuwa anafuatana na Abramu, alikuwa pia na makundi ya mbuzi, kondoo, ngʼombe na mahema. 6 13:6Lakini nchi haikuwatosha kukaa pamoja kwa ajili ya wingi wa mali zao. 7 13:7Ukazuka ugomvi kati ya wachunga mifugo wa Abramu na wale wa Loti. Wakati huo, Wakanaani na Waperizi ndio waliokuwa wenyeji wa nchi hiyo.

    8 13:8Hivyo Abramu akamwambia Loti, “Pasiwe na ugomvi wowote kati yangu na wewe, wala kati ya wachungaji wangu na wako, kwa kuwa sisi ni ndugu. 9 13:9Je, nchi yote haiko mbele yako? Tutengane. Kama ukielekea kushoto, nitakwenda kulia; kama ukielekea kulia, mimi nitakwenda kushoto.”

    10 13:10Loti akatazama akaona lile bonde lote la Yordani kuwa lilikuwa na maji tele, kama bustani ya Bwana, kama nchi ya Misri, kuelekea Soari. (Hii ilikuwa kabla Bwana hajaharibu Sodoma na Gomora.) 11 13:11Hivyo Loti akajichagulia bonde lote la Yordani, akaelekea upande wa mashariki. Watu hao wawili wakatengana: 12 13:12Abramu akaishi katika nchi ya Kanaani, wakati Loti aliishi miongoni mwa miji ya lile bonde na kupiga mahema yake karibu na Sodoma. 13 13:13Basi watu wa Sodoma walikuwa waovu, wakifanya sana dhambi dhidi ya Bwana.

    14 13:14Baada ya Loti kuondoka Bwana akamwambia Abramu, “Ukiwa hapo ulipo, inua macho yako utazame kaskazini na kusini, mashariki na magharibi. 15 13:15Nchi yote unayoiona nitakupa wewe na uzao wako hata milele. 16 13:16Nitaufanya uzao wako uwe mwingi kama mavumbi ya nchi, hivyo kama kuna yeyote awezaye kuhesabu mavumbi, basi uzao wako utahesabika. 17 13:17Ondoka, tembea katika marefu na mapana ya nchi, kwa maana ninakupa wewe.”

    18 13:18Basi Abramu akaondoa mahema yake, akaenda kuishi karibu na mialoni ya Mamre huko Hebroni, huko akamjengea Bwana madhabahu.

    14Abramu Amwokoa Loti

    1 14:1Wakati huu Amrafeli mfalme wa Shinari, Arioko mfalme wa Elasari, Kedorlaoma mfalme wa Elamu, na Tidali mfalme wa Goimu 2 14:2kwa pamoja walikwenda kupigana vita dhidi ya Bera mfalme wa Sodoma, Birsha mfalme wa Gomora, Shinabu mfalme wa Adma, Shemeberi mfalme wa Seboimu, na mfalme wa Bela (yaani Soari). 3 14:3Hawa wote waliotajwa mwishoni waliunganisha majeshi yao kutoka Bonde la Sidimu (yaani Bahari ya Chumvi). 4 14:4Walikuwa wametawaliwa na Mfalme Kedorlaoma kwa miaka kumi na miwili, lakini mwaka wa kumi na tatu waliasi.

    5 14:5Mnamo mwaka wa kumi na nne, Mfalme Kedorlaoma na wafalme waliojiunga naye walikwenda kupigana na kuwashinda Warefai katika Ashtaroth-Kanaimu, Wazuzi katika Hamu, Waemi katika Shawe-Kiriathaimu, 6 14:6na Wahori katika nchi ya kilima cha Seiri, hadi El-Parani karibu na jangwa. 7 14:7Kisha wakarudi wakaenda En-Misfati (yaani Kadeshi), wakashinda nchi yote ya Waamaleki, pamoja na Waamori waliokuwa wakiishi Hasason-Tamari.

    8 14:8Ndipo mfalme wa Sodoma, mfalme wa Gomora, mfalme wa Adma, mfalme wa Seboimu, na mfalme wa Bela (yaani Soari) wakatoka kupanga majeshi yao kwenye Bonde la Sidimu 9 14:9dhidi ya Kedorlaoma, mfalme wa Elamu, Tidali mfalme wa Goimu, Amrafeli mfalme wa Shinari, na Arioko mfalme wa Elasari, yaani wafalme wanne dhidi ya wafalme watano. 10 14:10Basi Bonde la Sidimu lilikuwa limejaa mashimo ya lami, nao wafalme wa Sodoma na wa Gomora walipokimbia, baadhi ya watu walitumbukia huko na wengine wakakimbilia vilimani. 11 14:11Wale wafalme wanne wakateka mali yote ya Sodoma na Gomora pamoja na vyakula vyao vyote, kisha wakaenda zao. 12 14:12Pia walimteka Loti mwana wa ndugu yake Abramu pamoja na mali zake, kwa kuwa alikuwa akiishi Sodoma.

    13 14:13Mtu mmoja aliyekuwa ametoroka akaja kumpa Abramu Mwebrania taarifa. Wakati huu Abramu alikuwa anaishi karibu na mialoni ya Mamre Mwamori, aliyekuwa ndugu yake Eshkoli na Aneri, ambao wote walikuwa wameungana na Abramu. 14 14:14Abramu alipopata habari kwamba jamaa yake amechukuliwa mateka, akawaita watu 318 wa nyumbani mwake waliokuwa wamefunzwa kupigana vita, wakawafuatilia hadi Dani. 15 14:15Wakati wa usiku Abramu aliwagawa watu wake katika vikosi ili awashambulie, na akawafuatilia, akawafukuza hadi Hoba, kaskazini ya Dameski. 16 14:16Akarudisha mali zote, na akamrudisha Loti jamaa yake na mali zake, pamoja na wanawake na watu wengine.

    17 14:17Abramu aliporudi baada ya kumshinda Mfalme Kedorlaoma na wale wafalme waliojiunga naye, mfalme wa Sodoma akatoka kwenda kumlaki katika Bonde la Shawe (yaani Bonde la Mfalme).

    18 14:18Ndipo Melkizedeki mfalme wa Salemu alipoleta mkate na divai. Alikuwa kuhani wa Mungu Aliye Juu Sana. 19 14:19Naye akambariki Abramu, akisema,

    “Abarikiwe Abramu na Mungu Aliye Juu Sana, Muumba wa mbingu na nchi. 20 14:20Abarikiwe Mungu Aliye Juu Sana, ambaye amewaweka adui zako mkononi mwako.” Ndipo Abramu akampa Melkizedeki sehemu ya kumi ya kila kitu.

    21 14:21Mfalme wa Sodoma akamwambia Abramu, “Nipe hao watu na hizo mali uchukue wewe mwenyewe.”

    22 14:22Lakini Abramu akamwambia mfalme wa Sodoma, “Nimeinua mkono wangu kwa Bwana, Mungu Aliye Juu Sana, Muumba wa mbingu na dunia, na nimeapa 23 14:23kwamba sitapokea kitu chochote kilicho chako, hata kama ni uzi au gidamu ya kiatu, ili kamwe usije ukasema, ‘Nimemtajirisha Abramu.’ 24 14:24Sitapokea chochote, ila kile tu watu wangu walichokula na sehemu ambayo ni fungu la watu waliokwenda pamoja nami, ambao ni Aneri, Eshkoli na Mamre. Wao na wapewe fungu lao.”

    15Agano La Mungu Na Abramu

    1 15:1Baada ya jambo hili, neno la Bwana likamjia Abramu katika maono:

    “Usiogope, Abramu. Mimi ni ngao yako, na thawabu yako kubwa sana.”

    2 15:2Lakini Abramu akasema, “Ee Bwana Mwenyezi, utanipa nini na mimi sina hata mtoto na atakayerithi nyumba yangu ni huyu Eliezeri Mdameski?” 3 15:3Abramu akasema, “Hukunipa watoto, hivyo mtumishi katika nyumba yangu ndiye atakuwa mrithi wangu.”

    4 15:4Ndipo neno la Bwana lilipomjia: “Mtu huyu hatakuwa mrithi wako, bali mwana atakayetoka katika viuno vyako mwenyewe ndiye atakayekuwa mrithi wako.” 5 15:5Akamtoa nje na kusema, “Tazama juu kuelekea mbinguni na uhesabu nyota, kama hakika utaweza kuzihesabu.” Ndipo akamwambia, “Hivyo ndivyo uzao wako utakavyokuwa.”

    6 15:6Abramu akamwamini Bwana, naye kwake hili likahesabiwa kuwa haki.

    7 15:7Pia akamwambia, “Mimi ndimi Bwana, niliyekutoa toka Uru ya Wakaldayo nikupe nchi hii uimiliki.”

    8 15:8Lakini Abramu akasema, “Ee Bwana Mwenyezi, nitawezaje kujua kwamba nitapata kuimiliki?”

    9 15:9Ndipo Bwana akamwambia, “Niletee mtamba wa ngʼombe, mbuzi na kondoo dume, kila mmoja wa miaka mitatu, pamoja na hua na kinda la njiwa.”

    10 15:10Abramu akamletea hivi vyote, akampasua kila mnyama vipande viwili, akavipanga kila kimoja kuelekea mwenzake, lakini hata hivyo ndege, hakuwapasua vipande viwili. 11 15:11Kisha ndege walao nyama wakatua juu ya mizoga, lakini Abramu akawafukuza.

    12 15:12Wakati jua lilipokuwa linatua, Abramu akashikwa na usingizi mzito, giza nene na la kutisha likaja juu yake. 13 15:13Kisha Bwana akamwambia, “Ujue hakika kwamba wazao wako watakuwa wageni kwenye nchi ambayo si yao, nao watafanywa watumwa na kuteswa kwa miaka mia nne. 14 15:14Lakini nitaliadhibu taifa lile watakalolitumikia kama watumwa, na baadaye watatoka huko na mali nyingi. 15 15:15Wewe, hata hivyo utakwenda kwa baba zako kwa amani na kuzikwa katika uzee mwema. 16 15:16Katika kizazi cha nne wazao wako watarudi hapa, kwa maana dhambi ya Waamori bado haijafikia kipimo kilichojaa.”

    17 15:17Wakati jua lilipokuwa limezama na giza limeingia, tanuru la moshi na mwali wa moto unaowaka vikatokea na kupita kati ya vile vipande vya nyama. 18 15:18Siku hiyo Bwana akafanya Agano na Abramu, na kumwambia, “Nitawapa wazao wako nchi hii, kuanzia Kijito cha Misri 15:18 Kijito cha Misri hapa ina maana Wadi-el-Arish kwenye mpaka wa kusini wa Yuda. hadi mto ule mkubwa, Frati, 19 15:19yaani nchi ya Wakeni, Wakenizi, Wakadmoni, 20 15:20Wahiti, Waperizi, Warefai, 21 15:21Waamori, Wakanaani, Wagirgashi na Wayebusi.”

    16Hagari Na Ishmaeli

    1 16:1Basi Sarai, mkewe Abramu, alikuwa hajamzalia watoto. Lakini alikuwa na mtumishi wa kike Mmisri jina lake Hagari, 2 16:2hivyo Sarai akamwambia Abramu, “Bwana amenizuilia kupata watoto. Nenda, ukakutane kimwili na mtumishi wangu wa kike, huenda nitaweza kupata watoto kupitia kwake.”

    Abramu akakubaliana na lile Sarai alilosema. 3 16:3Hivyo baada ya Abramu kuishi katika nchi ya Kanaani miaka kumi, Sarai akamchukua mtumishi wake wa kike wa Kimisri, Hagari na kumpa mumewe awe mke wake. 4 16:4Akakutana kimwili na Hagari, naye akapata mimba.

    Hagari alipojua kuwa ana mimba, alianza kumdharau Sarai. 5 16:5Ndipo Sarai akamwambia Abramu, “Unawajibika na manyanyaso ninayoyapata. Nilimweka mtumishi wangu mikononi mwako, sasa kwa vile anajua kwamba ana mimba, ananidharau mimi. Bwana na aamue kati yako na mimi.”

    6 16:6Abramu akamwambia, “Mtumishi wako yuko mikononi mwako. Mtendee lolote unalofikiri ni bora zaidi.” Ndipo Sarai akamtesa Hagari, hivyo akamtoroka.

    7 16:7Malaika wa Bwana akamkuta Hagari karibu na chemchemi huko jangwani; ilikuwa chemchemi ile iliyokuwa kando ya barabara iendayo Shuri. 8 16:8Malaika akamwambia, “Hagari, mtumishi wa Sarai, umetokea wapi, na unakwenda wapi?”

    Akamjibu, “Ninamkimbia bibi yangu Sarai.”

    9 16:9Ndipo malaika wa Bwana akamwambia, “Rudi kwa bibi yako ukajishushe chini yake.” 10 16:10Malaika akaendelea akasema, “Nitazidisha wazao wako, hivi kwamba watakuwa wengi mno wasiohesabika.”

    11 16:11Pia malaika wa Bwana akamwambia:

    “Wewe sasa una mimba nawe utamzaa mwana. Utamwita jina lake Ishmaeli, 16:11 Ishmaeli maana yake Mungu husikia. kwa sababu Bwana amesikia juu ya huzuni yako. 12 16:12Atakuwa punda-mwitu katikati ya wanadamu, mkono wake utakuwa dhidi ya kila mtu na mkono wa kila mtu dhidi yake, naye ataishi kwa uhasama na ndugu zake wote.”

    13 16:13Hagari akampa Bwana aliyezungumza naye jina hili: “Wewe ndiwe Mungu unionaye mimi,” kwa maana alisema, “Sasa nimemwona yeye anayeniona mimi.” 14 16:14Ndiyo sababu kisima kile kikaitwa Beer-Lahai-Roi, 16:14 Beer-Lahai-Roi maana yake Yeye Aliye Hai Anionaye Mimi. ambacho bado kipo huko hata leo kati ya Kadeshi na Beredi.

    15 16:15Hivyo Hagari akamzalia Abramu mwana, naye Abramu akamwita huyo mwana Hagari aliyemzalia, Ishmaeli. 16 16:16Abramu alikuwa na umri wa miaka themanini na sita wakati Hagari alipomzalia Ishmaeli.

    17Agano La Tohara

    1 17:1Abramu alipokuwa na miaka tisini na tisa, Bwana akamtokea akamwambia, “Mimi ndimi Mungu Mwenyezi; 17:1 Mungu Mwenyezi hapa ni jina la Kiebrania, El-Shaddai (yaani Mungu Mwenye utoshelevu wote). enenda mbele zangu na uishi kwa unyofu. 2 17:2Nami nitafanya Agano langu kati yangu na wewe, nami nitakuzidisha sana sana.”

    3 17:3Abramu akaanguka kifudifudi, naye Mungu akamwambia, 4 17:4“Kwa upande wangu, hili ndilo Agano langu na wewe: Wewe utakuwa baba wa mataifa mengi. 5 17:5Jina lako hutaitwa tena Abramu, bali jina lako litakuwa Abrahamu, 17:5 Abrahamu maana yake Baba wa watu wengi. kwa maana nimekufanya wewe baba wa mataifa mengi. 6 17:6Nitakufanya uwe na uzao mwingi sana, kwako yatatoka mataifa nao wafalme watatoka kwako. 7 17:7Nitalithibitisha Agano langu kama Agano la milele kati yangu na wewe na wazao wako baada yako na vizazi vijavyo niwe Mungu wako na Mungu wa wazao wako. 8 17:8Nchi yote ya Kanaani, unakoishi sasa kama mgeni, nitakupa kuwa milki yako milele, na uzao wako, nami nitakuwa Mungu wao.”

    9 17:9Ndipo Mungu akamwambia Abrahamu, “Kwa upande wako, lazima ushike Agano langu, wewe na wazao wako kwa ajili ya vizazi vijavyo. 10 17:10Hili ni Agano langu na wewe pamoja na wazao wako baada yako, Agano mtakalolishika: Kila mwanaume miongoni mwenu atatahiriwa. 11 17:11Mtafanyiwa tohara na hii itakuwa ni alama ya Agano kati yangu na ninyi. 12 17:12Kwa vizazi vijavyo, kila mwanaume miongoni mwenu mwenye siku nane ni lazima atahiriwe, pamoja na watakaozaliwa nyumbani mwako au walionunuliwa kwa fedha kutoka kwa mgeni, wale ambao sio watoto wako. 13 17:13Awe amezaliwa nyumbani mwako au amenunuliwa kwa fedha yako, ni lazima watahiriwe. Agano langu katika mwili wako litakuwa ni Agano la milele. 14 17:14Kila mwanaume asiyetahiriwa, ambaye hajapata tohara ya mwilini, atatengwa na watu wake, amelivunja Agano langu.”

    15 17:15Pia Bwana akamwambia Abrahamu, “Kwa upande wa Sarai mkeo, hutamwita tena Sarai bali jina lake litakuwa Sara. 16 17:16Nitambariki na hakika nitakupatia mwana kwake. Nitambariki na kwamba atakuwa mama wa mataifa, wafalme wa mataifa watatoka kwake.”

    17 17:17Abrahamu akaanguka kifudifudi, akacheka na kusema moyoni mwake, “Je, mtu wa miaka mia moja aweza kuzaa mwana? Je, Sara atazaa mtoto katika umri wa miaka tisini?” 18 17:18Abrahamu akamwambia Mungu, “Laiti Ishmaeli naye angeshiriki baraka yako!”

    19 17:19Ndipo Mungu akasema, “Ndiyo, lakini mkeo Sara atakuzalia wewe mwana, nawe utamwita jina lake Isaki. 17:19 Isaki maana yake Kucheka. Nitalithibitisha Agano langu naye kama Agano la milele kwa ajili yake na wazao wake baada yake. 20 17:20Kwa upande wa Ishmaeli, nimekusikia: hakika nitambariki, nitamfanya awe na uzao mwingi na nitaongeza sana idadi yake. Atakuwa baba wa watawala kumi na wawili, nami nitamfanya awe taifa kubwa. 21 17:21Lakini Agano langu nitalithibitisha kwa Isaki, ambaye Sara atakuzalia mwaka ujao majira kama haya.” 22 17:22Wakati alipomaliza kuzungumza na Abrahamu, Mungu akapanda juu akaondoka kwa Abrahamu.

    23 17:23Siku ile ile, Abrahamu akamchukua Ishmaeli mwanawe na wote waliozaliwa nyumbani mwake pamoja na walionunuliwa kwa fedha zake, kila mwanaume wa nyumbani mwake, akawatahiri, kama Mungu alivyomwagiza. 24 17:24Abrahamu alikuwa na umri wa miaka tisini na tisa alipotahiriwa, 25 17:25naye Ishmaeli mwanawe alitahiriwa akiwa na umri wa miaka kumi na mitatu. 26 17:26Abrahamu na Ishmaeli mwanawe walitahiriwa siku ile ile, 27 17:27Kila mwanaume nyumbani mwa Abrahamu, pamoja na wote waliozaliwa nyumbani mwake au aliyenunuliwa kwa fedha kutoka kwa mgeni, alitahiriwa pamoja naye.

    18Wageni Watatu

    1 18:1 Bwana akamtokea Abrahamu karibu na mialoni ya Mamre wakati alipokuwa ameketi kwenye ingilio la hema lake wakati wa adhuhuri. 2 18:2Abrahamu akainua macho akaona watu watatu wamesimama karibu naye. Alipowaona, aliharakisha kutoka kwenye ingilio la hema lake kuwalaki na kuwasujudia hadi nchi.

    3 18:3Akasema, “Kama nimepata kibali machoni penu, ee bwana wangu, usimpite mtumishi wako. 4 18:4Acha yaletwe maji kidogo, kisha ninyi nyote mnawe miguu yenu na mpumzike chini ya mti huu. 5 18:5Niruhusuni niwapatie chakula kidogo mle, ili mpate nguvu mwendelee na safari yenu, kwa kuwa mmekuja kwa mtumishi wenu.”

    Nao wakamjibu, “Vema sana, fanya kama unavyosema.”

    6 18:6Hivyo Abrahamu akaharakisha akaingia hemani kwa Sara, akamwambia, “Chukua vipimo vitatu vya unga laini haraka, ukande na uoke mikate.”

    7 18:7Kisha Abrahamu akakimbia kwenda kwenye kundi, akachagua ndama mzuri, laini na akampa mtumishi, ambaye aliharakisha kumtayarisha. 8 18:8Kisha akaleta jibini, maziwa na nyama ya yule ndama iliyoandaliwa, akaviweka mbele ya wageni. Walipokuwa wakila, alisimama karibu nao chini ya mti.

    9 18:9Wakamuuliza, “Yuko wapi Sara mkeo?”

    Akasema, “Yuko huko, ndani ya hema.”

    10 18:10Kisha Bwana akasema, “Hakika nitakurudia tena majira kama haya mwakani na Sara mkeo atakuwa ana mwana.”

    Sara alikuwa akiwasikiliza kwenye ingilio la hema, lililokuwa nyuma yake. 11 18:11Abrahamu na Sara walikuwa wazee tena waliosogea miaka, naye Sara alikuwa amekoma katika desturi ya wanawake. 12 18:12Hivyo Sara akacheka kimoyomoyo alipokuwa akiwaza, “Baada ya mimi kuwa mkongwe hivi na bwana wangu amezeeka, je, nitaweza kufurahia jambo hili?”

    13 18:13Ndipo Bwana akamwambia Abrahamu, “Kwa nini Sara amecheka na kusema, ‘Kweli nitazaa mtoto nami sasa ni mzee?’ 14 18:14Je, kuna jambo lolote gumu lisilowezekana kwa Bwana? Nitakurudia mwakani majira kama haya, naye Sara atakuwa na mwana.”

    15 18:15Sara akaogopa kwa kuwa alidanganya na kusema, “Mimi sikucheka.”

    Lakini Bwana akasema, “Ndiyo, ulicheka!”

    Abrahamu Aiombea Sodoma

    16 18:16Wakati watu hao waliposimama ili waondoke, walielekeza nyuso zao Sodoma, Abrahamu akawatoa kitambo kidogo ili awasindikize. 17 18:17Ndipo Bwana akasema, “Je, nimfiche Abrahamu jambo ninalokusudia kufanya? 18 18:18Hakika Abrahamu atakuwa taifa kubwa na lenye nguvu, kupitia kwake mataifa yote ya dunia yatabarikiwa. 19 18:19Kwa maana nimemchagua yeye, ili awaongoze watoto wake na jamaa yake kufuata njia ya Bwana, kwa kuwa waadilifu na kutenda haki, ili Bwana atimize ahadi yake kwa Abrahamu.”

    20 18:20Basi Bwana akasema, “Kilio dhidi ya Sodoma na Gomora ni kikubwa sana na dhambi yao inasikitisha sana, 21 18:21kwamba nitashuka nione kama waliyoyatenda ni mabaya kiasi cha kilio kilichonifikia. Kama sivyo, nitajua.”

    22 18:22Basi wale watu wakageuka wakaenda kuelekea Sodoma, lakini Abrahamu akabaki amesimama mbele za Bwana. 23 18:23Ndipo Abrahamu akamsogelea akasema: “Je, utawaangamiza wenye haki na waovu? 24 18:24Je, ikiwa watakuwepo watu wenye haki hamsini katika mji huo, hivi kweli utauangamiza na wala hutauacha kwa ajili ya hao watu hamsini wenye haki waliomo ndani yake? 25 18:25Hilo na liwe mbali nawe, kufanya jambo kama hilo, kuwaua wenye haki pamoja na waovu, kuwatendea wenye haki sawasawa na waovu. Iwe mbali nawe! Je, Mwamuzi wa dunia yote hatafanya lililo sawa?”

    26 18:26 Bwana akasema, “Kama nikipata watu hamsini wenye haki katika mji wa Sodoma, nitausamehe huo mji wote kwa ajili yao.”

    27 18:27Kisha Abrahamu akasema tena: “Sasa kwa kuwa nimekuwa na ujasiri wa kuzungumza na Bwana, ingawa mimi si kitu bali ni mavumbi na majivu; 28 18:28je, kama hesabu ya wenye haki imepungua watano katika hamsini, utauangamiza huo mji wote kwa ajili ya hao watano waliopungua?”

    Bwana akamwambia, “Kama nikiwakuta huko watu arobaini na watano, sitauangamiza.”

    29 18:29Abrahamu akazungumza naye kwa mara nyingine, “Je, kama huko watapatikana watu arobaini tu?”

    Akamjibu, “Kwa ajili ya hao arobaini, sitauangamiza.”

    30 18:30Ndipo akasema, “Bwana na asikasirike, lakini niruhusu nizungumze. Je, kama huko watakuwepo thelathini tu?”

    Akajibu, “Sitapaangamiza ikiwa nitawakuta huko watu thelathini.”

    31 18:31Abrahamu akasema, “Sasa kwa kuwa nimekuwa na ujasiri sana kuzungumza na Bwana, je, kama wakipatikana huko watu ishirini tu?”

    Bwana akajibu, “Kwa ajili ya hao ishirini, sitauangamiza.”

    32 18:32Abrahamu akasema, “Bwana na asikasirike, lakini niruhusu nizungumze tena mara moja tu. Itakuwaje kama watapatikana huko watu kumi tu?”

    Bwana akajibu, “Kwa ajili ya hao kumi, sitauangamiza.”

    33 18:33 Bwana alipomaliza kuzungumza na Abrahamu, akaondoka, naye Abrahamu akarudi nyumbani kwake.

    19Kuangamizwa Kwa Sodoma Na Gomora

    1 19:1Malaika wale wawili wakafika Sodoma wakati wa jioni, naye Loti alikuwa ameketi kwenye lango la mji. Wakati alipowaona, aliondoka kwenda kuwalaki na kuwasujudia hadi chini. 2 19:2Akasema, “Bwana zangu, tafadhali karibuni kwenye nyumba ya mtumishi wenu. Mnaweza kunawa miguu na kulala hapa kisha asubuhi na mapema mwendelee na safari yenu.”

    Wakamjibu, “La hasha, tutalala hapa nje uwanjani.”

    3 19:3Lakini akasisitiza kwa nguvu kwamba waingie pamoja naye nyumbani kwake. Akawaandalia chakula, mikate isiyotiwa chachu, nao wakala. 4 19:4Kabla hawajaenda kulala, watu wote kutoka kila sehemu ya mji wa Sodoma, vijana kwa wazee, waliizunguka nyumba. 5 19:5Wakamwita Loti wakisema, “Wako wapi wale watu ambao walikuja kwako jioni hii? Watoe nje kwetu ili tuweze kuwalawiti.”

    6 19:6Loti akatoka nje kuonana nao, akaufunga mlango nyuma yake, 7 19:7akasema, “La hasha, rafiki zangu. Msifanye jambo hili ovu. 8 19:8Tazama, ninao binti wawili ambao kamwe hawajakutana kimwili na mwanaume. Acha niwatoe nje kwenu, nanyi mnaweza kuwafanyia lolote mnalotaka. Lakini msiwafanyie chochote watu hawa, kwa sababu wako kwenye ulinzi chini ya dari langu.”

    9 19:9Wakamjibu, “Tuondokee mbali.” Wakaendelea kusema, “Huyu mtu alikuja hapa kama mgeni na sasa anataka kuwa mwamuzi wetu! Tutakutenda vibaya kuliko wao.” Waliendelea kumlazimisha Loti na kusonga mbele ili kuvunja mlango.

    10 19:10Lakini watu wale waliokuwa ndani wakanyoosha mkono wakamvuta Loti ndani ya nyumba na kufunga mlango. 11 19:11Kisha wakawapiga kwa upofu wale watu waliokuwa mlangoni mwa ile nyumba, vijana kwa wazee, hivyo hawakuweza kuupata mlango.

    12 19:12Wale watu wawili wakamwambia Loti, “Una mtu mwingine yeyote hapa, wakwe zako, wana au binti, ama yeyote mwingine aliye wako katika mji huu? Waondoe hapa, 13 19:13kwa sababu tunapaangamiza mahali hapa. Kilio kwa Bwana dhidi ya watu wa hapa ni kikubwa kiasi kwamba ametutuma kupaangamiza.”

    14 19:14Kwa hiyo Loti alitoka ili kuzungumza na wakwe zake, waliokuwa wamewaposa binti zake. Akawaambia, “Fanyeni haraka kuondoka mahali hapa, kwa kuwa Bwana yu karibu kuangamiza mji huu!” Lakini wakwe zake walifikiri kwamba alikuwa akitania.

    15 19:15Kunako mapambazuko, malaika wakamhimiza Loti, wakamwambia, “Fanya haraka! Mchukue mke wako na binti zako wawili walioko hapa, la sivyo utaangamizwa wakati mji utakapoadhibiwa.”

    16 19:16Alipositasita, wale watu wakamshika mkono wake na mikono ya mke wake na binti zake wawili na kuwaongoza salama nje ya mji, kwa kuwa Bwana alikuwa na huruma kwao. 17 19:17Mara walipokwisha kuwatoa nje, mmoja wao akawaambia, “Mkimbie kwa usalama wenu! Msitazame nyuma, wala msisimame popote katika nchi tambarare! Kimbilieni milimani, ama sivyo mtaangamizwa!”

    18 19:18Lakini Loti akawajibu, “La hasha, bwana zangu, tafadhalini! 19 19:19Mtumishi wenu amepata kibali mbele ya macho yenu, nanyi mmeonyesha wema mkubwa kwangu kwa kuokoa maisha yangu. Lakini siwezi kukimbilia milimani, janga hili litanikumba, nami nitakufa. 20 19:20Tazama, hapa kuna mji karibu wa kukimbilia, nao ni mdogo. Niruhusuni nikimbilie humo, ni mdogo sana, ama sivyo? Ndipo maisha yangu yatasalimika.”

    21 19:21Akamwambia, “Vema sana, nitalikubali hili ombi pia, sitauangamiza mji ulioutaja. 22 19:22Lakini ukimbilie huko haraka, kwa sababu sitaweza kufanya lolote mpaka ufike huko.” (Ndiyo maana mji huo ukaitwa Soari. 19:22 Soari maana yake Mdogo.)

    23 19:23Wakati Loti alipofika Soari, jua lilikuwa limechomoza katika nchi. 24 19:24Ndipo Bwana akanyesha moto wa kiberiti uliotoka mbinguni kwa Bwana juu ya Sodoma na Gomora. 25 19:25Hivyo akaiteketeza miji ile na eneo lote la tambarare, pamoja na wote waliokuwa wanaishi katika miji, hata pia mimea yote katika nchi. 26 19:26Lakini mke wa Loti akatazama nyuma, hivyo akawa nguzo ya chumvi.

    27 19:27Asubuhi na mapema siku iliyofuata, Abrahamu akaamka na kurudi mahali pale aliposimama mbele za Bwana. 28 19:28Akatazama upande wa Sodoma na Gomora, kuelekea nchi yote ya tambarare, akaona moshi mzito ukipanda kutoka kwenye nchi, kama moshi utokao kwenye tanuru.

    29 19:29Kwa hiyo Mungu alipoiangamiza miji ya tambarare alimkumbuka Abrahamu, akamtoa Loti kutoka kwenye lile janga lililoharibu miji ile ambamo Loti alikuwa ameishi.

    Loti Na Binti Zake

    30 19:30Loti na binti zake wawili waliondoka Soari na kufanya makao yao kule milimani, kwa maana aliogopa kukaa Soari. Yeye na binti zake wawili waliishi katika pango. 31 19:31Siku moja binti mkubwa akamwambia yule mdogo, “Baba yetu ni mzee na hakuna mwanaume mahali hapa atakayekutana na sisi kimwili, kama ilivyo desturi ya mahali pote duniani. 32 19:32Tumnyweshe baba yetu mvinyo kisha tukutane naye kimwili ili tuhifadhi uzao wetu kupitia baba yetu.”

    33 19:33Usiku ule walimnywesha baba yao mvinyo, alipolewa binti yake mkubwa akaingia na kukutana naye kimwili. Baba yao hakujua wakati binti yake alipoingia kulala naye wala alipotoka.

    34 19:34Siku iliyofuata binti mkubwa akamwambia yule mdogo, “Usiku uliopita mimi nilikutana kimwili na baba yangu. Tumnyweshe divai tena, usiku huu nawe ukutane naye kimwili ili tuweze kuhifadhi uzao wetu kupitia baba yetu.” 35 19:35Kwa hiyo wakamnywesha baba yao mvinyo tena usiku ule, naye binti yake mdogo akaingia, akakutana naye kimwili. Kwa mara nyingine baba yao hakujua binti yake alipolala naye wala alipoondoka.

    36 19:36Hivyo binti wawili wa Loti wakapata mimba kwa baba yao. 37 19:37Binti mkubwa akamzaa mwana, akamwita jina lake Moabu; ndio baba wa Wamoabu hata leo. 38 19:38Binti mdogo naye pia akamzaa mwana, naye akamwita Benami; ndiye baba wa Waamoni hata leo.

    20Abrahamu Na Abimeleki

    1 20:1Basi Abrahamu akaendelea mbele kutoka huko hadi nchi ya Negebu na akaishi kati ya Kadeshi na Shuri. Kwa muda mfupi alikaa Gerari kama mgeni, 2 20:2huko Abrahamu akasema kuhusu Sara mkewe, “Huyu ni dada yangu.” Kisha Abimeleki mfalme wa Gerari akatuma Sara aletwe, naye akamchukua.

    3 20:3Lakini Mungu akamjia Abimeleki katika ndoto wakati wa usiku na kumwambia, “Wewe ni kama mfu kwa sababu ya huyu mwanamke uliyemchukua; yeye ni mke wa mtu.”

    4 20:4Wakati huo Abimeleki alikuwa bado hajamsogelea, kwa hiyo akasema, “Je, Bwana utaliharibu taifa lisilo na hatia? 5 20:5Hakusema kwangu, ‘Huyu ni dada yangu,’ naye Sara pia hakusema, ‘Huyu ni kaka yangu’? Nimefanya haya kwa dhamiri njema na mikono safi.”

    6 20:6Kisha Mungu akamwambia katika ndoto, “Ndiyo, najua ya kwamba umefanya haya kwa dhamiri safi, kwa hiyo nimekuzuia usinitende dhambi. Ndiyo sababu sikukuacha umguse. 7 20:7Sasa umrudishe huyo mke wa mtu, kwa maana ni nabii, naye atakuombea nawe utaishi. Lakini kama hutamrudisha, ujue kwa hakika kuwa wewe na watu wako wote mtakufa.”

    8 20:8Kesho yake asubuhi na mapema Abimeleki akawaita maafisa wake wote, na baada ya kuwaambia yote yaliyotokea, waliogopa sana. 9 20:9Kisha Abimeleki akamwita Abrahamu na kumwambia, “Wewe umetufanyia nini? Nimekukosea nini hata ukaleta hatia kubwa namna hii juu yangu na ufalme wangu? Umenifanyia mambo ambayo hayakupasa kufanyika.” 10 20:10Abimeleki akamuuliza Abrahamu, “Ulikuwa na kusudi gani kufanya hivi?”

    11 20:11Abrahamu akajibu, “Niliwaza kwamba, ‘Hakika hakuna hofu ya Mungu mahali hapa, nao wataniua kwa sababu ya mke wangu.’ 12 20:12Pamoja na hayo, ni kweli kwamba yeye ni dada yangu, binti wa baba yangu ingawa si mtoto wa mama yangu; basi akawa mke wangu. 13 20:13Wakati Bwana aliponifanya nisafiri mbali na nyumbani mwa baba yangu, nilimwambia, ‘Hivi ndivyo utakavyoonyesha pendo lako kwangu: Kila mahali tutakapokwenda, kuhusu mimi sema, “Huyu ni kaka yangu.” ’ ”

    14 20:14Kisha Abimeleki akatwaa kondoo na ngʼombe, na watumwa wa kiume na wa kike akampa Abrahamu, akamrudisha Sara kwa mumewe. 15 20:15Abimeleki akasema, “Nchi yangu iko mbele yako, ishi popote unapotaka.”

    16 20:16Akamwambia Sara, “Ninampa kaka yako shekeli elfu moja za fedha. Hii ni kufidia kosa lililofanyika dhidi yako mbele ya wote walio pamoja nawe; haki yako imethibitishwa kabisa.”

    17 20:17Kisha Abrahamu akamwomba Mungu, naye Mungu akamponya Abimeleki, mke wake, na watumwa wake wa kike kwamba waweze kupata watoto tena, 18 20:18kwa kuwa Bwana alikuwa ameyafunga matumbo ya wote katika nyumba ya Abimeleki kwa sababu ya Sara, mke wa Abrahamu.

    21Kuzaliwa Kwa Isaki

    1 21:1Wakati huu Bwana akamrehemu Sara kama alivyokuwa amesema, naye Bwana akamtendea Sara kile alichokuwa ameahidi. 2 21:2Sara akapata mimba, akamzalia Abrahamu mwana katika uzee wake, majira yale ya Mungu aliomwahidi. 3 21:3Abrahamu akamwita Isaki yule mwana ambaye Sara alimzalia. 4 21:4Isaki alipokuwa na umri wa siku nane, Abrahamu akamtahiri, kama Mungu alivyomwamuru. 5 21:5Abrahamu alikuwa na miaka 100 wakati Isaki mwanawe alipozaliwa.

    6 21:6Sara akasema, “Mungu ameniletea kicheko, kila mmoja atakayesikia jambo hili atacheka pamoja nami.” 7 21:7Akaongeza kusema, “Nani angemwambia Abrahamu kuwa Sara angenyonyesha watoto? Tena nimemzalia mwana katika uzee wake.”

    Hagari Na Ishmaeli Wafukuzwa

    8 21:8Mtoto akakua, akaachishwa kunyonya. Siku hiyo Isaki alipoachishwa kunyonya, Abrahamu alifanya sherehe kubwa. 9 21:9Lakini Sara aliona kuwa mwana ambaye Hagari, Mmisri, aliyemzalia Abrahamu alikuwa anadhihaki, 10 21:10Sara akamwambia Abrahamu, “Mwondoe mwanamke huyo mtumwa pamoja na mwanawe, kwa kuwa mwana wa mwanamke mtumwa kamwe hatarithi pamoja na mwanangu Isaki.”

    11 21:11Jambo hili lilimhuzunisha sana Abrahamu kwa sababu lilimhusu mwanawe. 12 21:12Lakini Mungu akamwambia, “Usihuzunike hivyo kwa sababu ya kijana na mtumishi wako wa kike. Sikiliza lolote Sara analokuambia, kwa sababu uzao wako utahesabiwa kupitia kwake Isaki. 13 21:13Nitamfanya huyu mwana wa mtumishi wako wa kike kuwa taifa pia, kwa sababu naye ni uzao wako.”

    14 21:14Kesho yake asubuhi na mapema, Abrahamu akachukua chakula na kiriba cha maji, akampa Hagari. Akaviweka mabegani mwa Hagari, akamwondoa pamoja na kijana. Hagari akashika njia, akatangatanga katika jangwa la Beer-Sheba.

    15 21:15Maji yalipokwisha kwenye kiriba, akamwacha kijana chini ya mojawapo ya vichaka. 16 21:16Kisha akajiendea zake akaketi karibu, umbali wa kutupa mshale, akawaza, “Siwezi kumwangalia kijana akifa.” Ikawa alipokuwa ameketi pale karibu, akaanza kulia kwa huzuni.

    17 21:17Mungu akamsikia kijana akilia, malaika wa Mungu akamwita Hagari kutoka mbinguni na kumwambia, “Kuna nini Hagari? Usiogope, Mungu amesikia kijana analia akiwa amelala pale. 18 21:18Mwinue kijana na umshike mkono, kwa maana nitamfanya kuwa taifa kubwa.”

    19 21:19Ndipo Mungu akamfumbua Hagari macho yake naye akaona kisima cha maji. Hivyo akaenda akajaza kiriba maji na kumpa kijana anywe.

    20 21:20Mungu akawa pamoja na huyu kijana alipokuwa akiendelea kukua. Aliishi jangwani na akawa mpiga upinde. 21 21:21Alipokuwa akiishi katika Jangwa la Parani, mama yake akampatia mke kutoka Misri.

    Mapatano Katika Beer-Sheba

    22 21:22Wakati huo Abimeleki na Fikoli mkuu wa majeshi yake wakamwambia Abrahamu, “Mungu yu pamoja nawe katika kila kitu unachofanya. 23 21:23Sasa niapie hapa mbele za Mungu kwamba hutanitenda hila mimi, watoto wangu wala wazao wangu. Nitendee mimi na nchi ambayo unaishi kama mgeni wema ule ule ambao nimekutendea.”

    24 21:24Abrahamu akasema, “Ninaapa hivyo.”

    25 21:25Ndipo Abrahamu akalalamika kwa Abimeleki kuhusu kisima cha maji ambacho watumishi wa Abimeleki walikuwa wamekinyangʼanya. 26 21:26Lakini Abimeleki akasema, “Sijui ni nani ambaye amefanya hili. Hukuniambia, leo tu ndipo ninasikia habari zake.”

    27 21:27Hivyo Abrahamu akaleta kondoo na ngʼombe, akampa Abimeleki, nao watu hawa wawili wakafanya mapatano. 28 21:28Abrahamu akatenga kondoo wa kike saba kutoka kwenye kundi, 29 21:29Abimeleki akamuuliza Abrahamu, “Ni nini maana ya hawa kondoo wa kike saba uliowatenga peke yao?”

    30 21:30Abrahamu akamjibu, “Upokee hawa kondoo wa kike saba kutoka mkononi mwangu kama ushahidi kuwa nilichimba kisima hiki.”

    31 21:31Hivyo mahali pale pakaitwa Beer-Sheba, kwa sababu watu wawili waliapiana hapo.

    32 21:32Baada ya mapatano kufanyika huko Beer-Sheba, Abimeleki na Fikoli mkuu wa majeshi yake wakarudi katika nchi ya Wafilisti. 33 21:33Abrahamu akapanda mti wa mkwaju huko Beer-Sheba, na hapo akaliitia jina la Bwana, Mungu wa milele. 34 21:34Naye Abrahamu akakaa katika nchi ya Wafilisti kwa muda mrefu.

    22Kujua Uthabiti Wa Abrahamu

    1 22:1Baadaye Mungu akamjaribu Abrahamu. Akamwambia, “Abrahamu!”

    Abrahamu akajibu, “Mimi hapa.”

    2 22:2Kisha Mungu akamwambia, “Umchukue mwanao, mwana wako wa pekee, Isaki umpendaye, uende katika nchi ya Moria. Mtoe huko kama sadaka ya kuteketezwa juu ya mlima mmojawapo nitakaokuambia.”

    3 22:3Abrahamu akaamka asubuhi na mapema siku iliyofuata, akamtayarisha punda wake. Akawachukua watumishi wake wawili pamoja na Isaki mwanawe. Baada ya kuchanja kuni za kutosha kwa ajili ya hiyo sadaka ya kuteketezwa, akaondoka kuelekea mahali Mungu alipokuwa amemwambia. 4 22:4Siku ya tatu Abrahamu akainua macho, akapaona mahali pale kwa mbali. 5 22:5Akawaambia watumishi wake, “Kaeni hapa pamoja na punda, wakati mimi na kijana tunakwenda kule. Tutakwenda kuabudu na kisha tutawarudia.”

    6 22:6Abrahamu akachukua kuni kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa, akamtwika Isaki mwanawe, yeye mwenyewe akachukua moto na kisu. Walipokuwa wakienda pamoja, 7 22:7Isaki akanena akamwambia Abrahamu baba yake, “Baba yangu!”

    Abrahamu akaitika, “Mimi hapa, mwanangu.”

    Isaki akasema, “Moto na kuni zipo, Je, yuko wapi mwana-kondoo kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa?”

    8 22:8Abrahamu akajibu, “Mwanangu, Mungu mwenyewe atajipatia mwana-kondoo kwa ajili ya hiyo sadaka ya kuteketezwa.” Nao hawa wawili wakaendelea mbele pamoja.

    9 22:9Walipofika mahali pale alipokuwa ameambiwa na Mungu, Abrahamu akajenga madhabahu hapo, akaziweka kuni juu yake. Akamfunga Isaki mwanawe na akamlaza kwenye madhabahu, juu ya zile kuni. 10 22:10Kisha akanyoosha mkono wake na akachukua kisu ili amchinje mwanawe. 11 22:11Lakini malaika wa Bwana akamwita kutoka mbinguni, akamwambia, “Abrahamu! Abrahamu!”

    Akajibu, “Mimi hapa.”

    12 22:12Akamwambia, “Usimdhuru kijana, wala usimtendee jambo lolote. Sasa ninajua kwamba unamcha Mungu, kwa sababu hukunizuilia mwanao, mwana wako wa pekee.”

    13 22:13Abrahamu akainua macho yake, akaona kondoo dume amenaswa pembe zake nyuma yake katika kichaka. Akaenda akamchukua huyo kondoo dume, akamtoa awe sadaka ya kuteketezwa badala ya mwanawe. 14 22:14Abrahamu akapaita mahali pale Yehova-Yire. 22:14 Yehova-Yire maana yake Bwana atatupa. Mpaka siku ya leo inasemekana, “Katika mlima wa Bwana itapatikana.”

    15 22:15Basi malaika wa Bwana akamwita Abrahamu kutoka mbinguni mara ya pili, 16 22:16akasema, “Ninaapa kwa nafsi yangu, asema Bwana, kwamba kwa sababu umefanya jambo hili na hukunizuilia mwanao, mwana wako wa pekee, 17 22:17hakika nitakubariki, na nitauzidisha uzao wako kama nyota za angani na kama mchanga ulioko pwani. Wazao wako watamiliki miji ya adui zao, 18 22:18na kupitia uzao wako mataifa yote duniani yatabarikiwa, kwa sababu umenitii.”

    19 22:19Ndipo Abrahamu akawarudia watumishi wake, wakaondoka wakaenda wote pamoja mpaka Beer-Sheba. Abrahamu akaishi huko Beer-Sheba.

    Wana Wa Nahori

    20 22:20Baada ya muda, Abrahamu akaambiwa, “Milka pia amepata watoto, amemzalia ndugu yako Nahori wana: 21 22:21Usi mzaliwa wake wa kwanza, Buzi nduguye, Kemueli (baba wa Aramu), 22 22:22Kesedi, Hazo, Pildashi, Yidlafu na Bethueli.” 23 22:23Bethueli akamzaa Rebeka. Milka alimzalia Nahori nduguye Abrahamu hao wana wanane. 24 22:24Suria wake Nahori aliyeitwa Reuma pia alikuwa na wana: Teba, Gahamu, Tahashi na Maaka.

    23Kifo Cha Sara

    1 23:1Sara aliishi akawa na umri wa miaka mia na ishirini na saba. 2 23:2Sara akafa huko Kiriath-Arba (yaani Hebroni) katika nchi ya Kanaani, Abrahamu akamwombolezea na kumlilia Sara.

    3 23:3Ndipo Abrahamu akainuka kutoka pale penye maiti ya mke wake. Akazungumza na Wahiti, akasema, 4 23:4“Mimi ni mpitaji na mgeni miongoni mwenu. Niuzieni sehemu ya ardhi yenu ili niweze kumzika maiti wangu.”

    5 23:5Wahiti wakamjibu Abrahamu, 6 23:6“Bwana, tusikilize. Wewe ni mtawala mkuu sana miongoni mwetu. Zika maiti wako katika kaburi unalolipenda kati ya makaburi yetu. Hakuna mtu wa kwetu atakayekuzuia kaburi lake ili kuzika maiti wako.”

    7 23:7Abrahamu akainuka na akasujudu mbele ya wenyeji wa nchi, yaani Wahiti. 8 23:8Akawaambia, “Kama mnaniruhusu kumzika maiti wangu, basi nisikilizeni mkamsihi Efroni mwana wa Sohari kwa niaba yangu 9 23:9ili aniuzie pango la Makpela, lililo mali yake, nalo liko mwisho wa shamba lake. Mwambieni aniuzie kwa bei kamili atakayosema ili liwe mahali pangu pa kuzikia miongoni mwenu.”

    10 23:10Efroni Mhiti alikuwa ameketi miongoni mwa watu wake, akamjibu Abrahamu mbele ya Wahiti wote waliokuwepo katika lango la mji. 11 23:11“La hasha, bwana wangu, nisikilize, nakupa shamba, pia nakupa pango lililomo ndani yake. Nakupa mbele ya watu wangu. Uzike maiti wako.”

    12 23:12Abrahamu akasujudu tena, mbele ya wenyeji wa nchi, 13 23:13akamwambia Efroni wale watu wakiwa wanasikia, “Tafadhali nisikilize. Nitakulipa fedha za hilo shamba. Kubali kuzipokea ili niweze kumzika maiti wangu.”

    14 23:14Efroni akamjibu Abrahamu, 15 23:15“Nisikilize, bwana wangu, thamani ya ardhi hiyo ni shekeli 400 za fedha, 23:15 Shekeli 400 za fedha ni sawa na kilo 4.5. lakini hiyo ni nini kati yako na mimi? Mzike maiti wako.”

    16 23:16Abrahamu akakubali masharti ya Efroni, akampimia ile fedha aliyotaja masikioni mwa Wahiti: Shekeli 400 za fedha kulingana na viwango vya uzito vilivyokuwa vikitumika wakati huo na wafanyabiashara.

    17 23:17Hivyo shamba la Efroni huko Makpela karibu na Mamre, yaani shamba pamoja na pango lililokuwamo, nayo miti yote iliyokuwamo ndani ya mipaka ya shamba hilo, vilikabidhiwa, 18 23:18kwa Abrahamu kuwa mali yake mbele ya Wahiti wote waliokuwa wamekuja kwenye lango la mji. 19 23:19Baada ya hayo Abrahamu akamzika Sara mkewe kwenye pango ndani ya shamba la Makpela karibu na Mamre (huko Hebroni) katika nchi ya Kanaani. 20 23:20Hivyo Wahiti wakamkabidhi Abrahamu shamba pamoja na pango lililokuwa humo kuwa mahali pa kuzikia.

    24Isaki Na Rebeka

    1 24:1Wakati huu Abrahamu alikuwa mzee mwenye miaka mingi, naye Bwana alikuwa amembariki katika kila njia. 2 24:2Akamwambia mtumishi wake mkuu wa vitu vyote katika nyumba yake, yule aliyekuwa msimamizi wa vitu vyote alivyokuwa navyo, “Weka mkono wako chini ya paja langu, 3 24:3Ninataka uape kwa Bwana, Mungu wa mbingu na Mungu wa nchi, kwamba hutamtwalia mwanangu mke kutoka binti za Wakanaani, ambao ninaishi miongoni mwao, 4 24:4bali utakwenda katika nchi yangu na jamaa zangu umpatie Isaki mwanangu mke.”

    5 24:5Yule mtumishi akamuuliza, “Je, kama huyo mwanamke atakataa kuja nami katika nchi hii? Je, nimpeleke mwanao katika hiyo nchi uliyotoka?”

    6 24:6Abrahamu akasema, “Hakikisha kwamba hutamrudisha mwanangu huko. 7 24:7 Bwana, Mungu wa mbingu, aliyenitoa nyumbani kwa baba yangu na nchi yangu niliyozaliwa na aliyesema nami na akaniahidi kwa kiapo, akisema, ‘Nitawapa watoto wako nchi hii,’ atatuma malaika wake akutangulie ili umpatie mwanangu mke kutoka huko. 8 24:8Kama huyo mwanamke asipokubali kufuatana nawe, basi utafunguliwa kutoka kiapo nilichokuapisha. Ila usimrudishe mwanangu huko.” 9 24:9Basi yule mtumishi akaweka mkono wake chini ya paja la bwana wake Abrahamu akamwapia kuhusu shauri hili.

    10 24:10Ndipo huyo mtumishi akachukua ngamia kumi miongoni mwa ngamia za bwana wake, akaondoka, akiwa amechukua aina zote za vitu vizuri kutoka kwa bwana wake. Akaelekea Aramu-Naharaimu 24:10 Yaani Mesopotamia ya Kaskazini-Magharibi. na kushika njia kwenda mji wa Nahori. 11 24:11Akawapigisha ngamia magoti karibu na kisima cha maji nje ya mji, ilikuwa inaelekea jioni, wakati ambapo wanawake wanakuja kuteka maji.

    12 24:12Kisha akaomba, “Ee Bwana, Mungu wa bwana wangu Abrahamu, nipatie ushindi leo, uonyeshe huruma kwa bwana wangu Abrahamu. 13 24:13Tazama, nimesimama karibu na kisima hiki cha maji, nao binti za watu wa mji huu wanakuja kuteka maji. 14 24:14Basi na iwe hivi, nitakapomwambia binti mmojawapo, ‘Tafadhali tua mtungi wako nipate kunywa maji,’ naye akisema, ‘Kunywa, nitawanywesha na ngamia wako pia.’ Basi na awe ndiye uliyemchagua kwa ajili ya mtumishi wako Isaki. Kwa hili nitajua umemhurumia bwana wangu.”

    15 24:15Ikawa kabla hajamaliza kuomba, Rebeka akatokea akiwa na mtungi begani mwake. Alikuwa binti wa Bethueli. Bethueli alikuwa mwana wa Milka aliyekuwa mke wa Nahori ndugu wa Abrahamu. 16 24:16Huyu msichana alikuwa mzuri sana wa sura, bikira, ambaye hakuna mtu aliyekuwa amekutana naye kimwili. Aliteremka kisimani, akajaza mtungi wake akapanda juu.

    17 24:17Ndipo yule mtumishi akaharakisha kukutana naye akamwambia, “Tafadhali nipe maji kidogo katika mtungi wako.”

    18 24:18Yule msichana akasema, “Kunywa, bwana wangu.” Akashusha kwa haraka mtungi mkononi mwake na akampa, akanywa.

    19 24:19Baada ya kumpa yule mtumishi yale maji, akamwambia, “Nitateka maji kwa ajili ya ngamia zako pia mpaka wote watosheke.” 20 24:20Akafanya haraka kumimina maji kwenye birika ya kunyweshea wanyama, akakimbia kisimani kuteka maji mengine na akateka ya kuwatosha ngamia wake wote. 21 24:21Pasipo kusema neno, yule mtumishi akamtazama kwa makini aone kama Bwana ameifanikisha safari yake, au la.

    22 24:22Ikawa ngamia walipokwisha kunywa wote, yule mtumishi akampa huyo msichana pete ya puani ya dhahabu yenye uzito wa beka moja 24:22 Beka moja ya dhahabu ni sawa na gramu 5.5. na bangili mbili za dhahabu zenye uzito wa shekeli kumi. 24:22 Shekeli 10 za dhahabu ni sawa na gramu 110. 23 24:23Kisha akamuuliza, “Wewe ni binti wa nani? Tafadhali uniambie, je, kuna nafasi katika nyumba ya baba yako tutakapoweza kulala?”

    24 24:24Yule msichana akamjibu, “Mimi ni binti wa Bethueli, mwana wa Milka aliyemzalia Nahori.” 25 24:25Akaendelea kusema, “Kwetu kuna majani mengi na malisho, tena kuna nafasi kwa ajili yenu kulala.”

    26 24:26Yule mtumishi akasujudu na kumwabudu Bwana, 27 24:27akisema, “Atukuzwe Bwana, Mungu wa bwana wangu Abrahamu, ambaye hakuondoa wema na uaminifu wake kwa bwana wangu. Mimi nami, Bwana ameniongoza safarini akanifikisha nyumbani kwa jamaa za bwana wangu.”

    28 24:28Yule msichana akakimbia akawaeleza watu wa nyumbani mwa mama yake kuhusu mambo haya. 29 24:29Rebeka alikuwa na kaka aliyeitwa Labani, huyo akaharakisha kukutana na yule mtumishi kule kisimani. 30 24:30Mara alipoiona ile pete puani, na bangili mikononi mwa dada yake na kusikia yale maneno Rebeka aliyoambiwa na huyo mtumishi, alimwendea huyo mtumishi, akamkuta amesimama karibu na ngamia wake pale karibu na kisima. 31 24:31Akamwambia, “Karibu nyumbani wewe uliyebarikiwa na Bwana, kwa nini unasimama huko nje? Mimi nimekuandalia nyumba na mahali kwa ajili ya ngamia.”

    32 24:32Hivyo yule mtumishi akaenda nyumbani, mizigo ikaondolewa juu ya ngamia. Majani na malisho yakaletwa kwa ajili ya ngamia na maji kwa ajili yake na watu wake ili kunawa miguu. 33 24:33Ndipo chakula kikaandaliwa kwa ajili yake, lakini akasema, “Sitakula mpaka niwe nimewaambia yale niliyo nayo ya kusema.”

    Labani akasema, “Basi tuambie.”

    34 24:34Hivyo akasema, “Mimi ni mtumishi wa Abrahamu. 35 24:35 Bwana amembariki sana bwana wangu, amekuwa tajiri. Amempa kondoo na ngʼombe, fedha na dhahabu, watumishi wa kiume na wa kike, ngamia na punda. 36 24:36Sara mkewe bwana wangu amemzalia mwana katika uzee wake, naye amempa kila kitu alichokuwa nacho. 37 24:37Naye bwana wangu ameniapisha na akasema, ‘Kamwe usimtwalie mwanangu mke katika binti za Wakanaani, ambao ninaishi katika nchi yao, 38 24:38ila uende mpaka kwa jamaa ya baba yangu na ukoo wangu mwenyewe, ukamtwalie mwanangu mke huko.’

    39 24:39“Kisha nikamuuliza bwana wangu, ‘Je, kama huyo mwanamke hatakubali kurudi nami?’

    40 24:40“Akanijibu, ‘Bwana ambaye nimetembea mbele zake, atatuma malaika wake pamoja nawe, na kuifanikisha safari yako, ili uweze kupata mke kwa ajili ya mwanangu katika ukoo wangu na kutoka jamaa ya baba yangu. 41 24:41Kisha, utakapokwenda kwenye ukoo wangu, utakuwa umefunguliwa kutoka kiapo changu hata kama wakikataa kukupa huyo binti, utakuwa umefunguliwa kutoka kiapo changu.’

    42 24:42“Nilipokuja kisimani leo nilisema, ‘Ee Bwana, Mungu wa bwana wangu Abrahamu, ikikupendeza, naomba uifanikishe safari niliyoijia. 43 24:43Tazama, ninasimama kando ya kisima hiki, kama mwanamwali akija kuteka maji nami nikimwambia, tafadhali niruhusu ninywe maji kidogo kutoka kwenye mtungi wako, 44 24:44naye kama akiniambia, “Kunywa, nami nitateka maji kwa ajili ya ngamia wako pia,” basi huyo awe ndiye mke ambaye Bwana amemchagulia mwana wa bwana wangu.’

    45 24:45“Kabla sijamaliza kuomba moyoni mwangu, Rebeka akatokea, amebeba mtungi begani mwake. Akashuka kisimani akateka maji, nami nikamwambia, ‘Tafadhali nipe maji ninywe.’

    46 24:46“Akafanya haraka kushusha mtungi wake begani na kusema, ‘Kunywa na nitawanywesha ngamia wako pia,’ basi nikanywa, akawanywesha na ngamia pia.

    47 24:47“Nikamuuliza, ‘Wewe ni binti wa nani?’

    “Akasema, ‘Mimi ni binti wa Bethueli, mwana wa Nahori, Milka aliyemzalia.’

    “Ndipo nilipotia pete puani mwake na bangili mikononi mwake, 48 24:48nikasujudu na nikamwabudu Bwana. Nikamtukuza Bwana, Mungu wa bwana wangu Abrahamu, aliyeniongoza katika njia sahihi ili nimtwalie mwana na bwana wangu mke katika jamaa zake. 49 24:49Ikiwa mtaonyesha wema na uaminifu kwa bwana wangu, mniambie, la sivyo, mniambie, ili niweze kujua njia ya kugeukia.”

    50 24:50Labani na Bethueli wakajibu, “Jambo hili limetoka kwa Bwana, hatuwezi kukuambia jambo lolote baya au jema. 51 24:51Rebeka yuko hapa, mchukue na uende, awe mke wa mwana wa bwana wako, sawasawa na Bwana alivyoongoza.”

    52 24:52Ikawa huyo mtumishi wa Abrahamu aliposikia waliyosema, alisujudu mpaka nchi mbele za Bwana. 53 24:53Ndipo huyo mtumishi akatoa vitu vilivyotengenezwa kwa dhahabu na kwa fedha pamoja na mavazi, akampa Rebeka, pia akawapa zawadi za thamani kubwa nduguye na mamaye. 54 24:54Kisha yeye na wale watu waliokuwa pamoja naye wakala, wakanywa na kulala palepale.

    Walipoamka asubuhi, yule mtumishi, akasema, “Nipeni ruhusa nirudi kwa bwana wangu.”

    55 24:55Lakini ndugu yake Rebeka pamoja na mama yake wakajibu, “Acha binti akae kwetu siku kumi au zaidi, ndipo mwondoke.”

    56 24:56Lakini yule mtumishi akawaambia, “Msinicheleweshe, kwa kuwa Bwana amefanikisha safari yangu, nipeni ruhusa nirudi kwa bwana wangu.”

    57 24:57Ndipo wakasema, “Acha tumwite huyo binti tumuulize, tusikie atakavyosema.” 58 24:58Kwa hiyo wakamwita Rebeka na kumuuliza, “Je, utakwenda na mtu huyu?”

    Akasema, “Nitakwenda.”

    59 24:59Hivyo wakamwaga ndugu yao Rebeka aondoke, pamoja na mjakazi wake, mtumishi wa Abrahamu na watu wake. 60 24:60Wakambariki Rebeka, wakamwambia,

    “Ndugu yetu, uwe wewe kumi elfu, mara elfu nyingi, nao wazao wako wamiliki malango ya adui zao.”

    61 24:61Rebeka na vijakazi wake wakajiandaa, wakapanda ngamia zao wakafuatana na yule mtu. Hivyo yule mtumishi akamchukua Rebeka akaondoka.

    62 24:62Basi Isaki alikuwa ametoka Beer-Lahai-Roi, kwa kuwa alikuwa anaishi nchi ya Negebu. 63 24:63Isaki akatoka kwenda shambani kutafakari wakati wa jioni, alipoinua macho yake, akaona ngamia wanakuja. 64 24:64Rebeka pia akainua macho akamwona Isaki. Akashuka kutoka kwenye ngamia wake 65 24:65na akamuuliza yule mtumishi, “Ni nani mtu yule aliye kule shambani anayekuja kutulaki?”

    Yule mtumishi akajibu, “Huyu ndiye bwana wangu.” Hivyo Rebeka akachukua shela yake akajifunika.

    66 24:66Kisha yule mtumishi akamweleza Isaki mambo yote aliyoyatenda. 67 24:67Ndipo Isaki akamwingiza Rebeka katika hema la Sara mama yake, Isaki akamchukua Rebeka, hivyo akawa mke wake. Isaki akampenda, akafarijika baada ya kifo cha mama yake.

    25Kifo Cha Abrahamu

    1 25:1Abrahamu alioa mke mwingine, ambaye jina lake aliitwa Ketura. 2 25:2Huyu alimzalia Zimrani, Yokshani, Medani, Midiani, Ishbaki na Shua. 3 25:3Yokshani alikuwa baba wa Sheba na Dedani, wazao wa Dedani walikuwa Waashuri, Waletushi na Waleumi. 4 25:4Wana wa Midiani walikuwa Efa, Eferi, Hanoki, Abida na Eldaa. Hawa wote walikuwa uzao wa Ketura.

    5 25:5Abrahamu akamwachia Isaki kila kitu alichokuwa nacho. 6 25:6Lakini Abrahamu alipokuwa bado hai, akawapa watoto wa masuria wake zawadi, kisha akawaondoa waende kuishi pande za mashariki mbali na mwanawe Isaki.

    7 25:7Kwa jumla, Abrahamu aliishi miaka 175. 8 25:8Ndipo Abrahamu akapumua pumzi ya mwisho na akafa akiwa mwenye umri mzuri, mzee aliyeshiba siku, naye akakusanywa pamoja na watu wake. 9 25:9Watoto wake Isaki na Ishmaeli wakamzika katika pango la Makpela karibu na Mamre, katika shamba lililokuwa la Efroni mwana wa Sohari Mhiti, 10 25:10Shamba ambalo Abrahamu alilinunua kwa Wahiti. Hapo ndipo Abrahamu alipozikwa pamoja na mkewe Sara. 11 25:11Baada ya kifo cha Abrahamu, Mungu akambariki mwanawe Isaki, ambaye baadaye aliishi karibu na Beer-Lahai-Roi.

    Wana Wa Ishmaeli

    12 25:12Hivi ndivyo vizazi vya Ishmaeli mtoto wa Abrahamu, ambaye mjakazi wake Sara, Hagari Mmisri, alimzalia Abrahamu.

    13 25:13Haya ndiyo majina ya wana wa Ishmaeli, yaliyoorodheshwa kulingana na jinsi walivyozaliwa: Mzaliwa wa kwanza wa Ishmaeli ni Nebayothi, akafuatia Kedari, Adbeeli, Mibsamu, 14 25:14Mishma, Duma, Masa, 15 25:15Hadadi, Tema, Yeturi, Nafishi na Kedema. 16 25:16Hawa walikuwa wana wa Ishmaeli na haya ni majina ya viongozi wa makabila kumi na mawili kulingana na makao yao na kambi zao. 17 25:17Kwa jumla Ishmaeli aliishi miaka 137. Akapumua pumzi ya mwisho, akafa, naye akakusanywa pamoja na watu wake. 18 25:18Wazao wa Ishmaeli waliishi kuanzia nchi ya Havila hadi Shuri, karibu na mpaka wa Misri, unapoelekea Ashuru. Hao waliishi kwa uhasama na ndugu zao wote.

    Yakobo Na Esau

    19 25:19Hivi ndivyo vizazi vya Isaki mwana wa Abrahamu.

    Abrahamu akamzaa Isaki, 20 25:20Isaki alikuwa na umri wa miaka arobaini alipomwoa Rebeka binti Bethueli Mwaramu kutoka Padan-Aramu, nduguye Labani Mwaramu.

    21 25:21Isaki akamwomba Bwana kwa ajili ya mke wake, kwa sababu alikuwa tasa. Bwana akajibu maombi yake na Rebeka mkewe akapata mimba. 22 25:22Watoto wakashindana tumboni mwake, akasema, “Kwa nini haya yanatokea kwangu?” Kwa hiyo akaenda kumuuliza Bwana.

    23 25:23 Bwana akamjibu,

    “Mataifa mawili yamo tumboni mwako, na mataifa hayo mawili kutoka ndani yako watatenganishwa. Mmoja atakuwa na nguvu zaidi kuliko mwingine, na yule mkubwa atamtumikia yule mdogo.”

    24 25:24Wakati wake wa kujifungua ulipotimia, walikuwepo mapacha wa kiume tumboni mwake. 25 25:25Wa kwanza kuzaliwa alikuwa mwekundu, mwili wake wote ulikuwa kama mtu aliyevaa vazi lenye nywele; wakamwita jina lake Esau. 25:25 Esau maana yake Mwenye nywele nyingi. 26 25:26Baadaye, ndugu yake akatoka, mkono wake ukiwa umemshika Esau kisigino; akaitwa jina lake Yakobo. 25:26 Yakobo maana yake Ashikaye kisigino, au Atwaaye mahali pa mwingine, au Mdanganyaji, au Mwenye hila, au Mlaghai, au Mjanja. Isaki alikuwa mwenye miaka sitini Rebeka alipowazaa.

    27 25:27Watoto wakakua, naye Esau akakuwa mwindaji hodari, mtu wa mbugani, wakati Yakobo alikuwa mtu mtulivu, mwenye kukaa nyumbani. 28 25:28Isaki, ambaye alikuwa anapendelea zaidi nyama za porini, alimpenda Esau, bali Rebeka alimpenda Yakobo.

    29 25:29Siku moja Yakobo alipika mchuzi wa dengu, Esau akarudi kutoka porini akiwa na njaa kali. 30 25:30Esau akamwambia Yakobo, “Haraka, nipe huo mchuzi mwekundu! Nina njaa kali sana!” (Hii ndiyo sababu pia aliitwa Edomu.) 25:30 Edomu maana yake Mwekundu.

    31 25:31Yakobo akamjibu, “Niuzie kwanza haki yako ya mzaliwa wa kwanza.”

    32 25:32Esau akasema, “Tazama, mimi niko karibu ya kufa, itanifaa nini haki ya mzaliwa wa kwanza?”

    33 25:33Yakobo akamwambia, “Niapie kwanza.” Hivyo Esau akamwapia, akamuuzia Yakobo haki yake ya kuzaliwa.

    34 25:34Ndipo Yakobo akampa Esau mkate na ule mchuzi wa dengu. Akala na kunywa, kisha akainuka akaenda zake.

    Kwa hiyo Esau alidharau haki yake ya mzaliwa wa kwanza.

    26Isaki Na Abimeleki

    1 26:1Basi njaa kubwa ikawa katika nchi hiyo, kuliko ile njaa iliyotangulia iliyotokea wakati wa Abrahamu. Isaki akamwendea Abimeleki mfalme wa Wafilisti huko Gerari. 2 26:2 Bwana akamtokea Isaki, akamwambia, “Usiende Misri, bali ukae katika nchi nitakayokuambia. 3 26:3Kaa katika nchi hii kwa kitambo, mimi nitakuwa pamoja na wewe na nitakubariki. Kwa maana nitakupa wewe na uzao wako nchi hizi zote na nitatimiza kiapo nilichomwapia Abrahamu baba yako. 4 26:4Nitafanya wazao wako kuwa wengi kama nyota za angani, nami nitawapa nchi hizi zote na kutokana na uzao wako mataifa yote yatabarikiwa, 5 26:5kwa sababu Abrahamu alinitii mimi akatunza kanuni zangu na maagizo yangu, amri zangu pamoja na sheria zangu.” 6 26:6Hivyo Isaki akaishi huko Gerari.

    7 26:7Watu wa mahali pale walipomuuliza habari za mke wake, akasema, “Huyu ni dada yangu,” kwa sababu aliogopa kusema, “Huyu ni mke wangu.” Alifikiri, “Watu wa mahali pale wataweza kumuua kwa sababu ya Rebeka, kwa kuwa alikuwa mzuri wa sura.”

    8 26:8Wakati Isaki alipokuwa amekaa huko siku nyingi, Abimeleki mfalme wa Wafilisti akachungulia dirishani, akaona jinsi Isaki alivyomkumbatia Rebeka mke wake. 9 26:9Abimeleki akamwita Isaki akamwambia, “Hakika huyu ni mke wako! Mbona uliniambia, ‘Huyu ni dada yangu?’ ”

    Isaki akamjibu, “Kwa sababu nilifikiri ningeweza kuuawa kwa sababu yake.”

    10 26:10Ndipo Abimeleki akamjibu, “Ni nini hiki ulichotufanyia? Ingewezekana mtu yeyote akawa amekutana kimwili na mke wako, nawe ungeleta hatia juu yetu.”

    11 26:11Hivyo Abimeleki akatoa amri kwa watu wote, akisema, “Yeyote atakayemnyanyasa mtu huyu au mkewe hakika atauawa.”

    12 26:12Isaki akapanda mazao katika nchi hiyo, kwa mwaka huo huo, akavuna mara mia, kwa sababu Bwana alimbariki. 13 26:13Isaki akawa tajiri, mali zake zikaendelea kuongezeka mpaka akawa tajiri sana. 14 26:14Akawa na mifugo ya kondoo na ngʼombe, na watumishi wengi sana, kiasi kwamba Wafilisti wakamwonea wivu. 15 26:15Kwa hiyo visima vyote vilivyochimbwa na watumishi wakati wa Abrahamu baba yake, Wafilisti wakavifukia, wakavijaza udongo.

    16 26:16Ndipo Abimeleki akamwambia Isaki, “Ondoka kwetu, kwa maana umetuzidi nguvu sana.”

    17 26:17Basi Isaki akatoka huko akajenga kambi katika Bonde la Gerari, akaishi huko. 18 26:18Ndipo Isaki akavichimbua tena vile visima vya maji ambavyo vilichimbwa siku zile za Abrahamu baba yake, ambavyo Wafilisti walivifukia baada ya kufa Abrahamu, akavipa majina yale yale ambayo baba yake alikuwa amevipa.

    19 26:19Watumishi wa Isaki wakachimba katika lile bonde wakagundua huko kisima chenye maji safi. 20 26:20Lakini wachungaji wa Gerari wakagombana na wachungaji wa Isaki wakisema, “Maji haya ni yetu!” Ndipo akakiita kile kisima Eseki, 26:20 Eseki maana yake ni Ugomvi. kwa sababu waligombana naye. 21 26:21Kisha wakachimba kisima kingine, lakini hata hicho pia wakakigombania, akakiita Sitna. 26:21 Sitna maana yake Upinzani. 22 26:22Akaondoka huko, akachimba kisima kingine, wala hakuna yeyote aliyekigombania. Akakiita Rehobothi, 26:22 Rehobothi maana yake ni Mungu ametufanyia nafasi. akisema, “Sasa Bwana ametufanyia nafasi, nasi tutastawi katika nchi.”

    23 26:23Kutoka pale akaenda Beer-Sheba. 24 26:24Usiku ule Bwana akamtokea, akamwambia, “Mimi ndimi Mungu wa Abrahamu baba yako. Usiogope, kwa maana mimi niko pamoja nawe, nitakubariki na kuongeza idadi ya wazao wako kwa ajili ya Abrahamu mtumishi wangu.”

    25 26:25Isaki akajenga madhabahu huko, akaliitia jina la Bwana. Akapiga hema lake huko, nao watumishi wake wakachimba kisima.

    26 26:26Wakati huo, Abimeleki alikuwa amemjia kutoka Gerari, akifuatana na Ahuzathi mshauri wake, pamoja na Fikoli jemadari wa majeshi yake. 27 26:27Isaki akawauliza, “Mbona mmekuja kwangu na ninyi mlinichukia na kunifukuza?”

    28 26:28Wakamjibu, “Tuliona wazi kuwa Bwana alikuwa pamoja nawe, kwa hiyo tukasema, ‘Inabidi kuwe na kiapo cha mapatano kati yetu, kati yetu na wewe. Na tufanye mkataba pamoja nawe 29 26:29kwamba hutatudhuru, kama jinsi nasi hatukuwanyanyasa bali tuliwatendea mema wakati wote na kuwaondoa kwetu kwa amani. Tena sasa umebarikiwa na Bwana.’ ”

    30 26:30Basi Isaki akawaandalia karamu, nao wakala na kunywa. 31 26:31Kesho yake asubuhi na mapema, wakaapizana wao kwa wao. Kisha Isaki akawaruhusu waende zao, wakamwacha Isaki kwa amani.

    32 26:32Siku hiyo watumishi wa Isaki wakaja wakampa habari kuhusu kisima walichokuwa wamekichimba, wakamwambia, “Tumepata maji!” 33 26:33Naye akakiita Shiba, 26:33 Shiba kwa Kiebrania maana yake ni Saba. mpaka leo mji huo unaitwa Beer-Sheba. 26:33 Beer-Sheba maana yake ni Kisima cha wale saba, yaani wale kondoo saba ambao Abrahamu aliwatoa kama ushahidi kati yake na Abimeleki.

    34 26:34Esau alipokuwa na umri wa miaka arobaini, akamwoa Yudithi binti Beeri Mhiti, kisha akamwoa Basemathi binti Eloni Mhiti. 35 26:35Hawa walikuwa chanzo cha huzuni ya Isaki na Rebeka.

    27Yakobo Anaipata Baraka Ya Isaki

    1 27:1Isaki alipokuwa mzee na macho yake yalipokuwa yamekosa nguvu asiweze kuona tena, akamwita Esau mwanawe mkubwa, akamwambia, “Mwanangu.”

    Akajibu, “Mimi hapa.”

    2 27:2Isaki akasema, “Mimi sasa ni mzee na sijui siku ya kifo changu. 3 27:3Sasa basi, chukua silaha zako, podo na upinde, uende nyikani, ukawinde nyama pori kwa ajili yangu. 4 27:4Uniandalie aina ya chakula kitamu nikipendacho uniletee nile, ili niweze kukubariki kabla sijafa.”

    5 27:5Basi Rebeka alikuwa akisikiliza Isaki alipokuwa akizungumza na mwanawe Esau. Esau alipoondoka kwenda nyikani kuwinda nyama pori na kuleta, 6 27:6Rebeka akamwambia Yakobo mwanawe, “Tazama, nimemsikia baba yako akimwambia ndugu yako Esau, 7 27:7‘Niletee mawindo, kisha ukaniandalie chakula kitamu nile, ili niweze kukubariki mbele za Bwana kabla sijafa.’ 8 27:8Sasa, mwanangu, nisikilize kwa makini na ufanye yale ninayokuambia: 9 27:9Nenda sasa katika kundi ukaniletee wana-mbuzi wawili wazuri, ili niandalie chakula kitamu kwa ajili ya baba yako, kama vile anavyopenda. 10 27:10Kisha umpelekee baba yako ale, ili apate kukubariki kabla hajafa.”

    11 27:11Yakobo akamwambia Rebeka mama yake, “Lakini ndugu yangu Esau ana nywele mwilini, mimi nina ngozi nyororo. 12 27:12Itakuwaje kama baba yangu akinigusa? Itaonekana kwake kama niliyemfanyia ujanja na kuleta laana juu yangu badala ya baraka.”

    13 27:13Mama yake akamwambia, “Mwanangu, laana na iwe juu yangu. Fanya tu ninalokuambia, nenda ukaniletee hao wana-mbuzi.”

    14 27:14Kwa hiyo alikwenda akawaleta, akampa mama yake, akaandaa chakula kitamu, kama vile alivyopenda baba yake. 15 27:15Kisha Rebeka akachukua nguo nzuri za Esau mwanawe wa kwanza, alizokuwa nazo nyumbani, akamvika Yakobo mwanawe mdogo. 16 27:16Pia akamfunika mikononi na sehemu laini ya shingo kwa ngozi za mbuzi. 17 27:17Hatimaye akampa Yakobo hicho chakula kitamu pamoja na mkate aliouoka.

    18 27:18Akamwendea baba yake akasema, “Baba yangu.”

    Akajibu, “Naam, mwanangu, wewe ni nani?”

    19 27:19Yakobo akamwambia baba yake, “Mimi ni Esau mzaliwa wako wa kwanza. Nimefanya kama ulivyoniambia. Tafadhali uketi, ule sehemu ya mawindo yangu ili uweze kunibariki.”

    20 27:20Isaki akamuuliza mwanawe. “Umepataje haraka namna hii, mwanangu?”

    Akajibu, “Bwana Mungu wako amenifanikisha.”

    21 27:21Kisha Isaki akamwambia Yakobo, “Mwanangu tafadhali sogea karibu nami ili nikupapase, nione kama hakika ndiwe Esau mwanangu, au la.”

    22 27:22Yakobo akasogea karibu na baba yake Isaki, ambaye alimpapasa na kusema, “Sauti ni ya Yakobo, bali mikono ni ya Esau.” 23 27:23Hakumtambua, kwa sababu mikono yake ilikuwa na nywele kama ya ndugu yake Esau, kwa hiyo akambariki. 24 27:24Akamuuliza, “Hivi kweli wewe ni mwanangu Esau?”

    Akajibu, “Mimi ndiye.”

    25 27:25Kisha akasema, “Mwanangu, niletee sehemu ya mawindo yako nile, ili nipate kukubariki.”

    Yakobo akamletea naye akala, akamletea na divai akanywa. 26 27:26Kisha Isaki baba yake akamwambia, “Njoo hapa, mwanangu, unibusu.”

    27 27:27Kwa hiyo akamwendea akambusu. Isaki aliposikia harufu ya nguo zake, akambariki, akasema,

    “Aha, harufu ya mwanangu ni kama harufu ya shamba ambalo Bwana amelibariki. 28 27:28Mungu na akupe umande kutoka mbinguni na utajiri wa duniani: wingi wa nafaka na divai mpya. 29 27:29Mataifa na yakutumikie na mataifa yakusujudie. Uwe bwana juu ya ndugu zako, na wana wa mama yako wakusujudie. Walaaniwe wale wakulaanio, nao wale wakubarikio wabarikiwe.”

    30 27:30Baada ya Isaki kumaliza kumbariki na baada tu ya Yakobo kuondoka kwa baba yake, ndugu yake Esau akaingia kutoka mawindoni. 31 27:31Naye pia akaandaa chakula kitamu akamletea baba yake. Kisha akamwambia, “Baba yangu, keti ule sehemu ya mawindo yangu, ili upate kunibariki.”

    32 27:32Isaki baba yake akamuuliza, “Wewe ni nani?”

    Akajibu, “Mimi ni mwanao, mzaliwa wako wa kwanza, Esau.”

    33 27:33Isaki akatetemeka kwa nguvu sana, akasema, “Alikuwa nani basi, ambaye aliwinda mawindo akaniletea? Nilikula kabla tu hujaja na nikambariki, naye hakika atabarikiwa!”

    34 27:34Esau aliposikia maneno haya ya baba yake, akalia sauti kubwa na ya uchungu, na kumwambia baba yake, “Nibariki mimi, mimi pia, baba yangu!”

    35 27:35Lakini akasema, “Ndugu yako amekuja kwa udanganyifu na akachukua baraka yako.”

    36 27:36Esau akasema, “Si ndiyo sababu anaitwa Yakobo? Amenidanganya mara hizi mbili: Alichukua haki yangu ya kuzaliwa na sasa amechukua baraka yangu!” Kisha akauliza, “Hukubakiza hata baraka moja kwa ajili yangu?”

    37 27:37Isaki akamjibu Esau, “Nimemfanya yeye kuwa bwana juu yako, pia nimewafanya ndugu zako wote kuwa watumishi wake, nimemtegemeza kwa nafaka na divai mpya. Sasa nitaweza kukufanyia nini, mwanangu?”

    38 27:38Esau akamwambia baba yake, “Je, baba yangu una baraka moja tu? Unibariki mimi pia, baba yangu!” Kisha Esau akalia kwa sauti kubwa.

    39 27:39Baba yake Isaki akamjibu, akamwambia,

    “Makao yako yatakuwa mbali na utajiri wa dunia, mbali na umande wa mbinguni juu. 40 27:40Utaishi kwa upanga, nawe utamtumikia ndugu yako, lakini wakati utakapokuwa umejikomboa, utatupa nira yake kutoka shingoni mwako.” Yakobo Anakimbilia Kwa Labani

    41 27:41Esau akawa na kinyongo dhidi ya Yakobo kwa ajili ya baraka ambazo baba yake alikuwa amembariki. Akasema moyoni mwake, “Siku za kuomboleza kwa ajili ya baba yangu zimekaribia, ndipo nitamuua ndugu yangu Yakobo.”

    42 27:42Rebeka alipokwisha kuambiwa yale aliyoyasema Esau mwanawe mkubwa, alimwita Yakobo mwanawe mdogo, akamwambia, “Ndugu yako Esau anajifariji kwa wazo la kukuua. 43 27:43Sasa basi, mwanangu, fanya nisemalo: Kimbilia haraka kwa Labani ndugu yangu kule Harani. 44 27:44Ukae naye kwa muda mpaka ghadhabu ya ndugu yako itulie. 45 27:45Wakati ndugu yako atakapokuwa hana hasira nawe tena na amesahau uliyomtendea, nitakupelekea ujumbe urudi. Kwa nini niwapoteze wote wawili kwa siku moja?”

    46 27:46Kisha Rebeka akamwambia Isaki, “Nimechukia kuishi kwa sababu ya hawa wanawake wa Kihiti. Ikiwa Yakobo ataoa mke miongoni mwa wanawake wa nchi hii, wanawake wa Kihiti kama hawa, sitakuwa na faida kuendelea kuishi.”

    281 28:1Basi Isaki akamwita Yakobo, akambariki na akamwamuru, akisema, “Usioe mwanamke wa Kikanaani. 2 28:2Nenda mara moja mpaka Padan-Aramu, kwenye nyumba ya Bethueli baba wa mama yako. Uchukue mke kati ya binti za Labani ambaye ni ndugu wa mama yako. 3 28:3Mungu Mwenyezi 28:3 Mungu Mwenyezi hapa ni jina la Kiebrania, El-Shaddai (yaani Mungu Mwenye utoshelevu wote). na akubariki uwe na uzao uongezeke idadi yako upate kuwa jamii kubwa ya watu. 4 28:4Na akupe wewe na uzao wako baraka aliyopewa Abrahamu, upate kumiliki nchi unayoishi sasa kama mgeni, nchi ambayo Mungu alimpa Abrahamu.” 5 28:5Kisha Isaki akamuaga Yakobo, naye akaenda Padan-Aramu, kwa Labani mwana wa Bethueli Mwaramu, ndugu wa Rebeka, aliyekuwa mama wa Yakobo na Esau.

    6 28:6Sasa Esau akajua kuwa Isaki amembariki Yakobo na kumtuma kwenda Padan-Aramu ili achukue mke huko na kwamba alipombariki alimwamuru akisema, “Usioe mke katika binti za Wakanaani,” 7 28:7tena kwamba Yakobo amewatii baba yake na mama yake naye amekwenda Padan-Aramu. 8 28:8Esau akatambua jinsi ambavyo baba yake Isaki anavyowachukia binti za Wakanaani. 9 28:9Ndipo Esau akaenda kwa Ishmaeli, akamwoa Mahalati, ndugu wa Nebayothi na binti wa Ishmaeli mwana wa Abrahamu, kuongezea wale wake wengine aliokuwa nao.

    Ndoto Ya Yakobo Huko Betheli

    10 28:10Yakobo akatoka Beer-Sheba kwenda Harani. 11 28:11Alipofika mahali fulani, akalala hapo kwa sababu jua lilikuwa limetua. Akachukua jiwe moja la mahali pale, akaliweka chini ya kichwa chake akajinyoosha akalala usingizi. 12 28:12Akaota ndoto ambayo aliona ngazi imesimamishwa juu ya ardhi, ncha yake ikiwa imefika mbinguni na malaika wa Mungu wakawa wakipanda na kushuka juu yake. 13 28:13Juu yake alisimama Bwana, akasema, “Mimi ni Bwana, Mungu wa baba yako Abrahamu na Mungu wa Isaki. Nchi ambayo umelala juu yake, nitakupa wewe na uzao wako. 14 28:14Uzao wako utakuwa kama mavumbi ya nchi, nawe utaenea upande wa magharibi na mashariki, kaskazini na kusini. Kupitia wewe na uzao wako mataifa yote ya duniani yatabarikiwa. 15 28:15Niko pamoja nawe nami nitakulinda kila uendako na nitakurudisha katika nchi hii. Sitakuacha mpaka nitakapofanya hayo niliyokuahidi.”

    16 28:16Yakobo alipoamka kutoka usingizini, akawaza, “Hakika Bwana yuko mahali hapa, wala mimi sikujua.” 17 28:17Kwa hiyo akaogopa, akasema, “Mahali hapa panatisha kama nini! Bila shaka hapa ndipo nyumba ya Mungu ilipo, hili ni lango la mbinguni.”

    18 28:18Asubuhi yake na mapema, Yakobo akalichukua lile jiwe aliloliweka chini ya kichwa chake, akalisimamisha kama nguzo na kumimina mafuta juu yake. 19 28:19Mahali pale akapaita Betheli, 28:19 Betheli maana yake Nyumba ya Mungu. ingawa mji ule hapo kwanza uliitwa Luzu.

    20 28:20Kisha Yakobo akaweka nadhiri, akisema, “Kama Mungu akiwa pamoja nami na kunilinda katika safari niendayo, akinipa chakula nile na nguo nivae 21 28:21na nirudi salama nyumbani kwa baba yangu, hapo ndipo Bwana atakuwa Mungu wangu, 22 28:22nalo jiwe hili nililolisimamisha kama nguzo litakuwa nyumba ya Mungu na katika yote utakayonipa nitakutolea wewe sehemu ya kumi.”

    29Yakobo Awasili Padan-Aramu

    1 29:1Kisha Yakobo akaendelea na safari yake na akafika kwenye nchi za mataifa ya mashariki. 2 29:2Huko akaona kisima katika shamba, pamoja na makundi matatu ya kondoo yamelala karibu na kisima hicho kwa sababu walikuwa wanakunywa maji kutoka kwenye kisimani hicho. Jiwe lililokuwa mdomoni mwa kisima lilikuwa kubwa. 3 29:3Wakati kondoo wanapokuwa wamekusanyika hapo, wachungaji huvingirisha jiwe hilo kutoka kwenye mdomo wa kisima na kunywesha kondoo. Kisha hulirudisha jiwe mahali pake juu ya mdomo wa kisima.

    4 29:4Yakobo aliwauliza wachungaji, “Ndugu zangu, ninyi mmetoka wapi?”

    Wakamjibu, “Tumetoka Harani.”

    5 29:5Aliwaambia, “Je, mnamjua Labani, mjukuu wa Nahori?”

    Wakamjibu, “Ndiyo, tunamfahamu.”

    6 29:6Kisha Yakobo akawauliza, “Je, yeye ni mzima?”

    Wakasema, “Ndiyo, ni mzima, na hapa yuaja Raheli binti yake akiwa na kondoo.”

    7 29:7Akasema, “Tazama, jua bado liko juu, si wakati wa kukusanya mifugo. Nywesheni kondoo na mwarudishe malishoni.”

    8 29:8Walijibu, “Haiwezekani, mpaka kondoo wote wakusanyike na jiwe liwe limevingirishwa kutoka mdomo wa kisima. Ndipo tutanywesha kondoo.”

    9 29:9Alipokuwa akizungumza nao, Raheli akaja pamoja na kondoo wa baba yake, kwa maana alikuwa mchunga kondoo. 10 29:10Yakobo alipomwona Raheli binti Labani, ndugu wa mama yake, pamoja na kondoo wa Labani, alikwenda na kulivingirisha jiwe kutoka mdomoni mwa kisima na kuwanywesha kondoo wa mjomba wake. 11 29:11Kisha Yakobo akambusu Raheli na akaanza kulia kwa sauti. 12 29:12Yakobo alikuwa amemwambia Raheli kuwa yeye alikuwa jamaa ya baba yake, na kwamba ni mwana wa Rebeka. Basi Raheli alikimbia na kumweleza baba yake.

    13 29:13Mara Labani aliposikia habari kuhusu Yakobo, mwana wa ndugu yake, aliharakisha kwenda kumlaki. Akamkumbatia na kumbusu, halafu akamleta nyumbani kwake, kisha Yakobo akamwambia mambo yote. 14 29:14Ndipo Labani akamwambia, “Wewe ni nyama yangu na damu yangu mwenyewe.”

    Yakobo Awaoa Lea Na Raheli

    Baada ya Yakobo kukaa kwa Labani mwezi mzima, 15 29:15Labani akamwambia, “Kwa vile wewe ni jamaa yangu, ndiyo sababu unifanyie kazi bila ujira? Niambie ujira wako utakuwa nini.”

    16 29:16Labani alikuwa na binti wawili, binti mkubwa aliitwa Lea na binti mdogo aliitwa Raheli. 17 29:17Lea alikuwa na macho dhaifu, lakini Raheli alikuwa na umbo la kupendeza na mzuri wa sura. 18 29:18Yakobo akampenda Raheli, akamwambia Labani, “Nitakutumikia kwa miaka saba kwa ajili ya kumpata Raheli binti yako mdogo.”

    19 29:19Labani akasema, “Ni bora zaidi nikupe Raheli kuliko kumpa mtu mwingine yeyote. Kaa pamoja na mimi hapa.” 20 29:20Kwa hiyo Yakobo akatumika miaka saba ili kumpata Raheli, lakini ilionekana kwake kama siku chache tu kwa sababu ya upendo wake kwa Raheli.

    21 29:21Ndipo Yakobo akamwambia Labani, “Nipe mke wangu. Muda wangu umekamilika, nami nataka nikutane naye kimwili.”

    22 29:22Basi Labani akaalika watu wote wa mahali pale na akafanya karamu.

    23 29:23Lakini ilipofika jioni, akamchukua Lea binti yake akampa Yakobo, naye Yakobo akakutana naye kimwili. 24 29:24Naye Labani akamtoa Zilpa, mtumishi wake wa kike, kuwa mtumishi wa Lea, binti yake.

    25 29:25Kesho yake asubuhi, Yakobo akagundua kuwa amepewa Lea! Basi Yakobo akamwambia Labani, “Ni jambo gani hili ulilonitendea? Nilikutumikia kwa ajili ya Raheli, sivyo? Kwa nini umenidanganya?”

    26 29:26Labani akajibu, “Si desturi yetu kumwoza binti mdogo kabla ya kumwoza binti mkubwa. 27 29:27Maliza juma la arusi ya binti huyu, kisha pia nitakupa huyu binti mdogo, kwa kutumika miaka mingine saba.”

    28 29:28Naye Yakobo akafanya hivyo. Akamaliza juma na Lea, kisha Labani akampa Raheli binti yake kuwa mke wake. 29 29:29Labani akamtoa Bilha mtumishi wake wa kike kwa Raheli ili kuwa mtumishi wake. 30 29:30Pia Yakobo akakutana na Raheli kimwili, naye akampenda Raheli zaidi kuliko Lea. Yakobo akamtumikia Labani kwa miaka mingine saba.

    Wana Wa Yakobo

    31 29:31 Bwana alipoona kwamba Lea hapendwi, akampa watoto, lakini Raheli alikuwa tasa. 32 29:32Lea akapata mimba akazaa mwana. Akamwita Reubeni, 29:32 Reubeni maana yake Ona mwana, yaani Yehova ameangalia taabu yangu. kwa maana alisema, “Ni kwa sababu Bwana ameona huzuni yangu. Hakika mume wangu sasa atanipenda.”

    33 29:33Akapata tena mimba, naye alipozaa mwana, akasema, “Kwa sababu Bwana alisikia kwamba sipendwi, amenipa tena huyu mwana.” Kwa hiyo akamwita Simeoni. 29:33 Simeoni maana yake Anasikia, yaani sasa ataungana nami kama Raheli.

    34 29:34Akapata tena mimba, naye alipozaa mwana, akasema, “Sasa afadhali mume wangu ataambatana na mimi, kwa sababu nimemzalia wana watatu.” Kwa hiyo akamwita Lawi. 29:34 Lawi maana yake Nimeunganishwa, yaani na mume wangu.

    35 29:35Akapata tena mimba, naye alipozaa mwana, akasema, “Wakati huu nitamsifu Bwana.” Kwa hiyo akamwita Yuda. 29:35 Yuda maana yake Sifa, yaani Nitamsifu Yehova. Kisha akaacha kuzaa watoto.

    301 30:1Raheli alipoona hamzalii Yakobo watoto, akamwonea ndugu yake wivu. Hivyo akamwambia Yakobo, “Nipe watoto, la sivyo nitakufa!”

    2 30:2Yakobo akamkasirikia, akamwambia, “Je, mimi ni badala ya Mungu, ambaye amekuzuia usizae watoto?”

    3 30:3Ndipo Raheli akamwambia, “Hapa yupo Bilha, mtumishi wangu wa kike. Kutana naye kimwili ili aweze kunizalia watoto na kwa kupitia yeye mimi pia niweze kuwa na uzao.”

    4 30:4Hivyo Raheli akampa Yakobo Bilha awe mke wake. Yakobo akakutana naye kimwili, 5 30:5Bilha akapata mimba, naye akamzalia Yakobo mwana. 6 30:6Ndipo Raheli akasema, “Mungu amenipa haki yangu, amesikiliza maombi yangu na kunipa mwana.” Kwa sababu hiyo akamwita Dani. 30:6 Dani maana yake Anahukumu, yaani Mungu amenipa haki yangu.

    7 30:7Bilha mtumishi wa kike wa Raheli akapata mimba tena, akamzalia Yakobo mwana wa pili. 8 30:8Ndipo Raheli akasema, “Nilikuwa na mashindano makubwa na ndugu yangu, nami nimeshinda.” Kwa hiyo akamwita Naftali. 30:8 Naftali maana yake Nimeshindana nami nimeshinda.

    9 30:9Lea alipoona kuwa amekoma kuzaa watoto, alimchukua mtumishi wake wa kike Zilpa, naye akampa Yakobo awe mke wake. 10 30:10Mtumishi wa Lea yaani Zilpa, akamzalia Yakobo mwana. 11 30:11Ndipo Lea akasema, “Hii ni bahati nzuri aje!” Kwa hiyo akamwita Gadi.

    12 30:12Mtumishi wa kike wa Lea akamzalia Yakobo mwana wa pili. 13 30:13Ndipo Lea aliposema, “Jinsi gani nilivyo na furaha! Wanawake wataniita furaha.” Kwa hiyo akamwita Asheri. 30:13 Asheri maana yake Nimefurahi, yaani Mungu amenifurahisha.

    14 30:14Wakati wa kuvuna ngano, Reubeni akaenda shambani akakuta tunguja, ambazo alizileta kwa Lea mama yake. Raheli akamwambia Lea, “Tafadhali nakuomba unipe baadhi ya tunguja za mwanao.”

    15 30:15Lakini Lea akamwambia, “Haikukutosha kumtwaa mume wangu? Je, utachukua na tunguja za mwanangu pia?”

    Raheli akasema, “Vema sana! Yakobo atakutana nawe kimwili leo usiku, kwa malipo ya tunguja za mwanao.”

    16 30:16Kwa hiyo Yakobo alipokuja kutoka shambani jioni ile, Lea akaenda kumlaki, akamwambia, “Lazima ukutane nami kimwili. Nimekukodisha kwa tunguja za mwanangu.” Kwa hiyo akakutana naye kimwili usiku ule.

    17 30:17Mungu akamsikiliza Lea, naye akapata mimba akamzalia Yakobo mwana wa tano. 18 30:18Ndipo Lea akasema, “Mungu amenizawadia kwa kumpa mume wangu mtumishi wangu wa kike.” Kwa hiyo akamwita Isakari. 30:18 Isakari maana yake Zawadi, yaani Mungu amenizawadia.

    19 30:19Lea akapata mimba tena akamzalia Yakobo mwana wa sita. 20 30:20Ndipo Lea aliposema, “Mungu amenizawadia kwa zawadi ya thamani sana. Wakati huu mume wangu ataniheshimu kwa sababu nimemzalia wana sita.” Kwa hiyo akamwita Zabuloni. 30:20 Zabuloni maana yake Heshima.

    21 30:21Baadaye akamzaa mtoto wa kike akamwita Dina. 30:21 Dina maana yake Tetea haki, yaani Mungu amenitetea katika mashindano yangu.

    22 30:22Ndipo Mungu akamkumbuka Raheli, akasikia maombi yake na akafungua tumbo lake. 23 30:23Akapata mimba na akamzaa mwana na kusema, “Mungu ameniondolea aibu yangu.”

    24 30:24Akamwita Yosefu 30:24 Yosefu maana yake Yeye na aongeze, yaani Mungu na aniongezee. na kusema, “Bwana na anipe mwana mwingine.”

    Makundi Ya Yakobo Yaongezeka

    25 30:25Baada ya Raheli kumzaa Yosefu, Yakobo akamwambia Labani, “Nipe ruhusa nirudi katika nchi yangu. 26 30:26Nipe wake zangu na watoto, ambao nimetumika kuwapata, nami niende zangu. Unajua ni kazi kiasi gani ambayo nimekufanyia.”

    27 30:27Lakini Labani akamwambia, “Ikiwa nimepata kibali machoni pako, tafadhali ukae. Nimegundua kwa njia ya uaguzi kwamba Bwana amenibariki kwa sababu yako.” 28 30:28Akaongeza kumwambia, “Taja ujira wako nami nitakulipa.”

    29 30:29Yakobo akamwambia, “Unajua jinsi ambavyo nimekutumikia na jinsi ambavyo wanyama wako walivyolishwa vizuri chini ya uangalizi wangu. 30 30:30Kidogo ulichokuwa nacho kabla sijaja kimeongezeka sana, naye Bwana amekubariki popote nilipokuwa. Lakini sasa, ni lini nitashughulikia mambo ya nyumba yangu mwenyewe?”

    31 30:31Labani akamuuliza, “Nikupe nini?”

    Yakobo akamjibu, “Usinipe chochote lakini kama utanifanyia jambo hili moja, nitaendelea kuchunga na kuyaangalia makundi yako. 32 30:32Niruhusu nipite katika makundi yako yote leo niondoe humo kila kondoo mwenye mabakabaka au madoadoa, kila mwana-kondoo mweusi na kila mbuzi mwenye madoadoa au mabakabaka. Hawa watakuwa ujira wangu. 33 30:33Uadilifu wangu utanishuhudia siku zijazo, kila utakapochunguza ujira ambao umenilipa mimi. Mbuzi yeyote wangu ambaye hana mabakabaka wala madoadoa, au mwana-kondoo ambaye si mweusi, atahesabika ameibwa.”

    34 30:34Labani akasema, “Ninakubali na iwe kama ulivyosema.” 35 30:35Siku ile ile Yakobo akawaondoa beberu wote waliokuwa na mistari au madoadoa na mbuzi wake wote waliokuwa na mistari au madoadoa (wote waliokuwa na alama nyeupe juu yao) na wana-kondoo weusi wote, akawaweka chini ya uangalizi wa wanawe. 36 30:36Kisha Labani akamwacha Yakobo kwa mwendo wa safari ya siku tatu kati yake na Yakobo, wakati Yakobo akiendelea kuchunga lile kundi la Labani lililobaki.

    37 30:37Hata hivyo, Yakobo, akachukua fito mbichi zilizokatwa wakati huo huo za miti ya mlubna, mlozi na mwaramoni akazibambua ili mistari myeupe ionekane katika fito hizo. 38 30:38Kisha akaweka fito alizozibambua kwenye mabirika yote ya kunyweshea mifugo, ili ziwe mbele ya makundi walipokuja kunywa maji. Wanyama walipokuja kunywa maji, hali wakiwa wanahitaji mbegu, 39 30:39wakapandwa hizo fito zikiwa mbele yao. Wanyama waliopata mimba mbele ya hizo fito walizaa wanyama wenye mistari, madoadoa na mabakabaka. 40 30:40Yakobo akawatenga wadogo wa kundi peke yao, lakini akazielekeza nyuso za hao waliobaki kwenye wale wenye mistari na weusi waliokuwa mali ya Labani. Hivyo akatenga makundi yake mwenyewe, na wala hakuwachanganya na wanyama wa Labani. 41 30:41Kila mara wanyama wenye nguvu walipohitaji mbegu, Yakobo aliweka zile fito kwenye mabirika mbele ya hao wanyama, ili wapandwe karibu na hizo fito, 42 30:42lakini ikiwa wanyama walikuwa wadhaifu hakuziweka hizo fito. Hivyo wanyama wadhaifu wakawa wa Labani, na wanyama wenye nguvu wakawa wa Yakobo. 43 30:43Kwa njia hii Yakobo akastawi sana, tena akawa na makundi makubwa, watumishi wa kike na wa kiume na ngamia na punda.

    31Yakobo Akimbia Kutoka Kwa Labani

    1 31:1Yakobo akawasikia wana wa Labani wakisema, “Yakobo amechukua kila kitu kilichokuwa cha baba yetu naye amepata utajiri huu wote kutokana na vile vilivyokuwa mali ya baba yetu.” 2 31:2Yakobo akatambua kwamba moyo wa Labani kwake haukuwa kama ulivyokuwa mwanzo.

    3 31:3Ndipo Bwana akamwambia Yakobo, “Rudi katika nchi ya baba zako na kwa watu wako, nami nitakuwa pamoja nawe.”

    4 31:4Hivyo Yakobo akatuma ujumbe kwa Raheli na Lea waje machungani yalikokuwa makundi yake. 5 31:5Akawaambia, “Naona moyo wa baba yenu kwangu sivyo kama ulivyokuwa mwanzoni, lakini Mungu wa baba yangu amekuwa pamoja nami. 6 31:6Mnajua kwamba nimemtumikia baba yenu kwa nguvu zangu zote, 7 31:7hata hivyo baba yenu amenidanganya kwa kubadilisha ujira wangu mara kumi. Hata hivyo, Mungu hakumruhusu kunidhuru. 8 31:8Kama alisema, ‘Wenye madoadoa watakuwa ujira wako,’ basi makundi yote yalizaa wenye madoadoa, kama alisema, ‘Wenye mistari watakuwa ujira wako,’ basi makundi yote yalizaa wenye mistari. 9 31:9Hivyo Mungu amechukua mifugo ya baba yenu na amenipa mimi.

    10 31:10“Wakati fulani majira ya kuzaliana niliota ndoto ambayo niliinua macho na kuona kwamba wale mabeberu waliokuwa wakipanda kundi walikuwa wa mistari, madoadoa na mabakabaka. 11 31:11Malaika wa Mungu akaniambia katika ndoto, ‘Yakobo.’ Nikamjibu, ‘Mimi hapa.’ 12 31:12Akasema, ‘Inua macho yako uone wale mabeberu wote wanaopanda kundi wana mistari, madoadoa au mabakabaka, kwa maana nimeona yale yote ambayo Labani amekuwa akikutendea. 13 31:13Mimi ndiye Mungu wa Betheli, ulikomiminia ile nguzo mafuta na pale mahali uliponiwekea nadhiri. Sasa ondoka katika nchi hii mara moja urudi katika nchi uliyozaliwa.’ ”

    14 31:14Ndipo Raheli na Lea wakajibu, “Je bado tu tunalo fungu lolote katika urithi wa nyumba ya baba yetu? 15 31:15Je, yeye hatuhesabu sisi kama wageni? Sio kwamba ametuuza tu, bali ametumia hata na vile vilivyolipwa kwa ajili yetu. 16 31:16Hakika utajiri wote ambao Mungu ameuchukua kutoka kwa baba yetu ni mali yetu na watoto wetu. Hivyo fanya lolote lile Mungu alilokuambia.”

    17 31:17Ndipo Yakobo akawapandisha watoto wake na wake zake juu ya ngamia, 18 31:18naye akawaswaga wanyama wote mbele yake pamoja na vitu vyote alivyokuwa amechuma huko Padan-Aramu kwenda kwa baba yake Isaki katika nchi ya Kanaani.

    19 31:19Labani alipokuwa amekwenda kukata kondoo wake manyoya, Raheli aliiba miungu ya nyumba ya baba yake. 20 31:20Zaidi ya hayo, Yakobo alimdanganya Labani Mwaramu kwa kutokumwambia kwamba anakimbia. 21 31:21Hivyo akakimbia pamoja na vitu vyote alivyokuwa navyo na kuvuka Mto Frati akaelekea nchi ya vilima katika Gileadi.

    Labani Amfuatilia Yakobo

    22 31:22Siku ya tatu Labani akaambiwa kwamba Yakobo amekimbia. 23 31:23Akiwachukua jamaa zake, akamfuatia Yakobo kwa siku saba na kumkuta kwenye nchi ya vilima katika Gileadi. 24 31:24Ndipo Mungu akamjia Labani Mwaramu katika ndoto usiku na kumwambia, “Jihadhari usiseme neno lolote kwa Yakobo, liwe zuri au baya.”

    25 31:25Yakobo alikuwa amepiga hema lake katika nchi ya vilima katika Gileadi wakati Labani alipomkuta, Labani na jamaa yake wakapiga kambi huko pia. 26 31:26Ndipo Labani akamwambia Yakobo, “Umefanya nini? Umenidanganya na umewachukua binti zangu kama mateka katika vita. 27 31:27Kwa nini ulikimbia kwa siri na kunidanganya? Kwa nini hukuniambia ili nikuage kwa furaha na nyimbo za matari na vinubi? 28 31:28Hata hukuniruhusu niwabusu wajukuu zangu na kuwaaga binti zangu. Umefanya kitu cha kipumbavu. 29 31:29Nina uwezo wa kukudhuru, lakini usiku uliopita Mungu wa baba yako alisema nami, akaniambia, ‘Jihadhari, usiseme neno lolote kwa Yakobo liwe zuri au baya.’ 30 31:30Sasa umeondoka kwa sababu umetamani kurudi nyumbani kwa baba yako. Lakini kwa nini umeiba miungu yangu?”

    31 31:31Yakobo akamjibu Labani, “Niliogopa, kwa sababu nilifikiri ungeweza kuninyangʼanya binti zako kwa nguvu. 32 31:32Lakini kama ukimkuta yeyote aliye na miungu yako, hataishi. Mbele ya jamaa yetu, angalia mwenyewe uone kama kuna chochote chako hapa nilicho nacho, kama kipo, kichukue.” Basi Yakobo hakujua kwamba Raheli alikuwa ameiba hiyo miungu.

    33 31:33Kwa hiyo Labani akaingia ndani ya hema la Yakobo na ndani ya hema la Lea na ndani ya hema la watumishi wawili wa kike, lakini hakukuta chochote. Baadaye alipotoka katika hema la Lea, akaingia hema la Raheli. 34 31:34Basi Raheli ndiye alikuwa amechukua ile miungu ya nyumbani kwao na kuiweka katika matandiko ya ngamia na kukalia. Labani akatafuta kila mahali kwenye hema lakini hakupata chochote.

    35 31:35Raheli akamwambia baba yake, “Usikasirike, bwana wangu kwa kuwa siwezi kusimama ukiwepo, niko katika hedhi.” Labani akatafuta lakini hakuweza kuipata miungu ya nyumbani kwake.

    36 31:36Yakobo akakasirika na kumshutumu Labani, akisema, “Uhalifu wangu ni nini?” Akamuuliza Labani, “Ni dhambi gani niliyofanya hata unaniwinda? 37 31:37Sasa kwa kuwa umepekua vitu vyangu vyote umepata nini kilicho cha nyumbani mwako? Kiweke hapa mbele ya jamaa yako na yangu, nao waamue kati yetu sisi wawili.

    38 31:38“Mpaka sasa nimekuwa pamoja nawe miaka ishirini. Kondoo wako na mbuzi wako hawajaharibu mimba, wala sijala kondoo dume kutoka makundi yako. 39 31:39Sikukuletea mfugo aliyeraruliwa na wanyama pori, nilibeba hasara mimi mwenyewe. Tena ulinidai malipo kwa chochote kilichoibwa mchana au usiku. 40 31:40Hii ndiyo iliyokuwa hali yangu: Niliumia kwa joto la mchana na baridi usiku, pia usingizi ulinipa. 41 31:41Ilikuwa hivi kwa miaka ile ishirini niliyokuwa nyumbani kwako. Nilikutumikia miaka ile kumi na minne kwa ajili ya binti zako wawili, miaka sita kwa ajili ya makundi yako, nawe ulibadilisha ujira wangu mara kumi. 42 31:42Kama Mungu wa baba yangu, Mungu wa Abrahamu na Hofu ya Isaki, hakuwa pamoja nami, hakika ungenifukuza mikono mitupu. Lakini Mungu ameona taabu yangu na kazi ngumu ya mikono yangu, naye usiku uliopita amekukemea.”

    43 31:43Labani akamjibu Yakobo, “Wanawake hawa ni binti zangu, watoto hawa ni watoto wangu na makundi haya ni makundi yangu. Vyote unavyoviona ni vyangu. Lakini hata hivyo ninaweza kufanya nini kuhusu hawa binti zangu, au kuhusu watoto waliowazaa? 44 31:44Njoo sasa na tufanye agano, wewe na mimi, na liwe kama shahidi kati yetu.”

    45 31:45Hivyo Yakobo akachukua jiwe, akalisimamisha kama nguzo. 46 31:46Akawaambia jamaa yake, “Kusanyeni mawe.” Hivyo wakachukua mawe na kuyakusanya yakawa lundo, wakala chakula hapo karibu na hilo lundo. 47 31:47Labani akaliita Yegar-Sahadutha 31:47 Yegar-Sahadutha maana yake ni Lundo la ushahidi kwa Kiaramu. na Yakobo akaliita Galeedi. 31:47 Galeedi maana yake ni Lundo la ushahidi kwa Kiebrania.

    48 31:48Labani akasema, “Lundo hili ni shahidi kati yako na mimi leo.” Ndiyo maana likaitwa Galeedi. 49 31:49Pia liliitwa Mispa, 31:49 Mispa maana yake Mnara wa ulinzi. kwa sababu alisema, “Bwana na aweke ulinzi kati yako na mimi wakati kila mmoja akiwa mbali na mwingine. 50 31:50Kama ukiwatenda mabaya binti zangu au ukioa wake wengine zaidi ya binti zangu, hata ingawa hakuna hata mmoja aliye pamoja nasi, kumbuka kwamba Mungu ni shahidi kati yako na mimi.”

    51 31:51Pia Labani akamwambia Yakobo, “Hili ndilo lundo, na hii ndiyo nguzo niliyoisimamisha kati yako na mimi. 52 31:52Lundo hili ni shahidi na nguzo hii ni shahidi, kwamba sitavuka lundo hili kuja upande wako kukudhuru, nawe kwamba hutavuka lundo hili na nguzo hii kuja upande wangu kunidhuru. 53 31:53Mungu wa Abrahamu na Mungu wa Nahori, Mungu wa baba zao, aamue kati yetu.”

    Hivyo Yakobo akaapa kwa jina la Hofu ya baba yake Isaki. 54 31:54Yakobo akatoa dhabihu juu ya kilima na akawaalika jamaa zake kula chakula. Baada ya kula, wakalala huko.

    55 31:55Kesho yake asubuhi na mapema, Labani akawabusu wajukuu zake, binti zake na kuwabariki. Kisha akaondoka, akarudi nyumbani.

    32Yakobo Ajiandaa Kukutana Na Esau

    1 32:1Yakobo pia akaondoka akaenda zake, nao malaika wa Mungu wakakutana naye. 2 32:2Yakobo alipowaona, akasema, “Hii ni kambi ya Mungu!” Kwa hiyo akapaita mahali pale Mahanaimu. 32:2 Mahanaimu maana yake Kambi mbili.

    3 32:3Yakobo akatuma wajumbe kumtangulia kwa Esau ndugu yake huko Seiri, katika nchi ya Edomu. 4 32:4Akawaagiza akisema: “Hili ndilo mtakalomwambia bwana wangu Esau: ‘Mtumishi wako Yakobo anasema, nimekuwa nikiishi pamoja na Labani na nimekuwako huko mpaka sasa. 5 32:5Ninao ngʼombe na punda, kondoo na mbuzi, watumishi wa kiume na wa kike. Sasa ninatuma ujumbe huu kwa bwana wangu, ili nipate kibali machoni pako.’ ”

    6 32:6Wajumbe waliporudi kwa Yakobo, wakamwambia, “Tulikwenda kuonana na ndugu yako Esau, naye sasa anakuja kukulaki akifuatana na wanaume 400.”

    7 32:7Kwa hofu kuu na huzuni, Yakobo akagawanya watu aliokuwa nao katika makundi mawili, pia akagawanya makundi ya kondoo na mbuzi, na vilevile ngʼombe na ngamia. 8 32:8Yakobo alifikiri, “Kama Esau akija na kushambulia kundi moja, kundi lililobaki litaweza likanusurika.”

    9 32:9Ndipo Yakobo akaomba, “Ee Mungu wa baba yangu Abrahamu, Mungu wa baba yangu Isaki, Ee Bwana, ambaye uliniambia, ‘Rudi katika nchi yako na jamaa yako, nami nitakufanya ustawi,’ 10 32:10mimi sistahili fadhili na uaminifu wako wote ulionitendea mimi mtumishi wako. Nilikuwa na fimbo tu mkononi mwangu nilipovuka mto huu wa Yordani, lakini sasa ninayo makundi mawili. 11 32:11Nakuomba, uniokoe na mkono wa ndugu yangu Esau, kwa maana ninaogopa kuwa atakuja kunishambulia, pia mama pamoja na watoto wao. 12 32:12Lakini umeshasema, ‘Hakika nitakufanya ustawi na kuufanya uzao wako kuwa mwingi kama mchanga wa baharini ambao hauwezi kuhesabika!’ ”

    13 32:13Akalala pale usiku ule, miongoni mwa vitu alivyokuwa navyo, akachagua zawadi kwa ajili ya Esau ndugu yake: 14 32:14Mbuzi waume ishirini na mbuzi wake 200, kondoo dume ishirini na kondoo wake 200. 15 32:15Ngamia wake thelathini pamoja na ndama zao, ngʼombe wake arobaini na mafahali kumi, punda wake ishirini na punda waume kumi. 16 32:16Akaviweka chini ya uangalizi wa watumishi wake, kila kundi peke yake na kuwaambia, “Nitangulieni na kuacha nafasi kati ya makundi.”

    17 32:17Akamwagiza yule aliyetangulia kuwa, “Ndugu yangu Esau atakapokutana nawe na kukuuliza, ‘Wewe ni wa nani? Unakwenda wapi? Wanyama hawa wote mbele yako ni mali ya nani?’ 18 32:18Ndipo utakaposema, ‘Ni mali ya mtumishi wako Yakobo. Ni zawadi ambazo zimetumwa kwa bwana wangu Esau, naye anakuja nyuma yetu.’ ”

    19 32:19Akamwagiza pia yule mtumishi wa kundi la pili, la tatu na yale mengine yote yaliyofuata akiwaambia, “Mtamwambia Esau maneno hayo hayo mtakapokutana naye. 20 32:20Hakikisheni mmesema, ‘Mtumishi wako Yakobo anakuja nyuma yetu.’ ” Kwa kuwa alifikiri, “Nitaweza kumtuliza kwa zawadi hizi ninazotanguliza, hatimaye, nitakapomwona, huenda atanikubali.” 21 32:21Kwa hiyo zawadi za Yakobo zilitangulia mbele yake, lakini yeye mwenyewe alilala kambini usiku ule.

    Yakobo Ashindana Mweleka Na Mungu

    22 32:22Usiku ule Yakobo akaamka akawachukua wake zake wawili, watumishi wake wawili wa kike na wanawe kumi na mmoja na akavuka kivuko cha Yaboki. 23 32:23Baada ya kuwavusha ngʼambo ya kijito, alivusha pia mali zake zote. 24 32:24Kwa hiyo Yakobo akaachwa peke yake na mtu mmoja akashikana naye mweleka mpaka mapambazuko. 25 32:25Yule mtu alipoona kuwa hawezi kumshinda, aligusa kiungio cha nyonga ya Yakobo kwa hiyo nyonga yake ikateguka wakati alipokuwa akishikana mweleka na yule mtu. 26 32:26Ndipo yule mtu akasema, “Niache niende, kwa kuwa ni mapambazuko.”

    Lakini Yakobo akajibu, “Sitakuacha uende usiponibariki.”

    27 32:27Yule mtu akamuuliza, “Jina lako nani?”

    Akajibu, “Yakobo.”

    28 32:28Ndipo yule mtu akasema, “Jina lako halitakuwa tena Yakobo, bali Israeli, 32:28 Israeli maana yake Yeye ashindanaye na Mungu. kwa sababu umeshindana na Mungu na watu pia, nawe umeshinda.”

    29 32:29Yakobo akasema, “Tafadhali niambie jina lako.”

    Lakini akajibu, “Kwa nini kuniuliza Jina langu?” Ndipo akambariki huko.

    30 32:30Kwa hiyo Yakobo akapaita mahali pale Penieli, 32:30 Penieli maana yake Uso wa Mungu, ambalo ni sawa na Penueli kwa Kiebrania. akasema, “Ni kwa sababu nimemwona Mungu uso kwa uso na bado maisha yangu yameokoka.”

    31 32:31Jua lilikuwa linachomoza Yakobo alipoondoka Penueli, naye alikuwa akichechemea kwa sababu ya nyonga yake. 32 32:32Kwa hiyo mpaka leo Waisraeli hawali mshipa ulioungana na kiungio cha nyonga, kwa sababu kiungio cha nyonga ya Yakobo kiliteguliwa karibu na mshipa huo.

    33Yakobo Akutana Na Esau

    1 33:1Yakobo akainua macho akamwona Esau akija na watu wake 400, kwa hiyo akawagawanya watoto kati ya Lea, Raheli na wale watumishi wake wawili wa kike. 2 33:2Akawaweka wale watumishi wa kike na watoto wao mbele, Lea na watoto wake wakafuata, Raheli na Yosefu wakaja nyuma. 3 33:3Yeye mwenyewe akatangulia mbele na kusujudu mara saba alipomkaribia ndugu yake.

    4 33:4Lakini Esau akamkimbilia Yakobo kumlaki na kumkumbatia, akamwangukia shingoni na kumbusu. Nao wakalia. 5 33:5Esau akainua macho akawaona wale wanawake na watoto. Akauliza, “Hawa uliofuatana nao ni nani?”

    Yakobo akamjibu, “Ni watoto ambao Mungu amempa mtumishi wako kwa neema.”

    6 33:6Kisha wale watumishi wa kike na watoto wao wakakaribia na kusujudu. 7 33:7Kisha Lea na watoto wake wakaja na kusujudu. Mwisho wa wote wakaja Yosefu na Raheli, nao pia wakasujudu.

    8 33:8Esau akauliza, “Una maana gani kuhusu makundi hayo yote niliyokutana nayo?”

    Akasema, “Ni ili kupata kibali machoni pako, bwana wangu.”

    9 33:9Lakini Esau akamwambia, “Ndugu yangu, tayari nina wingi wa mali. Ulivyo navyo viwe vyako mwenyewe.”

    10 33:10Yakobo akasema, “La hasha! Tafadhali, kama nimepata kibali machoni pako, upokee zawadi hii kutoka kwangu. Kwa maana kuuona uso wako, ni kama kuuona uso wa Mungu, kwa kuwa umenipokea kwa takabali kubwa. 11 33:11Tafadhali ukubali zawadi iliyoletwa kwako, kwa kuwa Mungu amenineemesha na ninavyo vyote ninavyohitaji.” Kwa sababu Yakobo alisisitiza, Esau akapokea.

    12 33:12Ndipo Esau akasema, “Na tuendelee na safari, nitakuwa pamoja nawe.”

    13 33:13Lakini Yakobo akamwambia, “Bwana wangu unajua kwamba watoto ni wachanga na kwamba ni lazima nitunze hawa kondoo wake na ngʼombe wanaonyonyesha. Wakipelekwa kwa haraka hata kama ni kwa siku moja tu, wanyama wote watakufa. 14 33:14Hivyo bwana wangu umtangulie mtumishi wako, wakati mimi nikija polepole kwa mwendo wa makundi yaliyo mbele yangu na mwendo wa watoto, mpaka nifike kwa bwana wangu huko Seiri.”

    15 33:15Esau akamwambia, “Basi na niwaache baadhi ya watu wangu pamoja nawe.”

    Yakobo akauliza, “Lakini kwa nini ufanye hivyo, niache tu nipate kibali machoni pa bwana wangu.”

    16 33:16Hivyo siku hiyo Esau akashika njia akarudi Seiri. 17 33:17Pamoja na hayo, Yakobo akaenda Sukothi, 33:17 Sukothi maana yake Vibanda. mahali alipojijengea makazi kwa ajili yake na mabanda kwa ajili ya mifugo yake. Hii ndiyo sababu sehemu ile inaitwa Sukothi.

    18 33:18Baada ya Yakobo kutoka Padan-Aramu, alifika salama katika mji wa Shekemu huko Kanaani na kuweka kambi yake karibu na mji. 19 33:19Akanunua kiwanja kutoka kwa wana wa Hamori, baba wa Shekemu, kwa bei ya vipande mia vya fedha, ambapo alipiga hema lake. 20 33:20Pale akajenga madhabahu na kupaita El-Elohe-Israeli. 33:20 El-Elohe-Israeli maana yake Mungu, Mungu wa Israeli au Mwenye Nguvu ni Mungu wa Israeli.

    34Dina Na Washekemu

    1 34:1Basi Dina, binti wa Yakobo aliyezaliwa na Lea, akatoka nje kuwatembelea wanawake wa nchi ile. 2 34:2Ikawa Shekemu mwana wa Hamori Mhivi, mtawala wa eneo lile alipomwona, akamchukua na kumnajisi. 3 34:3Moyo wake ukavutwa sana kwa Dina binti Yakobo, akampenda huyu msichana na akazungumza naye kwa kumbembeleza. 4 34:4Shekemu akamwambia baba yake Hamori, “Nipatie msichana huyu awe mke wangu.”

    5 34:5Yakobo aliposikia kwamba binti yake Dina amenajisiwa, wanawe walikuwa mashambani wakichunga mifugo yake, kwa hiyo akalinyamazia jambo hilo mpaka waliporudi nyumbani.

    6 34:6Kisha Hamori baba yake Shekemu akaenda kuzungumza na Yakobo. 7 34:7Basi wana wa Yakobo walikuwa wamerudi kutoka mashambani mara tu waliposikia kilichotokea. Walikuwa wamejawa na huzuni na ghadhabu, kwa sababu Shekemu alikuwa amefanya jambo la aibu katika Israeli kwa kukutana kimwili na binti wa Yakobo, kitu ambacho hakingepasa kufanyika.

    8 34:8Lakini Hamori akawaambia, “Moyo wa mwanangu Shekemu umeelekea kwa binti yenu. Tafadhali mpeni awe mke wake. 9 34:9Oaneni na sisi, tupeni binti zenu, nanyi mchukue binti zetu. 10 34:10Mwaweza kuishi katikati yetu, nchi ni wazi kwenu. Ishini ndani yake, fanyeni biashara humu na mjipatie mali.”

    11 34:11Kisha Shekemu akamwambia baba yake Dina pamoja na ndugu zake, “Na nipate kibali machoni penu, nami nitawapa chochote mtakachosema. 12 34:12Niambieni kiasi cha mahari na zawadi nitakayoileta, hata iwe kubwa kiasi gani, nami nitawalipa chochote mtakachodai. Nipeni tu huyu msichana awe mke wangu.”

    13 34:13Kwa sababu ndugu yao Dina alikuwa amenajisiwa, wana wa Yakobo wakajibu kwa udanganyifu walipozungumza na Shekemu pamoja na baba yake Hamori. 14 34:14Wakawaambia, “Hatuwezi kufanya jambo kama hili, hatuwezi kumtoa dada yetu kwa mtu ambaye hakutahiriwa. Hiyo itakuwa aibu kwetu. 15 34:15Tutakuruhusu kwa sharti moja tu, kwamba mtakuwa kama sisi kwa kuwatahiri wanaume wenu wote. 16 34:16Kisha tutawapa binti zetu na sisi tutawachukua binti zenu. Tutaishi kwenu na tutakuwa watu wamoja nanyi. 17 34:17Lakini mkikataa kutahiriwa, tutamchukua ndugu yetu na kuondoka.”

    18 34:18Pendekezo lao likawa jema kwa Hamori na Shekemu mwanawe. 19 34:19Kijana mdogo, ambaye alikuwa ameheshimiwa kati ya wote walioishi nyumbani mwa baba yake, hakupoteza muda kufanya waliyoyasema, kwa sababu alikuwa amependezwa sana na binti Yakobo. 20 34:20Kwa hiyo Hamori na Shekemu mwanawe walikwenda kwenye lango la mji kuzungumza na wenzao wa mjini. 21 34:21Wakasema, “Hawa watu ni marafiki kwetu, tuwaruhusu waishi katika nchi yetu na kufanya biashara ndani yake, nchi ina nafasi tele kwa ajili yao. Tunaweza kuoa binti zao. Nao wanaweza kuoa binti zetu. 22 34:22Lakini watu hao watakuwa tayari kukubali kuishi nasi kama watu wamoja nao kwa sharti kwamba wanaume wetu watahiriwe, kama wao. 23 34:23Je, si mifugo yao, mali zao na wanyama wao wengine wote watakuwa wetu? Basi na tuwape kibali, nao wataishi miongoni mwetu.”

    24 34:24Wanaume wote waliotoka nje ya lango la mji walikubaliana na Hamori na Shekemu mwanawe na kila mwanaume katika mji ule akatahiriwa.

    25 34:25Baada ya siku tatu, wakati wote wakiwa wangali katika maumivu, wana wawili wa Yakobo, yaani Simeoni na Lawi, ndugu zake Dina, wakachukua panga zao na kuvamia mji ambao haukutazamia vita, wakaua kila mwanaume. 26 34:26Wakawaua Hamori na Shekemu mwanawe kwa upanga kisha wakamchukua Dina kutoka nyumba ya Shekemu na kuondoka. 27 34:27Wana wa Yakobo walipita juu ya maiti katika kuteka nyara mji ule ambamo dada yao alikuwa amenajisiwa. 28 34:28Wakachukua kondoo na mbuzi, ngʼombe, punda na kila kitu kilichokuwa chao ndani ya mji ule na mashambani. 29 34:29Walichukua utajiri wao wote pamoja na wanawake na watoto wao, wakachukua nyara kila kitu ndani ya nyumba zao.

    30 34:30Kisha Yakobo akawaambia Simeoni na Lawi, “Mmeleta taabu kwangu kwa kunifanya ninuke kama uvundo kwa Wakanaani na Waperizi, watu waishio katika nchi hii. Sisi ni wachache, kama wakiunganisha nguvu zao dhidi yangu na kunishambulia, mimi na nyumba yangu tutaangamizwa.”

    31 34:31Lakini wakamjibu, “Je, ilikuwa vyema kumtendea dada yetu kama kahaba?”

    35Yakobo Arudi Betheli

    1 35:1Kisha Mungu akamwambia Yakobo, “Panda uende Betheli ukakae huko na ukamjengee Mungu madhabahu huko, Yeye aliyekutokea ulipokuwa unamkimbia Esau ndugu yako.”

    2 35:2Hivyo Yakobo akawaambia watu wa nyumbani mwake pamoja na wote waliokuwa naye, “Iondoeni miungu ya kigeni ile iliyoko katikati yenu, jitakaseni na mkabadilishe nguo zenu. 3 35:3Kisha njooni, twende Betheli, mahali nitakapomjengea Mungu madhabahu, aliyenijibu katika siku ya shida yangu, ambaye amekuwa pamoja nami popote nilipokwenda.” 4 35:4Kwa hiyo wakampa Yakobo miungu yote ya kigeni waliyokuwa nayo, pamoja na pete zilizokuwa masikioni mwao. Yakobo akavizika chini ya mti wa mwaloni huko Shekemu. 5 35:5Kisha wakaondoka, na hofu ya Mungu ikawapata miji yote iliyowazunguka. Kwa hiyo hakuna aliyewafuatia wana wa Yakobo.

    6 35:6Yakobo na watu wote waliokuwa pamoja naye wakafika Luzu (ndio Betheli), katika nchi ya Kanaani. 7 35:7Huko akajenga madhabahu na akapaita mahali pale El-Betheli, 35:7 El-Betheli maana yake Mungu wa Betheli. kwa sababu mahali pale ndipo Mungu alipojifunua kwake alipokuwa akimkimbia ndugu yake.

    8 35:8Wakati huu Debora, mlezi wa Rebeka, akafa na akazikwa chini ya mti wa mwaloni ulioko chini ya Betheli. Kwa hiyo pakaitwa Alon-Bakuthi. 35:8 Alon-Bakuthi maana yake Mwaloni wa Kilio.

    9 35:9Baada ya Yakobo kurudi kutoka Padan-Aramu, Mungu alimtokea tena na kumbariki. 10 35:10Mungu akamwambia, “Jina lako ni Yakobo, lakini hutaitwa tena Yakobo, jina lako utakuwa Israeli.” Kwa hiyo akamwita Israeli.

    11 35:11Mungu akamwambia, “Mimi ndimi Mungu Mwenyezi, 35:11 Mungu Mwenyezi hapa ni jina la Kiebrania, El-Shaddai (yaani Mungu Mwenye utoshelevu wote). ukazae na kuongezeka. Taifa na jamii ya mataifa itatoka kwako, nao wafalme watatoka viunoni mwako. 12 35:12Nchi niliyowapa Abrahamu na Isaki nakupa wewe pia, nami nitawapa wazao wako baada yako.” 13 35:13Kisha Mungu akapanda juu kutoka kwake mahali pale alipozungumza naye.

    14 35:14Yakobo akasimamisha nguzo ya jiwe mahali pale Mungu alipozungumza naye, akamimina sadaka ya kinywaji juu yake, pia akamimina mafuta juu yake. 15 35:15Yakobo akapaita mahali pale Mungu alipozungumza naye Betheli. 35:15 Betheli maana yake Nyumba ya Mungu.

    Vifo Vya Raheli Na Isaki

    16 35:16Kisha wakaondoka Betheli. Walipokuwa umbali fulani kabla ya kufika Efrathi, Raheli akaanza kusikia uchungu na alipata shida kuu. 17 35:17Alipokuwa katika shida hii katika kujifungua, mkunga akamwambia, “Usiogope, kwa sababu umempata mwana mwingine.” 18 35:18Hapo alipopumua pumzi yake ya mwisho, kwa maana alikuwa akifa, akamwita mwanawe Benoni. 35:18 Benoni maana yake Mwana wa huzuni yangu. Lakini babaye akamwita Benyamini. 35:18 Benyamini maana yake Mwana wa mkono wangu wa kuume.

    19 35:19Kwa hiyo Raheli akafa, akazikwa kando ya njia iendayo Efrathi (ndio Bethlehemu). 20 35:20Juu ya kaburi lake, Yakobo akasimamisha nguzo, ambayo mpaka leo inatambulisha kaburi la Raheli.

    21 35:21Israeli akaendelea tena na safari yake na kupiga hema mbele mnara wa Ederi. 22 35:22Wakati Israeli alipokuwa akiishi katika nchi ile, Reubeni mwanawe alikutana kimwili na suria wa baba yake aitwaye Bilha, naye Israeli akasikia jambo hili.

    Yakobo alikuwa na wana kumi na wawili:
  • 23 35:23Wana wa Lea walikuwa:
  • Reubeni mzaliwa wa kwanza wa Yakobo, Simeoni, Lawi, Yuda, Isakari na Zabuloni.
  • 24 35:24Wana wa Raheli walikuwa:
  • Yosefu na Benyamini.
  • 25 35:25Wana waliozaliwa na Bilha mtumishi wa kike wa Raheli walikuwa:
  • Dani na Naftali.
  • 26 35:26Wana waliozaliwa na Zilpa mtumishi wa kike wa Lea walikuwa:
  • Gadi na Asheri.

    Hawa walikuwa wana wa Yakobo, waliozaliwa kwake akiwa Padan-Aramu.

    27 35:27Yakobo akarudi nyumbani kwa baba yake Isaki huko Mamre, karibu na Kiriath-Arba (yaani Hebroni), ambapo walikuwa wameishi Abrahamu na Isaki. 28 35:28Isaki aliishi miaka 180. 29 35:29Kisha Isaki akapumua pumzi yake ya mwisho akafa, akakusanywa pamoja na watu wake akiwa mzee wa miaka mingi. Nao wanawe Esau na Yakobo wakamzika.

    36Wazao Wa Esau (1 Nyakati 1:34-42)

    1 36:1Hivi ndivyo vizazi vya Esau (yaani Edomu).

    2 36:2Esau akaoa wake kutoka miongoni mwa wanawake wa Kanaani: Ada binti wa Eloni Mhiti, Oholibama binti wa Ana, mjukuu wa kike wa Sibeoni Mhivi, 3 36:3pia akaoa Basemathi binti wa Ishmaeli, dada yake Nebayothi. 4 36:4Ada akamzalia Esau Elifazi, Basemathi akamzaa Reueli, 5 36:5Oholibama akamzaa Yeushi, Yalamu na Kora. Hawa ndio wana wa Esau waliozaliwa kwake huko Kanaani. 6 36:6Esau akawachukua wake zake, watoto wake wa kiume na wa kike na wote wa nyumbani mwake, mifugo yake pamoja na wanyama wake wengine wote na mali yake yote ambayo alikuwa ameipata akiwa Kanaani, akahamia katika nchi iliyo mbali na Yakobo ndugu yake. 7 36:7Mali zao zilikuwa nyingi sana kiasi kwamba haikuwa rahisi wao kuishi pamoja, nchi waliyokuwa wakiishi isingewatosha wote kwa ajili ya mifugo yao. 8 36:8Kwa hiyo Esau (ambaye ni Edomu) aliishi katika nchi ya kilima huko Seiri.

    9 36:9Hawa ndio wazao wa Esau, baba wa Waedomu, katika nchi ya kilima cha Seiri.

  • 10 36:10Haya ndiyo majina ya wana wa Esau:
  • Elifazi, mwana wa Esau ambaye mkewe Ada alimzalia; na Reueli, mwana wa Esau ambaye mkewe Basemathi alimzalia.
  • 11 36:11Wana wa Elifazi ni:
  • Temani, Omari, Sefo, Gatamu na Kenazi. 12 36:12Elifazi mwana wa Esau alikuwa pia na suria aliyeitwa Timna, ambaye alimzalia Amaleki. Hawa ndio waliokuwa wajukuu wa Ada mke wa Esau.
  • 13 36:13Wana wa Reueli ni:
  • Nahathi, Zera, Shama na Miza. Hawa ndio waliokuwa wajukuu wa Basemathi mkewe Esau. 14 36:14Wana wa Oholibama binti Ana, mkewe Esau, aliyekuwa mjukuu wa Sibeoni, aliomzalia Esau ni: Yeushi, Yalamu na Kora.

    15 36:15Hawa ndio waliokuwa wakuu miongoni mwa wazao wa Esau:

  • Wakuu wa wana wa Elifazi, mzaliwa wa kwanza wa Esau ni:
  • Temani, Omari, Sefo, Kenazi, 16 36:16Kora, Gatamu na Amaleki. Hawa ndio waliokuwa wakuu waliotoka kwa Elifazi huko Edomu, waliokuwa wajukuu wa kiume wa Ada.
  • 17 36:17Wakuu wa wana wa Reueli, mwana wa Esau ni:
  • Nahathi, Zera, Shama na Miza. Hawa ndio wakuu waliotoka kwa Reueli huko Edomu, waliokuwa wajukuu wa kiume wa Basemathi mkewe Esau.
  • 18 36:18Wakuu wa wana wa Esau ambao mkewe Oholibama alimzalia ni:
  • Yeushi, Yalamu na Kora. Hawa ndio wakuu waliotoka kwa mke wa Esau, Oholibama binti Ana.

    19 36:19Hawa ndio waliokuwa wana wa Esau (ndiye Edomu), na hawa ndio waliokuwa wakuu wao.

    20 36:20Hawa ndio walikuwa wana wa Seiri, Mhori, waliokuwa wakiishi katika nchi ile:

    Lotani, Shobali, Sibeoni, Ana, 21 36:21Dishoni, Eseri na Dishani. Hawa ndio wana wa Seiri huko Edomu waliokuwa wakuu kwa Wahori.
  • 22 36:22Wana wa Lotani walikuwa:
  • Hori na Homamu. Timna alikuwa dada yake Lotani.
  • 23 36:23Wana wa Shobali walikuwa:
  • Alvani, Manahathi, Ebali, Shefo na Onamu.
  • 24 36:24Wana wa Sibeoni walikuwa:
  • Aiya na Ana. Huyu Ana ndiye aligundua chemchemi ya maji moto jangwani alipokuwa akichunga punda za Sibeoni baba yake.
  • 25 36:25Watoto wa Ana walikuwa:
  • Dishoni na Oholibama binti wa Ana.
  • 26 36:26Wana wa Dishoni walikuwa:
  • Hemdani, Eshbani, Ithrani na Kerani.
  • 27 36:27Wana wa Eseri walikuwa:
  • Bilhani, Zaavani na Akani.
  • 28 36:28Wana wa Dishani walikuwa:
  • Usi na Arani.
  • 29 36:29Hawa ndio waliokuwa wakuu wa Wahori:
  • Lotani, Shobali, Sibeoni, Ana, 30 36:30Dishoni, Eseri na Dishani. Hawa ndio walikuwa wakuu wa Wahori, kufuatana na makundi yao, katika nchi ya Seiri. Watawala Wa Edomu (1 Nyakati 1:43-54)

    31 36:31Wafuatao ni wafalme waliotawala Edomu kabla ya mfalme yeyote wa Israeli kutawala:

    32 36:32Bela mwana wa Beori alikuwa mfalme wa Edomu. Mji wake uliitwa Dinhaba.
  • 33 36:33Bela alipofariki, Yobabu mwana wa Zera kutoka Bosra akawa mfalme baada yake.
  • 34 36:34Yobabu alipofariki, Hushamu kutoka nchi ya Watemani akawa mfalme baada yake.
  • 35 36:35Hushamu alipofariki, Hadadi mwana wa Bedadi, aliyeshinda Midiani katika nchi ya Moabu, akawa mfalme baada yake. Mji wake uliitwa Avithi.
  • 36 36:36Hadadi alipofariki, Samla kutoka Masreka akawa mfalme baada yake.
  • 37 36:37Samla alipofariki, Shauli kutoka Rehobothi ngʼambo ya Mto Frati akawa mfalme baada yake.
  • 38 36:38Shauli alipofariki, Baal-Hanani mwana wa Akbori akawa mfalme baada yake.
  • 39 36:39Baal-Hanani mwana wa Akbori alipofariki, Hadadi akawa mfalme baada yake. Mji wake uliitwa Pau, na mkewe aliitwa Mehetabeli binti Matredi, binti Me-Zahabu.
  • 40 36:40Hawa ndio wakuu waliotokana na Esau, kwa majina, kufuatana na koo zao na nchi zao:

    Timna, Alva, Yethethi, 41 36:41Oholibama, Ela, Pinoni, 42 36:42Kenazi, Temani, Mibsari, 43 36:43Magdieli na Iramu. Hawa ndio walikuwa wakuu wa Edomu, kufuatana na makazi yao katika nchi waliyoimiliki.

    Huyu ndiye alikuwa Esau, baba wa Waedomu.

    37Ndoto Za Yosefu

    1 37:1Yakobo akaishi Kanaani katika nchi ambayo baba yake alikuwa ameishi.

    2 37:2Zifuatazo ni habari za Yakobo.

    Yosefu, kijana wa miaka kumi na saba, alikuwa akichunga makundi ya kondoo na mbuzi pamoja na ndugu zake wa mama wengine, yaani wana wa Bilha na wana wa Zilpa wake za baba yake, naye akawa akimletea baba yake taarifa mbaya kuhusu hao ndugu zake.

    3 37:3Basi, Israeli akampenda Yosefu kuliko yeyote miongoni mwa kaka zake, kwani ni mwanawe wa uzeeni, akamshonea joho lililorembwa vizuri sana. 4 37:4Ndugu zake walipoona kwamba baba yao anampenda Yosefu kuliko yeyote mwingine miongoni mwao, walimchukia na hawakusema naye neno lolote jema.

    5 37:5Yosefu akaota ndoto, naye alipowaeleza ndugu zake, wakamchukia zaidi. 6 37:6Akawaambia, “Sikilizeni ndoto niliyoota: 7 37:7Tulikuwa tukifunga miganda ya nafaka shambani, ghafula mganda wangu ukasimama wima, wakati miganda yenu ikiuzunguka na kuuinamia.”

    8 37:8Ndugu zake wakamwambia, “Wewe unakusudia kututawala? Hivi kweli wewe utatutawala sisi?” Wakaongeza kumchukia zaidi kwa sababu ya ndoto yake pamoja na yale aliyowaambia.

    9 37:9Kisha akaota ndoto nyingine, akawaambia ndugu zake akisema, “Sikilizeni, nimeota ndoto nyingine, wakati huu jua, mwezi na nyota kumi na moja zilikuwa zinanisujudia.”

    10 37:10Alipomwambia baba yake pamoja na ndugu zake, baba yake akamkemea akisema, “Ni ndoto gani hii uliyoota? Hivi kweli mama yako na mimi na ndugu zako tutakuja kukusujudia wewe hadi nchi?” 11 37:11Ndugu zake wakamwonea wivu, lakini baba yake akaliweka jambo hilo moyoni.

    Yosefu Auzwa Na Ndugu Zake

    12 37:12Basi, ndugu zake walikuwa wamekwenda kuchunga makundi ya baba yao karibu na Shekemu, 13 37:13naye Israeli akamwambia Yosefu, “Kama ujuavyo, ndugu zako wanachunga makundi huko karibu na Shekemu. Njoo, nitakutuma kwao.”

    Yosefu akajibu, “Vema sana, niko tayari.”

    14 37:14Kwa hiyo akamwambia, “Nenda uone kama mambo yote ni salama kwa ndugu zako na makundi, kisha uniletee habari.” Ndipo akamtuma Yosefu kutoka Bonde la Hebroni.

    Yosefu alipofika Shekemu, 15 37:15mtu mmoja akamkuta akizungukazunguka mashambani na akamuuliza, “Unatafuta nini?”

    16 37:16Akajibu, “Ninawatafuta ndugu zangu. Unaweza kuniambia wanachunga wapi makundi yao?”

    17 37:17Yule mtu akajibu, “Wamehama hapa. Nilisikia wakisema, ‘Twende Dothani.’ ”

    Kwa hiyo Yosefu akawafuatilia ndugu zake na kuwakuta karibu na Dothani. 18 37:18Ndugu zake walipomwona akiwa mbali, kabla hajawafikia, wakapanga shauri baya la kumuua.

    19 37:19Wakaambiana, “Yule mwota ndoto anakuja! 20 37:20Njooni sasa, tumuue na kumtupa katika shimo mojawapo na tuseme kwamba mnyama mkali amemrarua. Kisha tutaona matokeo ya ndoto zake.”

    21 37:21Reubeni aliposikia jambo hili, akajaribu kumwokoa kutoka mikononi mwao akasema, “Tusiutoe uhai wake. 22 37:22Tusimwage damu yoyote. Mtupeni katika shimo lililoko hapa jangwani, lakini msimguse.” Reubeni alisema hivyo ili amwokoe kutoka mikononi mwao, kisha amrudishe nyumbani kwa baba yake.

    23 37:23Kwa hiyo Yosefu alipowafikia ndugu zake, walimvua lile joho lake, lile joho lililorembwa vizuri alilokuwa amevaa. 24 37:24Kisha wakamchukua wakamtupa katika shimo. Wakati huo shimo lilikuwa tupu, halikuwa na maji ndani yake.

    25 37:25Walipokaa ili wale chakula chao, wakainua macho wakaona msafara wa Waishmaeli ukija kutoka Gileadi. Ngamia wao walikuwa wamepakizwa mizigo ya vikolezo, uvumba na manemane, nao walikuwa njiani kuvipeleka Misri.

    26 37:26Yuda akawaambia ndugu zake, “Tutafaidi nini ikiwa tutamuua ndugu yetu na kuificha damu yake? 27 37:27Njooni, tumuuze kwa hawa Waishmaeli. Tusimguse, kwa kuwa hata hivyo yeye ni ndugu yetu, nyama yetu na damu yetu wenyewe.” Ndugu zake wakakubali.

    28 37:28Kwa hiyo wale wafanyabiashara Wamidiani walipofika pale, ndugu zake wakamtoa Yosefu kutoka kwenye lile shimo, na kumuuza kwa shekeli ishirini 37:28 Shekeli 20 ni sawa na gramu 200. za fedha kwa wale Waishmaeli, ambao walimpeleka Misri.

    29 37:29Reubeni aliporudi kutazama kwenye lile shimo na kuona kwamba Yosefu hayupo, alirarua nguo zake. 30 37:30Akawarudia ndugu zake na kusema, “Kijana hayuko mle! Nielekee wapi sasa?”

    31 37:31Kisha wakalichukua lile joho la Yosefu, wakachinja mbuzi na kulichovya katika damu. 32 37:32Wakalichukua lile joho lililorembwa vizuri na kulipeleka kwa baba yao na kusema, “Tumeliokota hili joho. Uchunguze uone kama ni la mwanao.”

    33 37:33Baba yao akalitambua akasema, “Hili ni joho la mwanangu! Mnyama mkali amemrarua. Hakika Yosefu ameraruliwa vipande vipande.”

    34 37:34Kisha Yakobo akararua nguo zake, akavaa nguo ya gunia na kumwombolezea mwanawe kwa siku nyingi. 35 37:35Wanawe wote na binti zake wakaja kumfariji, lakini hakukubali kufarijiwa. Akasema, “Hapana, nitamwombolezea mwanangu mpaka nimfikie kaburini.” Kwa hiyo baba yake akaendelea kumlilia.

    36 37:36Wakati ule ule, Wamidiani wakamuuza Yosefu huko Misri kwa Potifa, mmojawapo wa maafisa wa Farao, aliyekuwa mkuu wa ulinzi.

    38Yuda Na Tamari

    1 38:1Wakati ule, Yuda akawaacha ndugu zake, akaenda kuishi na Hira Mwadulami. 2 38:2Huko Yuda akakutana na binti wa Kikanaani aitwaye Shua, akamwoa na akakutana naye kimwili, 3 38:3akapata mimba, akamzaa mwana, ambaye alimwita Eri. 4 38:4Akapata mimba tena, akamzaa mwana na kumwita Onani. 5 38:5Akamzaa mwana mwingine tena, akamwita Shela. Huyu alimzalia mahali paitwapo Kezibu.

    6 38:6Yuda akampatia Eri, mzaliwa wake wa kwanza, mke aitwaye Tamari. 7 38:7Lakini Eri, mzaliwa wa kwanza wa Yuda, alikuwa mwovu machoni pa Bwana, kwa hiyo Bwana akamuua.

    8 38:8Kisha Yuda akamwambia Onani, “Kutana kimwili na mke wa ndugu yako, na utimize wajibu wako kwake kama mke wa ndugu yako, ili umpatie ndugu yako uzao.” 9 38:9Lakini Onani alijua kwamba uzao haungekuwa wake, kwa hiyo kila alipokutana kimwili na mke wa ndugu yake, alimwaga chini mbegu za kiume ili asimpatie ndugu yake uzao. 10 38:10Alichofanya kilikuwa kiovu machoni pa Bwana, hivyo, pia Bwana akamuua Onani.

    11 38:11Kisha Yuda akamwambia Tamari mkwewe, “Ishi kama mjane nyumbani mwa baba yako mpaka mwanangu Shela atakapokua.” Kwa maana alifikiri, “Angeweza kufa pia kama ndugu zake.” Kwa hiyo Tamari alikwenda kuishi nyumbani kwa baba yake.

    12 38:12Baada ya muda mrefu mke wa Yuda binti wa Shua akafariki. Baada ya msiba, Yuda alikwenda Timna, kwa watu waliokuwa wakikata kondoo wake manyoya, naye alifuatana na rafiki yake Hira Mwadulami.

    13 38:13Tamari alipoambiwa, “Baba mkwe wako yuko njiani kwenda Timna kukata kondoo wake manyoya,” 14 38:14alivua mavazi yake ya ujane, akajifunika kwa shela ili asifahamike, akaketi kwenye mlango wa Enaimu, ambao upo njiani kuelekea Timna. Akafanya hivyo kwa sababu aliona kwamba, ingawa Shela amekua, lakini alikuwa hajakabidhiwa kwake kuwa mkewe.

    15 38:15Yuda alipomwona alifikiri ni kahaba, kwa sababu alikuwa amefunika uso wake. 16 38:16Pasipo kutambua kwamba alikuwa mkwe wake, akamwendea kando ya njia na kumwambia, “Njoo sasa, nikutane na wewe kimwili.”

    Yule mkwewe akamuuliza, “Utanipa nini nikikutana nawe kimwili?”

    17 38:17Akamwambia, “Nitakutumia mwana-mbuzi kutoka kundi langu.”

    Akamuuliza, “Utanipa kitu chochote kama amana mpaka utakapompeleka?”

    18 38:18Akamuuliza, “Nikupe amana gani?”

    Akamjibu, “Pete yako na kamba yake pamoja na fimbo iliyo mkononi mwako.” Kwa hiyo akampa vitu hivyo kisha akakutana naye kimwili, naye akapata mimba yake. 19 38:19Tamari akaondoka, akavua shela yake akavaa tena nguo zake za ujane.

    20 38:20Wakati ule ule, Yuda akamtuma rafiki yake Mwadulami apeleke yule mwana-mbuzi ili arudishiwe amana yake kutoka kwa yule mwanamke, lakini yule rafiki yake hakumkuta yule mwanamke. 21 38:21Akawauliza watu wanaoishi mahali pale, “Yuko wapi yule kahaba wa mahali pa kuabudia miungu aliyekuwa kando ya barabara hapa Enaimu?”

    Wakamjibu, “Hajawahi kuwepo mwanamke yeyote kahaba wa mahali pa kuabudia miungu hapa.”

    22 38:22Kwa hiyo akamrudia Yuda na kumwambia, “Sikumpata. Zaidi ya hayo, watu wanaoishi mahali pale walisema ‘Hapakuwahi kuwepo mwanamke yeyote kahaba wa mahali pa kuabudia miungu hapa.’ ”

    23 38:23Kisha Yuda akasema, “Mwache avichukue vitu hivyo, ama sivyo tutakuwa kichekesho. Hata hivyo, nilimpelekea mwana-mbuzi, lakini hukumkuta.”

    24 38:24Baada ya miezi mitatu Yuda akaambiwa, “Tamari mkweo ana hatia ya kuwa kahaba, na matokeo yake ana mimba.”

    Yuda akasema, “Mtoeni nje na achomwe moto hadi afe!”

    25 38:25Alipokuwa akitolewa nje, akatuma ujumbe kwa baba mkwe wake kusema, “Nina mimba ya mtu mwenye vitu hivi.” Akaongeza kusema, “Angalia kama utatambua kwamba pete hii na kamba yake pamoja na fimbo hii ni vya nani.”

    26 38:26Yuda akavitambua na kusema, “Yeye ana haki kuliko mimi, kwa kuwa sikumkabidhi kwa mwanangu Shela ili awe mkewe.” Tangu hapo hakukutana naye kimwili tena.

    27 38:27Wakati ulipofika wa kujifungua, kukawa na wana mapacha tumboni mwake. 28 38:28Alipokuwa akijifungua, mmoja akatoa mkono wake nje, kwa hiyo mkunga akachukua uzi mwekundu na kuufunga mkononi mwa yule mtoto, akasema, “Huyu ametoka kwanza.” 29 38:29Lakini alipourudisha mkono wake ndugu yake akaanza kutoka, naye akasema, “Hivi ndivyo ulivyotoka kwa nguvu!” Akaitwa Peresi. 30 38:30Kisha ndugu yake, aliyekuwa na uzi mwekundu mkononi, akatoka, naye akaitwa Zera.

    39Yosefu Na Mke Wa Potifa

    1 39:1Wakati huu Yosefu alikuwa amechukuliwa mpaka Misri. Mmisri aliyeitwa Potifa aliyekuwa mmojawapo wa maafisa wa Farao, mkuu wa ulinzi, akamnunua Yosefu kutoka kwa Waishmaeli waliomleta Misri.

    2 39:2 Bwana alikuwa pamoja na Yosefu, naye akastawi, Yosefu akaishi nyumbani kwa bwana wake Mmisri. 3 39:3Potifa alipoona kuwa Bwana alikuwa pamoja na Yosefu na kwamba Bwana alimfanikisha kwa kila kitu alichokifanya, 4 39:4Yosefu alipata kibali machoni pa Potifa, akamfanya mhudumu wake. Potifa akamweka kuwa msimamizi wa nyumba yake, naye akamkabidhi kuwa mwangalizi wa kila kitu alichokuwa nacho. 5 39:5Kuanzia wakati huo Potifa alipomweka Yosefu kuwa msimamizi wa nyumba na mali zake zote alizokuwa nazo, Bwana aliibariki nyumba ya Mmisri huyo kwa sababu ya Yosefu. Baraka ya Bwana ilikuwa juu ya kila kitu alichokuwa nacho Potifa, nyumbani na shambani. 6 39:6Kwa hiyo Potifa akamwachia Yosefu uangalizi wa kila kitu alichokuwa nacho, Yosefu alipokuwa katika uongozi, Potifa hakuwa na sababu ya kujishughulisha na kitu chochote isipokuwa chakula alichokula.

    Yosefu alikuwa mwenye umbo zuri na sura ya kuvutia; 7 39:7baada ya kitambo mke wa Potifa akamtamani Yosefu, akamwambia, “Njoo, ukutane nami kimwili!”

    8 39:8Lakini Yosefu akakataa. Akamwambia yule mwanamke, “Mimi nikiwa katika uongozi, bwana wangu hahusiki na kitu chochote katika nyumba hii, kila kitu alicho nacho amenikabidhi. 9 39:9Hapa nyumbani hakuna aliye mkuu kuliko mimi. Bwana wangu hakunizuilia kitu chochote isipokuwa wewe, kwa kuwa wewe ni mke wake. Nitawezaje basi kufanya uovu huu na kutenda dhambi dhidi ya Mungu?” 10 39:10Ingawa yule mwanamke aliendelea kumshawishi Yosefu siku baada ya siku, Yosefu alikataa kukutana naye kimwili wala kukaa karibu naye.

    11 39:11Siku moja Yosefu akaingia ndani ya nyumba kufanya kazi zake, wala hapakuwepo na mfanyakazi yeyote ndani ya nyumba. 12 39:12Mke wa Potifa akashika vazi Yosefu alilokuwa amevaa, akamwambia, “Njoo tukutane kimwili!” Lakini Yosefu akaacha vazi lake mkononi mwa huyo mwanamke, akatoka nje ya nyumba akikimbia.

    13 39:13Yule mwanamke alipoona kwamba Yosefu amemwachia vazi lake mkononi na kukimbilia nje ya nyumba, 14 39:14akawaita watumishi wake wa nyumbani, akawaambia, “Tazameni! Huyu Mwebrania ameletwa hapa kutudhihaki! Aliingia hapa ndani ili akutane nami kimwili, lakini nikapiga kelele. 15 39:15Aliposikia kelele za kuomba msaada, akaacha vazi lake kando yangu akakimbilia nje.”

    16 39:16Yule mwanamke akaliweka lile vazi karibu naye mpaka Potifa aliporudi nyumbani. 17 39:17Ndipo akamweleza kisa hiki, akisema: “Yule mtumwa wa Kiebrania uliyetuletea alinijia ili kunidhihaki. 18 39:18Lakini mara nilipopiga kelele kuomba msaada, akaliacha vazi lake kando yangu akakimbia nje ya nyumba.”

    19 39:19Potifa aliposikia kisa hiki mkewe alichomweleza, akisema, “Hivi ndivyo mtumwa wako alivyonitenda.” Hasira ya Potifa ikawaka. 20 39:20Potifa akamchukua Yosefu na kumweka gerezani, mahali ambapo wahalifu wa mfalme walikuwa wamefungwa.

    Lakini wakati Yosefu alipokuwa huko gerezani, 21 39:21 Bwana alikuwa pamoja naye, akamhurumia na kumpa kibali mbele ya msimamizi wa gereza. 22 39:22Kwa hiyo msimamizi wa gereza akamweka Yosefu awe mkuu wa wafungwa pamoja na kusimamia yote ambayo yalitendeka mle gerezani. 23 39:23Msimamizi wa gereza hakujishughulisha tena na kitu chochote kilichokuwa chini ya uangalizi wa Yosefu, kwa sababu Bwana alikuwa pamoja na Yosefu akimfanikisha kwa kila alichofanya.

    40Mnyweshaji Na Mwokaji

    1 40:1Baada ya muda, mnyweshaji na mwokaji wa mfalme wa Misri, wakamkosea bwana wao, mfalme wa Misri. 2 40:2Farao akawakasirikia hawa maafisa wake wawili, mnyweshaji mkuu na mwokaji mkuu, 3 40:3akawaweka chini ya ulinzi katika nyumba ya mkuu wa kikosi cha ulinzi katika gereza lile lile alimofungwa Yosefu. 4 40:4Mkuu wa kikosi cha ulinzi akawakabidhi kwa Yosefu, naye akawahudumia.

    Walipokuwa wamekaa chini ya ulinzi kwa muda, 5 40:5kila mmoja wa hao wawili waliokuwa wamewekwa gerezani, yaani mnyweshaji na mwokaji wa mfalme wa Misri, waliota ndoto usiku mmoja, na kila ndoto ilikuwa na maana yake tofauti.

    6 40:6Yosefu alipowajia asubuhi yake, akawaona kwamba walikuwa na huzuni. 7 40:7Ndipo Yosefu akawauliza maafisa hao wa Farao waliokuwa chini ya ulinzi pamoja naye nyumbani mwa bwana wake, akasema, “Mbona nyuso zenu zimejaa huzuni leo?”

    8 40:8Wakamjibu, “Sisi sote tuliota ndoto, lakini hapakuwa na mtu yeyote wa kuzifasiri.”

    Ndipo Yosefu akawaambia, “Je, kufasiri ndoto si kazi ya Mungu? Niambieni ndoto zenu.”

    9 40:9Basi mkuu wa wanyweshaji akamweleza Yosefu ndoto yake. Akamwambia, “Katika ndoto yangu niliona mzabibu mbele yangu, 10 40:10nao mzabibu ulikuwa na matawi matatu. Mara tu ulipoanza kuchipua, maua yalichanua na vishada vyake vikawa zabibu zilizoiva. 11 40:11Kikombe cha Farao kilikuwa mkononi mwangu, nikazitwaa zabibu, nikazikamua katika kikombe cha Farao, na nikaweka kikombe mkononi mwake.”

    12 40:12Yosefu akamwambia, “Hii ndiyo maana yake: Matawi matatu ni siku tatu. 13 40:13Katika siku hizi tatu, Farao atakutoa gerezani na kukuweka tena kwenye nafasi yako, nawe utaweka kikombe cha Farao mikononi mwake, kama vile ulivyokuwa unafanya ulipokuwa mnyweshaji wake. 14 40:14Lakini wakati mambo yatakapokuwia mazuri, unikumbuke, unifanyie wema, useme mema juu yangu kwa Farao ili niondoke huku gerezani. 15 40:15Kwa maana nilichukuliwa kwa nguvu kutoka nchi ya Waebrania, na hata hapa nilipo sikufanya lolote linalostahili niwekwe gerezani.”

    16 40:16Yule mwokaji mkuu alipoona kuwa Yosefu amefasiri ikiwa na maana nzuri, akamwambia Yosefu, “Mimi pia niliota ndoto: Kichwani mwangu kulikuwepo vikapu vitatu vya mikate. 17 40:17Katika kikapu cha juu kulikuwa na aina zote za vyakula vilivyookwa kwa ajili ya Farao, lakini ndege walikuwa wakivila kutoka kwenye kikapu nilichokuwa nimebeba kichwani.”

    18 40:18Yosefu akamwambia, “Hii ndiyo maana yake: Vikapu vitatu ni siku tatu. 19 40:19Katika siku hizi tatu, Farao atakata kichwa chako na kukutundika juu ya mti. Nao ndege watakula nyama ya mwili wako.”

    20 40:20Mnamo siku ya tatu, ilikuwa kumbukumbu ya kuzaliwa kwa Farao, naye akawaandalia maafisa wake wote karamu. Akawatoa gerezani mnyweshaji mkuu na mwokaji mkuu, akawaweka mbele ya maafisa wake: 21 40:21Ndipo akamrudisha mnyweshaji mkuu kwenye nafasi yake, ili aweke kikombe mikononi mwa Farao tena, 22 40:22lakini akamwangika yule mwokaji mkuu, sawasawa na jinsi Yosefu alivyowaambia katika tafsiri yake.

    23 40:23Pamoja na hayo, mnyweshaji mkuu hakumkumbuka Yosefu, bali alimsahau.

    41Ndoto Za Farao

    1 41:1Baada ya miaka miwili kamili kupita, Farao aliota ndoto: Tazama alikuwa amesimama kando ya Mto Naili, 2 41:2wakati ngʼombe saba, wazuri na wanono, walitokea mtoni wakajilisha kwenye matete. 3 41:3Baada yao ngʼombe wengine saba, wabaya na waliokonda, wakatokea mtoni Naili wakasimama kando ya wale wanono ukingoni mwa mto. 4 41:4Wale ngʼombe wabaya na waliokonda wakawala wale saba wazuri na wanono. Kisha Farao akaamka.

    5 41:5Farao akaingia usingizini tena akaota ndoto ya pili: Akaona masuke saba ya nafaka, yenye afya na mazuri, yanakua katika bua moja. 6 41:6Baadaye, masuke mengine saba yakachipua, yakiwa membamba yaliyonyaushwa na upepo wa mashariki. 7 41:7Masuke yale membamba yakameza yale masuke saba yenye afya na yaliyojaa. Basi Farao akaamka kutoka usingizini, kumbe ilikuwa ndoto.

    8 41:8Asubuhi yake, alifadhaika akilini, hivyo akawaita waaguzi wote pamoja na watu wenye busara wa Misri. Walipokuja, Farao akawaeleza ndoto zake, lakini hakuna hata mmoja aliyeweza kumfasiria.

    9 41:9Ndipo mnyweshaji mkuu alipomwambia Farao, “Leo nimekumbushwa kuhusu kosa langu. 10 41:10Wakati fulani Farao aliwakasirikia watumishi wake, akanifunga mimi na mwokaji mkuu katika nyumba ya mkuu wa ulinzi. 11 41:11Kila mmoja wetu aliota ndoto katika usiku mmoja na kila ndoto ilikuwa na maana yake tofauti. 12 41:12Basi kijana wa Kiebrania aliyekuwa pamoja nasi huko, alikuwa mtumishi wa mkuu wa kikosi cha ulinzi. Tulimweleza ndoto zetu, naye akatufasiria, akitupa kila mtu tafsiri ya ndoto yake. 13 41:13Nayo mambo yakawa sawa kabisa na jinsi alivyotufasiria ndoto zetu: Mimi nilirudishwa kazini mwangu na huyo mtu mwingine akaangikwa.”

    14 41:14Basi, Farao akatuma Yosefu aitwe, naye akatolewa kifungoni haraka. Baada ya kunyoa na kubadilisha nguo zake akaenda mbele ya Farao.

    15 41:15Farao akamwambia Yosefu, “Nimeota ndoto, wala hakuna mtu hata mmoja anayeweza kuifasiri. Lakini nimesikia ikisemwa kwa habari yako kwamba unapoelezwa ndoto waweza kuifasiri.”

    16 41:16Yosefu akamjibu Farao, “Siwezi kuifasiri, lakini Mungu atampa Farao jibu analolihitaji.”

    17 41:17Kisha Farao akamwambia Yosefu, “Katika ndoto yangu nilikuwa nimesimama ukingoni mwa Mto Naili, 18 41:18nikawaona ngʼombe saba, wazuri na wanono, wakijitokeza kutoka mtoni wakaja kujilisha kwenye matete. 19 41:19Baada ya hao, ngʼombe wengine saba wadhaifu wakatokea, wabaya sana na waliokonda. Kamwe sikuwahi kuona ngʼombe wabaya jinsi hiyo katika nchi yote ya Misri. 20 41:20Hao ngʼombe waliokonda na wabaya sana wakawala wale ngʼombe saba walionona waliojitokeza kwanza. 21 41:21Lakini hata baada ya kuwala, hakuna mtu ambaye angeweza kusema kwamba wamekula, bado walionekana wabaya kama mwanzoni. Kisha nikaamka kutoka usingizini.

    22 41:22“Pia katika ndoto zangu niliona masuke saba ya nafaka, yamejaa na mazuri, yanakua katika bua moja. 23 41:23Baada ya hayo masuke mengine saba yakachipua, yaliyonyauka, membamba na yamekaushwa na upepo wa mashariki. 24 41:24Yale masuke membamba ya nafaka yakayameza yale masuke saba mazuri yaliyojaa nafaka. Nimewaeleza waaguzi, wala hakuna yeyote aliyeweza kunifasiria.”

    25 41:25Ndipo Yosefu akamwambia Farao, “Ndoto za Farao ni ndoto iyo hiyo moja. Mungu amemfunulia Farao jambo analokusudia kufanya karibuni. 26 41:26Ngʼombe saba wazuri ni miaka saba, nayo masuke saba mazuri yaliyojaa nafaka ni miaka saba, ni ndoto iyo hiyo moja. 27 41:27Ngʼombe saba waliokonda na wabaya wale waliojitokeza baadaye ni miaka saba, vivyo hivyo masuke saba ya ngano yaliyodhoofika na kukaushwa na upepo wa mashariki, ni miaka saba ya njaa.

    28 41:28“Ni kama vile nilivyomwambia Farao: Mungu amemwonyesha Farao jambo analokusudia kufanya karibuni. 29 41:29Miaka saba ya neema inakuja katika nchi yote ya Misri, 30 41:30lakini itafuata miaka saba ya njaa. Ndipo neema yote ya Misri itasahaulika na njaa itaikumba nchi.

    31 41:31“Neema iliyokuwa katika nchi haitakumbukwa, kwa sababu njaa itakayofuata itakuwa kali mno. 32 41:32Sababu ya ndoto kumjia Farao kwa namna mbili ni kwamba jambo hilo Mungu ameshaamua kwa hakika, naye Mungu atalifanya karibuni.

    33 41:33“Basi sasa Farao na atafute mtu mwenye akili na hekima ili amweke kuwa msimamizi wa nchi ya Misri. 34 41:34Farao na aweke wenye amri nchini kote wakusanye sehemu ya tano ya mavuno ya Misri katika miaka hii saba ya neema. 35 41:35Wakusanye chakula chote katika miaka hii saba ya neema inayokuja na kuhifadhi nafaka chini ya mamlaka ya Farao, iwe akiba ya chakula katika miji. 36 41:36Chakula hiki kitakuwa akiba ya tahadhari kwa ajili ya nchi, ili kitumike katika ile miaka saba ya njaa itakayokuja Misri, ili nchi isiharibiwe na njaa.”

    37 41:37Mpango huu ulionekana mzuri kwa Farao na kwa maafisa wake wote. 38 41:38Hivyo Farao akawauliza, “Je tunaweza kumpata yeyote kama mtu huyu, ambaye Roho wa Mungu yumo ndani yake?”

    39 41:39Ndipo Farao akamwambia Yosefu, “Maadamu Mungu amekufunulia yote haya, hakuna mwingine yeyote mwenye akili na hekima kama wewe. 40 41:40Wewe utakuwa msimamizi wa jumba langu la kifalme, na watu wangu wote watatii amri zako. Ni kuhusu kiti cha ufalme tu nitakuwa mkuu kuliko wewe.”

    Yosefu Msimamizi Wa Misri

    41 41:41Kwa hiyo Farao akamwambia Yosefu, “Sasa nakuweka uwe msimamizi wa nchi yote ya Misri.” 42 41:42Ndipo Farao akaivua pete yake ya muhuri kutoka kidoleni mwake na kuivalisha katika kidole cha Yosefu. Akamvika majoho mazuri ya kitani safi na mkufu wa dhahabu shingoni mwake. 43 41:43Akampandisha katika gari lake la farasi kama msaidizi wake, watu wakatangulia wakishangilia, wakisema, “Fungueni njia!” Ndivyo Farao alivyomweka Yosefu kuwa msimamizi wa nchi yote ya Misri.

    44 41:44Kisha Farao akamwambia Yosefu, “Mimi ni Farao, lakini pasipo neno lako, hakuna mtu mwenye ruhusa kuinua mkono au mguu katika nchi yote ya Misri.” 45 41:45Farao akamwita Yosefu Safenath-Panea, pia akampa Asenathi binti Potifera, kuhani wa mji wa Oni, 41:45 Yaani Heliopoli (Mji wa Jua). kuwa mke wake. Ndipo Yosefu akaitembelea nchi yote ya Misri.

    46 41:46Yosefu alikuwa na miaka thelathini alipoingia katika utumishi wa Farao mfalme wa Misri. Naye Yosefu akatoka mbele ya Farao akasafiri katika nchi yote ya Misri. 47 41:47Katika ile miaka saba ya neema nchi ilizaa mazao kwa wingi sana. 48 41:48Yosefu akakusanya chakula chote kilichozalishwa katika ile miaka saba ya neema nchini Misri, akakihifadhi katika ghala za miji. Katika kila mji kulihifadhiwa chakula kilichozalishwa katika mashamba yaliyouzunguka mji huo. 49 41:49Yosefu alihifadhi nafaka nyingi, mfano wa mchanga wa bahari, ilikuwa nyingi mno kiasi kwamba walishindwa kuweka kumbukumbu kwa sababu akiba ilizidi sana kupita kipimo.

    50 41:50Kabla ya miaka ya njaa kuanza, Asenathi binti Potifera, kuhani wa mji wa Oni, alikuwa amemzalia Yosefu wana wawili wa kiume. 51 41:51Yosefu akamwita mzaliwa wake wa kwanza Manase, akisema, “Ni kwa sababu Mungu amenifanya nisahau taabu zangu zote pamoja na jamaa yote ya nyumba ya baba yangu.” 52 41:52Mwana wa pili akamwita Efraimu, akisema, “Ni kwa sababu Mungu amenistawisha katika nchi ya mateso yangu.”

    53 41:53Ile miaka saba ya neema huko Misri ikaisha, 54 41:54nayo miaka ile saba ya njaa ikaanza, sawasawa na alivyosema Yosefu. Kulikuwa na njaa katika nchi nyingine zote, bali katika nchi yote ya Misri kulikuwa na chakula. 55 41:55Wakati nchi yote ya Misri ilipopatwa na njaa, watu wakamlilia Farao ili awape chakula. Ndipo Farao alipowaagiza Wamisri wote, akisema, “Nendeni kwa Yosefu, nanyi mfanye anachowaambia.”

    56 41:56Wakati njaa ilipokuwa imeenea katika nchi yote, Yosefu akafungua ghala za vyakula na kuwauzia Wamisri nafaka, kwa sababu njaa ilikuwa kali mno katika nchi yote ya Misri. 57 41:57Pia nchi nyingine zote zilikuja Misri kununua nafaka kutoka kwa Yosefu, kwa sababu njaa ilikuwa kali mno duniani kote.

    42Ndugu Za Yosefu Waenda Misri

    1 42:1Wakati Yakobo alipofahamu kuwa kuna nafaka huko Misri, akawaambia wanawe, “Mbona mnakaa tu hapa mnatazamana?” 2 42:2Akaendelea kuwaambia, “Nimesikia kuwa huko Misri kuna nafaka. Telemkeni huko mkanunue chakula kwa ajili yetu, ili tuweze kuishi wala tusife.”

    3 42:3Ndipo wale ndugu kumi wa Yosefu, wakateremka huko Misri kununua nafaka. 4 42:4Lakini Yakobo hakumtuma Benyamini, ndugu yake Yosefu, pamoja na wengine, kwa sababu aliogopa asije akapatwa na madhara. 5 42:5Hivyo wana wa Israeli walikuwa miongoni mwa wale waliokwenda Misri kununua nafaka, kwani njaa ilikuwa katika nchi ya Kanaani pia.

    6 42:6Wakati huo Yosefu alikuwa mtawala wa nchi ya Misri, naye alikuwa ndiye aliwauzia watu wote nafaka. Kwa hiyo wakati ndugu zake Yosefu walipofika, wakamsujudia hadi nyuso zao zikagusa ardhi. 7 42:7Mara Yosefu alipowaona ndugu zake, akawatambua, lakini akajifanya mgeni na kuzungumza nao kwa ukali, akiwauliza, “Ninyi mnatoka wapi?”

    Wakamjibu, “Tumetoka katika nchi ya Kanaani kuja kununua chakula.”

    8 42:8Ingawa Yosefu aliwatambua ndugu zake, wao hawakumtambua. 9 42:9Ndipo Yosefu alipokumbuka ndoto zake kuwahusu wao, akawaambia, “Ninyi ni wapelelezi! Mmekuja kuangalia mahali ambapo nchi yetu haina ulinzi.”

    10 42:10Wakamjibu, “Sivyo bwana wangu. Watumishi wako wamekuja kununua chakula. 11 42:11Sisi sote ni wana wa baba mmoja. Watumishi wako ni watu waaminifu, wala sio wapelelezi.”

    12 42:12Akawaambia, “La hasha! Mmekuja kuangalia mahali ambapo nchi yetu haina ulinzi.”

    13 42:13Lakini wakamjibu, “Watumishi wako walikuwa kumi na wawili, wana wa mtu mmoja ambaye anaishi katika nchi ya Kanaani. Sasa mdogo wetu wa mwisho yupo na baba yetu na mwingine alikufa.”

    14 42:14Yosefu akawaambia, “Ni sawa kabisa kama nilivyowaambia: Ninyi ni wapelelezi! 15 42:15Na hivi ndivyo mtakavyojaribiwa: Hakika kama Farao aishivyo, hamtaondoka mahali hapa mpaka ndugu yenu mdogo aje hapa. 16 42:16Tumeni mmoja wenu akamlete huyo ndugu yenu, wengine mtawekwa gerezani, ili maneno yenu yajaribiwe kuona kama mnasema kweli. La sivyo, hakika kama Farao aishivyo ninyi ni wapelelezi!” 17 42:17Akawaweka wote chini ya ulinzi kwa siku tatu.

    18 42:18Siku ya tatu Yosefu akawaambia, “Fanyeni hili nanyi mtaishi, kwa maana namwogopa Mungu: 19 42:19Ikiwa ninyi ni watu waaminifu, mmoja wa ndugu zenu na abaki kifungoni, nanyi wengine pelekeni nafaka kwa jamaa yenu wanaoteseka kwa njaa. 20 42:20Lakini ni lazima mniletee ndugu yenu mdogo hapa, ili maneno yenu yathibitike na kwamba msife.” Wakakubali kufanya hivyo.

    21 42:21Wakaambiana wao kwa wao, “Hakika tunaadhibiwa kwa sababu ya ndugu yetu. Tuliona jinsi alivyohuzunika alipokuwa anatusihi kuponya maisha yake, lakini hatukumsikiliza, hiyo ndiyo sababu dhiki hii imetupata.”

    22 42:22Reubeni akawajibu, “Sikuwaambieni msitende dhambi dhidi ya kijana? Lakini hamkunisikiliza! Sasa ni lazima tuadhibiwe kwa ajili ya damu yake.” 23 42:23Hawakujua kuwa Yosefu angewaelewa, kwa sababu alitumia mkalimani.

    24 42:24Yosefu akajitenga nao akaanza kulia, kisha akawarudia na kuzungumza nao tena. Akataka Simeoni akamatwe na kufungwa mbele yao.

    25 42:25Yosefu akatoa amri ya kujaza magunia yao nafaka na kuweka fedha ya kila mmoja ndani ya gunia lake, kisha wapewe mahitaji ya njiani. Baada ya kufanyiwa hayo yote, 26 42:26wakapakiza nafaka juu ya punda zao, wakaondoka.

    27 42:27Walipofika mahali pa kulala huko njiani mmoja wao akafungua gunia lake ili amlishe punda wake, akakuta fedha yake kwenye mdomo wa gunia lake. 28 42:28Akawaambia ndugu zake, “Fedha yangu imerudishwa. Iko ndani ya gunia langu.”

    Mioyo yao ikazimia, na kila mmoja akamgeukia mwenzake wakitetemeka, wakaulizana, “Ni nini hiki Mungu alichotufanyia?”

    29 42:29Walipofika kwa Yakobo baba yao katika nchi ya Kanaani, wakamweleza mambo yote yaliyowapata. Wakasema, 30 42:30“Huyo mtu ambaye ndiye bwana katika nchi hiyo alisema nasi kwa ukali, akatutendea kana kwamba sisi tulikuwa tunaipeleleza nchi. 31 42:31Lakini tulimwambia, ‘Sisi ni watu waaminifu, sio wapelelezi. 32 42:32Tulizaliwa ndugu kumi na wawili, wana wa baba mmoja. Mmoja alikufa, na mdogo wetu wa mwisho yupo na baba yetu huko Kanaani.’

    33 42:33“Ndipo huyo mtu aliye bwana katika nchi hiyo alipotuambia, ‘Hivi ndivyo nitafahamu kuwa ninyi ni watu waaminifu: Mwacheni mmoja wa ndugu zenu pamoja nami hapa, kisha nendeni mpeleke chakula kwa ajili ya jamaa yenu inayoteseka kwa njaa. 34 42:34Lakini mleteni huyo ndugu yenu mdogo kwangu, ndipo nitajua kuwa ninyi sio wapelelezi, ila ni watu waaminifu. Kisha nitamrudisha ndugu yenu, nanyi mtaweza kufanya biashara katika nchi hii.’ ”

    35 42:35Walipokuwa wanamimina nafaka kutoka kwenye magunia yao, ndani ya gunia la kila mtu kulikuwa na mfuko wa fedha! Wakati wao na baba yao walipoona mifuko ya fedha, wakaogopa. 36 42:36Yakobo baba yao akawaambia, “Ninyi mmenipokonya watoto wangu. Yosefu hayupo na Simeoni hayupo tena na sasa mnataka kumchukua Benyamini. Kila kitu ni kinyume nami!”

    37 42:37Ndipo Reubeni akamwambia baba yake, “Waweza kuwaua wanangu wote wawili, ikiwa sitamrudisha Benyamini kwako. Mkabidhi Benyamini katika uangalizi wangu, nami nitamrudisha.”

    38 42:38Lakini Yakobo akasema, “Mwanangu hatashuka huko pamoja nanyi; ndugu yake amekufa naye ndiye peke yake aliyebaki. Ikiwa atapatwa na madhara katika safari mnayoiendea, mtashusha kichwa changu chenye mvi kaburini kwa masikitiko.”

    43Safari Ya Pili Ya Kwenda Misri

    1 43:1Wakati huu njaa ilikuwa bado ni kali mno katika nchi. 2 43:2Hivyo wakati walikuwa wamemaliza kula nafaka yote waliyoileta kutoka Misri, Yakobo baba yao akawaambia, “Rudini Misri mkatununulie chakula kingine zaidi.”

    3 43:3Lakini Yuda akamwambia, “Mtu yule alituonya kwa msisitizo, ‘Hamtauona uso wangu tena mpaka mje na ndugu yenu.’ 4 43:4Kama utakubali ndugu yetu aende pamoja nasi, tutakwenda kuwanunulia chakula. 5 43:5Lakini ikiwa hutamruhusu aende, hatutakwenda, kwa sababu mtu yule alituambia, ‘Hamtauona uso wangu tena mpaka mje pamoja na ndugu yenu.’ ”

    6 43:6Israeli akauliza, “Kwa nini mkaniletea taabu hii kwa kumwambia yule mtu mlikuwa na ndugu mwingine?”

    7 43:7Wakamjibu, “Yule mtu alituhoji kwa undani sana habari zetu na za jamaa yetu. Alituuliza, ‘Je, baba yenu bado yungali hai? Je mnaye ndugu mwingine?’ Sisi tulimjibu maswali yake tu. Tungewezaje kujua kwamba angesema, ‘Mleteni mdogo wenu hapa’?”

    8 43:8Ndipo Yuda akamwambia baba yake Israeli, “Mtume kijana pamoja nami, nasi tutaondoka mara, ili sisi na wewe pamoja na watoto wetu tuweze kuishi, wala tusife. 9 43:9Mimi mwenyewe nitakuhakikishia usalama wake, mimi mwenyewe nitawajibika kumrudisha. Ikiwa sitamrudisha kwako na kumweka mbele yako, nitakuwa mwenye lawama mbele yako maisha yangu yote. 10 43:10Hakika, kama hatukuchelewa kuondoka, tungekuwa tumekwenda na kurudi mara mbili.”

    11 43:11Basi baba yao Israeli akawaambia, “Kama ni lazima iwe hivyo, basi fanyeni hivi: Wekeni baadhi ya mazao bora ya nchi katika mifuko yenu na mpelekeeni yule mtu kama zawadi, zeri kidogo, asali kidogo, vikolezo, manemane, kungu na lozi. 12 43:12Chukueni fedha mara mbili, kwa kuwa mtazirudisha zile fedha zilizowekwa midomoni mwa magunia yenu. Labda ziliwekwa kwa makosa. 13 43:13Mchukueni ndugu yenu pia mrudi kwa huyo mtu mara moja. 14 43:14Naye Mungu Mwenyezi 43:14 Mungu Mwenyezi hapa ni jina la Kiebrania, El-Shaddai (yaani Mungu Mwenye utoshelevu wote). awajalieni rehema mbele ya huyo mtu ili apate kumwachia yule ndugu yenu na Benyamini mweze kurudi pamoja. Kwangu mimi kama nikufiwa nimefiwa.”

    15 43:15Basi hao watu wakazichukua zile zawadi na zile fedha mara mbili pamoja na Benyamini. Wakafanya haraka kwenda Misri na walipofika wakajionyesha kwa Yosefu. 16 43:16Yosefu alipomwona Benyamini pamoja nao, akamwambia msimamizi wa nyumba yake, “Wachukue watu hawa nyumbani kwangu, mchinje mnyama na kuandalia chakula kwa kuwa watakula chakula cha mchana pamoja nami.”

    17 43:17Yule Msimamizi akafanya kama Yosefu alivyomwambia na akawachukua wale watu nyumbani kwa Yosefu. 18 43:18Basi watu hao wakaogopa walipopelekwa nyumbani kwa Yosefu. Wakafikiri, “Tumeletwa hapa kwa ajili ya zile fedha zilizorudishwa katika magunia yetu mara ile ya kwanza. Anataka kutushambulia na kutushinda, atuchukue sisi kama watumwa, na atwae hawa punda zetu.”

    19 43:19Hivyo wakamwendea msimamizi wa nyumba wa Yosefu na kuzungumza naye kwenye ingilio la nyumbani. 20 43:20Wakasema, “Tafadhali bwana, tulikuja hapa mara ya kwanza kununua chakula. 21 43:21Lakini mahali pale tulipotua wakati wa jioni tulifungua magunia yetu, na kila mmoja wetu akakuta fedha zake, kwenye mdomo wa gunia lake kiasi kile kile tulicholeta. Kwa hiyo tumezirudisha. 22 43:22Pia tumeleta fedha nyingine kwa ajili ya kununulia chakula. Hatujui ni nani aliziweka fedha hizo katika magunia yetu.”

    23 43:23Akawaambia, “Vema, msiogope. Mungu wenu, Mungu wa baba yenu, amewapa ninyi hazina katika magunia yenu; mimi nilipokea fedha yenu.” Ndipo akawaletea Simeoni.

    24 43:24Msimamizi akawapeleka wale watu katika nyumba ya Yosefu, akawapa maji ya kunawa miguu na kuwapa punda wao majani. 25 43:25Wakaandaa zawadi zao ili wampe Yosefu wakati atakapofika adhuhuri, kwa kuwa walikuwa wamesikia kwamba watakula chakula huko.

    26 43:26Yosefu alipokuja nyumbani, walimkabidhi zile zawadi walizokuwa nazo, ambazo walikuwa wamezileta mle nyumbani, nao wakamsujudia hadi nchi. 27 43:27Akawauliza kuhusu hali yao, kisha akawaambia, “Yule baba yenu mzee mliyeniambia habari zake, yu hali gani? Je, bado yu hai?”

    28 43:28Wakamjibu, “Mtumishi wako baba yetu bado anaishi na ni mzima.” Kisha wakainama chini kumpa heshima.

    29 43:29Alipotazama na kumwona Benyamini ndugu yake, mwana wa mama yake hasa, akauliza, “Je, huyu ndiye ndugu yenu wa mwisho, ambaye mlinieleza habari zake?” Ndipo akasema, “Mungu na akufadhili, mwanangu.” 30 43:30Akiwa ameguswa sana kwa kumwona ndugu yake, Yosefu akatoka nje kwa haraka na kutafuta mahali pa kulilia. Akaingia kwenye chumba chake cha pekee na kulilia humo.

    31 43:31Baada ya kunawa uso wake, akatoka nje na huku akijizuia akasema, “Pakueni chakula.”

    32 43:32Wakampakulia Yosefu peke yake, ndugu zake peke yao na Wamisri waliokula pamoja naye peke yao, kwa sababu Wamisri wasingeweza kula pamoja na Waebrania, kwa maana ilikuwa ni chukizo kwa Wamisri. 33 43:33Watu hao walikuwa wameketi mbele yake kwa mfuatano wa umri wao, kuanzia mzaliwa wa kwanza hadi mzaliwa wa mwisho, wakatazamana wao kwa wao kwa mshangao. 34 43:34Wakati walipelekewa sehemu ya chakula kutoka mezani mwa Yosefu, sehemu ya Benyamini ilikuwa mara tano zaidi ya sehemu ya wale wengine. Kwa hiyo wakanywa na kufurahi pamoja naye.

    44Kikombe Cha Fedha Ndani Ya Gunia

    1 44:1Kisha Yosefu akampa yule msimamizi wa nyumbani mwake maagizo haya: “Jaza magunia ya watu hawa kiasi cha chakula ambacho wanaweza kuchukua, na uweke fedha ya kila mtu kwenye mdomo wa gunia lake. 2 44:2Kisha weka kikombe changu kile cha fedha kwenye mdomo wa gunia la yule mdogo wa wote pamoja na fedha zake ambazo angenunulia nafaka yake.” Naye akafanya kama Yosefu alivyosema.

    3 44:3Kulipopambazuka, hao watu wakaruhusiwa kuondoka pamoja na punda zao. 4 44:4Kabla hawajafika mbali kutoka mjini, Yosefu akamwambia mtumishi wake, “Wafuatilie wale watu mara moja, utakapowakuta, waambie, ‘Kwa nini mmelipiza wema kwa ubaya? 5 44:5Je, kikombe hiki sicho anachonywea bwana wangu na pia hukitumia kwa kutabiri mambo yajayo? Hili ni jambo ovu mlilolitenda.’ ”

    6 44:6Alipowafikia, akarudia maneno haya kwao. 7 44:7Lakini wakamwambia mtumishi, “Kwa nini bwana wangu anasema maneno kama haya? Liwe mbali na watumishi wako wasije wakafanya jambo kama hilo! 8 44:8Hata hivyo tulikurudishia zile fedha kutoka nchi ya Kanaani ambazo tulizikuta kwenye midomo ya magunia yetu. Hivyo kwa nini tuibe fedha au dhahabu kutoka nyumbani kwa bwana wako? 9 44:9Ikiwa yeyote miongoni mwa watumishi wako atapatikana nacho, auawe, na sisi wengine tutakuwa watumwa wa bwana wangu.”

    10 44:10Akajibu, “Vema sana; na iwe kama msemavyo. Yeyote atakayekutwa nacho atakuwa mtumwa wangu, lakini ninyi wengine mtakuwa hamna lawama.”

    11 44:11Kila mmoja wao akafanya haraka kushusha gunia lake chini na kulifungua. 12 44:12Ndipo msimamizi akaendelea kutafuta, akianzia kwa mkubwa wa wote na akaishia kwa mdogo wa wote. Basi kikombe kikapatikana katika gunia la Benyamini. 13 44:13Kwa jambo hili, wakararua nguo zao. Ndipo wote wakapakiza mizigo yao juu ya punda zao na kurudi mjini.

    14 44:14Yosefu alikuwa bado yuko nyumbani mwake wakati Yuda na kaka zake walipoingia, wote wakajitupa chini mbele yake. 15 44:15Yosefu akawaambia, “Ni jambo gani hili mlilolifanya? Hamjui kuwa mtu kama mimi anaweza kufahamu mambo kwa njia ya kutabiri?”

    16 44:16Yuda akajibu, “Tutaweza kusema nini kwa bwana wangu? Tutaweza kuzungumza nini? Tutawezaje kuthibitisha kwamba hatuna hatia? Mungu amefunua hatia ya watumishi wako. Sasa sisi tu watumwa wa bwana wangu, sisi wenyewe pamoja na yule aliyepatikana na kikombe.”

    17 44:17Lakini Yosefu alisema, “Liwe mbali nami kufanya jambo kama hili! Mtu yule tu aliyekutwa na kikombe ndiye atakayekuwa mtumwa wangu. Ninyi wengine, rudini kwa baba yenu kwa amani.”

    18 44:18Ndipo Yuda akamwendea na kumwambia: “Tafadhali bwana wangu, mruhusu mtumishi wako aseme neno kwa bwana wangu. Usimkasirikie mtumishi wako, ingawa wewe ni sawa na Farao mwenyewe. 19 44:19Bwana wangu aliwauliza watumishi wake, ‘Mnaye baba au ndugu?’ 20 44:20Nasi tukakujibu, ‘Tunaye baba yetu ambaye ni mzee; pia yupo mwanawe mdogo aliyezaliwa katika uzee wake. Ndugu yake amekufa, na huyu mdogo ndiye mwana pekee kwa mama yake aliyebaki, naye baba yake anampenda.’

    21 44:21“Ndipo ulipowaambia watumishi wako, ‘Mleteni kwangu ili niweze kumwona kwa macho yangu mwenyewe.’ 22 44:22Nasi tukamwambia bwana wangu, ‘Kijana hawezi kumwacha baba yake; akimwacha, baba yake atakufa.’ 23 44:23Lakini ukawaambia watumishi wako, ‘Ndugu yenu mdogo asiposhuka pamoja nanyi, hamtauona uso wangu tena.’ 24 44:24Tuliporudi nyumbani kwa mtumwa wako baba yangu, tulimwambia lile bwana wangu alilokuwa amesema.

    25 44:25“Ndipo baba yetu aliposema, ‘Rudini Misri mkanunue chakula kingine.’ 26 44:26Lakini tukamwambia, ‘Hatuwezi kushuka Misri mpaka ndugu yetu mdogo awe pamoja nasi ndipo tutakapokwenda. Hatutaweza kuuona uso wa yule mtu mpaka ndugu yetu mdogo awe pamoja nasi.’

    27 44:27“Mtumwa wako baba yangu alituambia, ‘Mnajua mke wangu alinizalia wana wawili. 28 44:28Mmojawapo alipotea, nami nikasema, “Hakika ameraruliwa vipande vipande.” Nami sijamwona tangu wakati huo. 29 44:29Ikiwa mtaniondolea huyu tena na akapatwa na madhara, mtashusha kichwa changu chenye mvi kaburini nikiwa mwenye huzuni.’

    30 44:30“Hivyo sasa, kama kijana hatakuwa pamoja nasi nitakaporudi kwa mtumishi wako baba yangu, na kama baba yangu, ambaye maisha yake yamefungamanishwa na uhai wa kijana huyu, 31 44:31akiona kijana hayupo nasi, atakufa. Watumishi wako watashusha kichwa chenye mvi cha baba yetu kaburini kwa huzuni. 32 44:32Mtumwa wako alimhakikishia baba yangu usalama wa kijana. Nikamwambia, ‘Kama sikumrudisha kwako nitakuwa mwenye lawama mbele yako, baba yangu, maisha yangu yote!’

    33 44:33“Sasa basi, tafadhali mruhusu mtumishi abaki hapa kama mtumwa wa bwana wangu badala ya kijana, naye kijana umruhusu arudi na ndugu zake. 34 44:34Ninawezaje kurudi kwa baba yangu kama kijana hatakuwa pamoja nami? La hasha! Usiniache nikaone huzuni ile itakayompata baba yangu.”

    45Yosefu Anajitambulisha

    1 45:1Hapo Yosefu hakuweza kujizuia zaidi mbele ya wote waliokuwa wamesimama karibu naye, akapaza sauti, akasema, “Mwondoeni kila mtu mbele yangu!” Kwa hiyo hapakuwepo mtu yeyote pamoja na Yosefu alipojitambulisha kwa ndugu zake. 2 45:2Naye akalia kwa sauti kubwa kiasi kwamba Wamisri walimsikia, hata watu wa nyumbani mwa Farao wakapata hizo habari.

    3 45:3Yosefu akawaambia ndugu zake, “Mimi ni Yosefu! Je, baba yangu angali hai bado?” Lakini ndugu zake hawakuweza kumjibu, kwa sababu walipatwa na hofu kuu mbele yake.

    4 45:4Ndipo Yosefu akawaambia ndugu zake, “Sogeeni karibu nami.” Waliposogea, akasema, “Mimi ni ndugu yenu Yosefu, yule ambaye mlimuuza Misri! 5 45:5Sasa, msihuzunike wala msijichukie wenyewe kwa kuniuza huku, kwa sababu ilikuwa ni ili kuokoa maisha ya watu ndiyo sababu Mungu alinituma niwatangulie ninyi. 6 45:6Kwa miaka miwili sasa imekuwepo njaa katika nchi, pia kwa miaka mitano ijayo hapatakuwepo kulima wala kuvuna. 7 45:7Lakini Mungu alinitanguliza mbele yenu ili kuhifadhi mabaki kwa ajili yenu katika nchi, na kuokoa maisha yenu kwa wokovu mkuu.

    8 45:8“Kwa hiyo basi, si ninyi mlionileta huku, bali ni Mungu. Alinifanya kuwa baba kwa Farao, bwana wa watu wa nyumbani mwake wote, na mtawala wa Misri yote. 9 45:9Sasa rudini haraka kwa baba yangu na mwambieni, ‘Hili ndilo mwanao Yosefu asemalo: Mungu amenifanya mimi kuwa bwana wa Misri yote. Shuka uje kwangu, wala usikawie. 10 45:10Nawe utaishi katika nchi ya Gosheni na kuwa karibu nami, wewe, watoto wako na wajukuu wako, makundi yako ya kondoo, mbuzi na ngʼombe, pamoja na vyote ulivyo navyo. 11 45:11Nitawatunza huko, kwa sababu bado iko miaka mingine mitano inayokuja ya njaa. La sivyo, wewe na nyumba yako na wote ulio nao mtakuwa fukara.’

    12 45:12“Mnaweza kujionea wenyewe, hata ndugu yangu Benyamini, kwamba hakika ni mimi ninayezungumza nanyi. 13 45:13Mwambieni baba yangu juu ya heshima yote niliyopewa huku Misri, na kuhusu kila kitu mlichokiona. Mleteni baba yangu huku haraka.”

    14 45:14Ndipo akamkumbatia Benyamini ndugu yake na kulia, naye Benyamini akamkumbatia akilia. 15 45:15Pia akawabusu ndugu zake wote, huku akilia. Baada ya hayo ndugu zake wakazungumza naye.

    16 45:16Habari zilipofika kwenye jumba la Farao kwamba ndugu zake Yosefu wamefika, Farao na maafisa wake wote wakafurahi. 17 45:17Farao akamwambia Yosefu, “Waambie ndugu zako, ‘Fanyeni hivi: Pakieni wanyama wenu mrudi mpaka nchi ya Kanaani, 18 45:18mkamlete baba yenu na jamaa zenu kwangu. Nitawapa sehemu nzuri sana ya nchi ya Misri nanyi mtafurahia unono wa nchi.’

    19 45:19“Mnaagizwa pia kuwaambia, ‘Fanyeni hivi: Chukueni magari ya kukokotwa kutoka Misri, kwa ajili ya watoto wenu na wake zenu, mkamchukue baba yenu mje. 20 45:20Msijali kamwe kuhusu mali zenu, kwa sababu mema yote ya Misri yatakuwa yenu.’ ”

    21 45:21Hivyo wana wa Israeli wakafanya hivyo. Yosefu akawapa magari ya kukokotwa, kama Farao alivyoagiza, pia akawapa mahitaji kwa ajili ya safari yao. 22 45:22Kila mmoja mavazi mapya, lakini Benyamini akampa shekeli 300 45:22 Shekeli 300 za fedha ni sawa na kilo 3.4. za fedha, na jozi tano za nguo. 23 45:23Hivi ndivyo vitu alivyotuma kwa baba yake: punda kumi waliochukua vitu vizuri vya Misri, punda wake kumi waliobeba nafaka, mikate na mahitaji mengine ya safari. 24 45:24Akaagana na ndugu zake walipokuwa wakiondoka, akawaambia, “Msigombane njiani!”

    25 45:25Basi wakatoka Misri na kufika kwa baba yao Yakobo katika nchi ya Kanaani. 26 45:26Wakamwambia baba yao, “Yosefu angali hai! Ukweli ni kwamba yeye ndiye mtawala wa Misri yote.” Yakobo akapigwa na bumbuazi; hakuwasadiki. 27 45:27Lakini walipokwisha kumweleza kila kitu ambacho Yosefu alikuwa amewaambia, na alipoona magari ya kukokotwa Yosefu aliyokuwa amempelekea ya kumchukua aende Misri, roho ya baba yao Yakobo ikahuishwa. 28 45:28Ndipo Israeli akasema, “Nimesadiki! Mwanangu Yosefu bado yu hai. Nitakwenda nikamwone kabla sijafa.”

    46Yakobo Aenda Misri

    1 46:1Hivyo Israeli akaondoka na vyote vilivyokuwa mali yake, naye alipofika Beer-Sheba, akamtolea dhabihu Mungu wa Isaki baba yake.

    2 46:2Mungu akanena na Israeli katika maono usiku na kusema, “Yakobo! Yakobo!”

    Akajibu, “Mimi hapa.”

    3 46:3Mungu akamwambia, “Mimi ndimi Mungu wa baba yako, usiogope kushuka Misri, kwa maana huko nitakufanya taifa kubwa. 4 46:4Nitashuka Misri pamoja nawe, nami hakika nitakurudisha tena Kanaani. Mikono ya Yosefu mwenyewe ndiyo itakayofunga macho yako.”

    5 46:5Ndipo Yakobo akaondoka Beer-Sheba nao wana wa Israeli wakamchukua baba yao Yakobo na watoto wao na wake zao katika magari ya kukokotwa yale Farao aliyokuwa amempelekea kumsafirisha. 6 46:6Wakachukua pia mifugo yao na mali walizokuwa wamezipata Kanaani, Yakobo na uzao wake wote wakashuka Misri. 7 46:7Akawachukua wanawe na binti zake, wajukuu wake wa kiume na wa kike, yaani uzao wake wote mpaka Misri.

    8 46:8Haya ndiyo majina ya wana wa Israeli (Yakobo na wazao wake), waliokwenda Misri:

  • Reubeni mzaliwa wa kwanza wa Yakobo.
  • 9 46:9Wana wa Reubeni ni:
  • Hanoki, Palu, Hesroni na Karmi.
  • 10 46:10Wana wa Simeoni ni:
  • Yemueli, Yamini, Ohadi, Yakini, Sohari na Shauli mwana wa mwanamke Mkanaani.
  • 11 46:11Wana wa Lawi ni:
  • Gershoni, Kohathi na Merari.
  • 12 46:12Wana wa Yuda ni:
  • Eri, Onani, Shela, Peresi na Zera (lakini Eri na Onani walifariki katika nchi ya Kanaani). Wana wa Peresi ni: Hesroni na Hamuli.
  • 13 46:13Wana wa Isakari ni:
  • Tola, Puva, Yashubu na Shimroni.
  • 14 46:14Wana wa Zabuloni ni:
  • Seredi, Eloni na Yaleeli.

    15 46:15Hawa ndio wana wa Lea aliomzalia Yakobo huko Padan-Aramu pamoja na binti yake Dina. Jumla ya wanawe na binti zake walikuwa thelathini na watatu.

  • 16 46:16Wana wa Gadi ni:
  • Sefoni, Hagi, Shuni, Esboni, Eri, Arodi na Areli.
  • 17 46:17Wana wa Asheri ni:
  • Imna, Ishva, Ishvi na Beria. Dada yao alikuwa Sera. Wana wa Beria ni: Heberi na Malkieli.

    18 46:18Hawa ndio watoto Zilpa aliomzalia Yakobo, ambao Labani alimpa binti yake Lea; jumla yao walikuwa kumi na sita.

  • 19 46:19Wana wa Raheli mke wa Yakobo ni:
  • Yosefu na Benyamini. 20 46:20Huko Misri, Asenathi binti wa Potifera, aliyekuwa kuhani wa mji wa Oni, 46:20 Yaani Heliopoli (Mji wa Jua). alimzalia Yosefu wana wawili, Manase na Efraimu.
  • 21 46:21Wana wa Benyamini ni:
  • Bela, Bekeri, Ashbeli, Gera, Naamani, Ehi, Roshi, Mupimu, Hupimu na Ardi.

    22 46:22Hawa ndio wana wa Raheli aliomzalia Yakobo; jumla yao ni kumi na wanne.

  • 23 46:23Mwana wa Dani ni:
  • Hushimu.
  • 24 46:24Wana wa Naftali ni:
  • Yaseeli, Guni, Yeseri na Shilemu.

    25 46:25Hawa walikuwa wana wa Bilha aliomzalia Yakobo, ambaye Labani alikuwa amempa Raheli binti yake; jumla yao walikuwa saba.

    26 46:26Wote waliokwenda Misri pamoja na Yakobo, waliokuwa wazao wake hasa pasipo kuhesabu wakwe zake, walikuwa watu sitini na sita. 27 46:27Pamoja na wana wawili waliozaliwa na Yosefu huko Misri, jumla yote ya jamaa ya Yakobo, waliokwenda Misri, walikuwa sabini.

    28 46:28Basi Yakobo akamtanguliza Yuda aende kwa Yosefu ili amwelekeze njia ya Gosheni. Walipofika nchi ya Gosheni, 29 46:29gari kubwa zuri la Yosefu liliandaliwa, naye akaenda Gosheni kumlaki baba yake Israeli. Mara Yosefu alipofika mbele yake, alimkumbatia baba yake, akalia kwa muda mrefu.

    30 46:30Israeli akamwambia Yosefu, “Sasa niko tayari kufa, kwa kuwa nimejionea mwenyewe kwamba bado uko hai.”

    31 46:31Ndipo Yosefu akawaambia ndugu zake na watu wa nyumbani mwa baba yake, “Nitapanda kwa Farao na kumwambia, ‘Ndugu zangu na watu wa nyumbani mwa baba yangu, waliokuwa wakiishi katika nchi ya Kanaani, wamekuja kwangu. 32 46:32Watu hao ni wachunga mifugo, huchunga mifugo, wamekuja na makundi ya kondoo, mbuzi na ngʼombe pamoja na kila kitu walicho nacho.’ 33 46:33Farao atakapowaita na kuwaulizeni, ‘Kazi yenu ni nini?’ 34 46:34Mjibuni, ‘Watumwa wako wamekuwa wachunga mifugo tangu ujana wetu mpaka sasa, kama baba zetu walivyofanya.’ Ndipo mtakaporuhusiwa kukaa katika nchi ya Gosheni, kwa kuwa wachunga mifugo wote ni chukizo kwa Wamisri.”

    47Yakobo Ambariki Farao

    1 47:1Yosefu akaenda na kumwambia Farao, “Baba yangu na ndugu zangu wamekuja kutoka nchi ya Kanaani wakiwa na makundi yao ya kondoo, mbuzi na ngʼombe, pamoja na kila kitu walicho nacho, nao sasa wapo huko Gosheni.” 2 47:2Akachagua ndugu zake watano na kuwaonyesha kwa Farao.

    3 47:3Farao akawauliza hao ndugu zake, “Kazi yenu ni nini?”

    Wakamjibu, “Watumishi wako ni wachunga mifugo, kama vile baba zetu walivyokuwa.” 4 47:4Pia wakamwambia Farao, “Tumekuja kukaa huku kwa muda mfupi, kwa sababu njaa ni kali huko Kanaani, na mifugo ya watumishi wako haina malisho. Kwa hiyo sasa, tafadhali uruhusu watumishi wako wakae huko Gosheni.”

    5 47:5Farao akamwambia Yosefu, “Baba yako na ndugu zako wamekuja kwako, 6 47:6nayo nchi ya Misri ipo mbele yako, uwakalishe baba yako na ndugu zako katika sehemu iliyo bora kupita zote katika nchi. Na waishi Gosheni. Kama unamfahamu yeyote miongoni mwao mwenye uwezo maalum, waweke wawe wasimamizi wa mifugo yangu.”

    7 47:7Ndipo Yosefu akamleta Yakobo baba yake na kumtambulisha mbele ya Farao. Baada ya Yakobo kumbariki Farao, 8 47:8Farao akamuuliza, “Je una umri gani?”

    9 47:9Naye Yakobo akamwambia Farao, “Siku za miaka ya kusafiri kwangu ni miaka 130. Miaka yangu imekuwa michache na ya taabu, wala haikufikia miaka ya kusafiri ya baba zangu.” 10 47:10Kisha Yakobo akambariki Farao, naye akaondoka mbele ya uso wake.

    11 47:11Ndipo Yosefu akawakalisha baba yake na ndugu zake katika nchi ya Misri na kuwapa milki katika sehemu bora sana ya nchi, wilaya ya Ramesesi, kama Farao alivyoelekeza. 12 47:12Pia Yosefu akampa baba yake, na ndugu zake na wote wa nyumbani mwa baba yake vyakula, kwa kulingana na hesabu ya watoto wao.

    Uongozi Wa Yosefu Wakati Wa Njaa

    13 47:13Hata hivyo, hapakuwepo chakula katika sehemu yote kwa kuwa njaa ilikuwa kali sana; Misri na Kanaani zote zikaharibiwa kwa sababu ya njaa. 14 47:14Yosefu akakusanya fedha zote zilizopatikana kutoka mauzo ya nafaka huko Misri na Kanaani, akazileta kwenye jumba la kifalme la Farao. 15 47:15Fedha za watu wa Misri na Kanaani zilipokwisha, Wamisri wote wakamjia Yosefu na kumwambia, “Tupatie chakula. Kwa nini tufe mbele ya macho yako? Fedha zetu zimekwisha.”

    16 47:16Yosefu akawaambia, “Basi leteni mifugo yenu, nitawauzia chakula kwa kubadilisha na mifugo yenu, kwa kuwa fedha zenu zimekwisha.” 17 47:17Kwa hiyo wakaleta mifugo yao kwa Yosefu, naye akawapa chakula kwa kubadilishana na farasi zao, kondoo na mbuzi zao, ngʼombe na punda zao. Katika mwaka huo wote Yosefu akawapa chakula kwa kubadilishana na mifugo yao yote.

    18 47:18Mwaka ule ulipokwisha, wakamjia mwaka uliofuata na kumwambia, “Hatuwezi kuficha ukweli mbele za bwana wetu kwamba, kwa kuwa fedha zetu zimekwisha na wanyama wetu ni mali yako, sasa hakuna chochote kilichosalia kwa ajili ya bwana wetu isipokuwa miili yetu na ardhi yetu. 19 47:19Kwa nini tuangamie mbele ya macho yako, sisi pamoja na nchi yetu? Utununue sisi pamoja na ardhi yetu ili kubadilishana kwa chakula. Nasi pamoja na nchi yetu tutakuwa watumwa wa Farao. Tupe sisi mbegu ili tuweze kuishi wala tusife, nchi yetu isije ikawa ukiwa.”

    20 47:20Kwa hiyo Yosefu akamnunulia Farao nchi yote ya Misri. Wamisri, mmoja baada ya mwingine, waliuza mashamba yao, kwa sababu njaa ilikuwa kali sana kwao. Nchi ikawa mali ya Farao, 21 47:21naye Yosefu akawafanya watu watumike kama watumwa, kuanzia upande mmoja wa Misri hadi upande mwingine. 22 47:22Hata hivyo, hakununua nchi ya makuhani, kwa sababu walikuwa wanapata mgawo wao wa kawaida kutoka kwa Farao, nao walikuwa na chakula cha kuwatosha kutokana na mgawo waliopewa na Farao. Hii ndiyo sababu hawakuuza ardhi yao.

    23 47:23Yosefu akawaambia watu, “Kwa vile nimewanunua ninyi pamoja na nchi yenu leo kuwa mali ya Farao, hapa kuna mbegu kwa ajili yenu ili mweze kuziotesha. 24 47:24Lakini wakati mazao yatakapokuwa tayari, mpeni Farao sehemu ya tano. Sehemu hizo nne zitakazobaki mtaziweka kama mbegu kwa ajili ya mashamba na kwa ajili ya chakula chenu wenyewe na cha watu wa nyumbani mwenu na watoto wenu.”

    25 47:25Wakamwambia, “Umeokoa maisha yetu. Basi na tupate kibali mbele ya macho ya bwana wetu; tutakuwa watumwa wa Farao.”

    26 47:26Basi Yosefu akaiweka iwe sheria kuhusu nchi ya Misri, ambayo inatumika mpaka leo, kwamba, sehemu ya tano ya mazao ni mali ya Farao. Ni nchi ya makuhani tu ambayo haikuwa ya Farao.

    27 47:27Basi Waisraeli wakaishi Misri katika nchi ya Gosheni. Wakapata mali huko wakastawi na kuongezeka kwa wingi sana.

    28 47:28Yakobo akaishi Misri miaka kumi na saba, nayo miaka ya maisha yake ilikuwa 147. 29 47:29Wakati ulipokaribia wa Israeli kufa, akamwita mwanawe Yosefu na kumwambia, “Kama nimepata kibali machoni pake, weka mkono wako chini ya paja langu na uniahidi kuwa utanifanyia fadhili na uaminifu. Usinizike Misri, 30 47:30lakini nitakapopumzika na baba zangu, unichukue kutoka Misri, ukanizike walipozikwa.”

    Yosefu akamwambia, “Nitafanya kama unavyosema.”

    31 47:31Akamwambia, “Niapie.” Ndipo Yosefu akamwapia, naye Israeli akaabudu, akiwa ameegemea juu ya kichwa cha fimbo yake.

    48Manase Na Efraimu

    1 48:1Baada ya muda Yosefu akaambiwa kwamba, “Baba yako ni mgonjwa.” Kwa hiyo akawachukua wanawe wawili Manase na Efraimu, pamoja naye. 2 48:2Yakobo alipoambiwa, “Mwanao Yosefu amekujia kukuona,” Israeli akakusanya nguvu zake, akaketi kitandani.

    3 48:3Yakobo akamwambia Yosefu, “Mungu Mwenyezi 48:3 Mungu Mwenyezi hapa ni jina la Kiebrania, El-Shaddai (yaani Mungu Mwenye utoshelevu wote). alinitokea huko Luzu katika nchi ya Kanaani, huko akanibariki, 4 48:4naye akaniambia, ‘Nitakufanya ustawi na kuongezeka hesabu yako, nitakufanya kuwa jamii ya mataifa, nami nitakupa nchi hii uimiliki milele wewe na wazao wako baada yako.’

    5 48:5“Sasa basi, wanao wawili waliozaliwa kwako huku Misri kabla sijaja hapa kwako watahesabiwa kuwa ni wangu; Efraimu na Manase watakuwa wangu, kama vile Reubeni na Simeoni walivyo wangu. 6 48:6Lakini watoto utakaowazaa baada yao watakuwa wako. Katika nchi watakayoirithi, watatambuliwa kwa jina la ndugu zao. 7 48:7Nilipokuwa ninarudi kutoka Padani, katika huzuni yangu Raheli alifariki katika nchi ya Kanaani tulipokuwa tungali tukisafiri, tukiwa karibu kufika Efrathi. Kwa hiyo nilimzika huko, kando ya njia iendayo Efrathi” (yaani Bethlehemu).

    8 48:8Wakati Israeli alipowaona wana wa Yosefu, akauliza, “Hawa ni nani?”

    9 48:9Yosefu akamjibu baba yake, “Hawa ni wana ambao Mungu amenipa nikiwa huku.”

    Ndipo Israeli akasema, “Walete kwangu ili niwabariki.”

    10 48:10Basi macho ya Israeli yalikuwa hayaoni vizuri kwa sababu ya uzee, naye aliona kwa shida. Kwa hiyo Yosefu akawaleta wanawe karibu na baba yake, Israeli akawabusu na akawakumbatia.

    11 48:11Israeli akamwambia Yosefu, “Kamwe sikutazamia kuuona uso wako tena, lakini sasa Mungu ameniruhusu kuwaona watoto wako pia.”

    12 48:12Ndipo Yosefu akawaondoa wanawe magotini mwa Israeli naye akasujudu hadi nchi. 13 48:13Yosefu akachukua wale wana wawili, Efraimu kwenye mkono wake wa kuume akimwelekeza kwenye mkono wa kushoto wa Israeli, na Manase katika mkono wake wa kushoto akimwelekeza kwenye mkono wa kuume wa Israeli, akawaleta karibu na babu yao. 14 48:14Lakini Israeli akaupeleka mkono wake wa kuume, akauweka juu ya kichwa cha Efraimu, ingawa alikuwa ndiye mdogo, na mkono wake wa kushoto akaukatisha, akauweka juu ya kichwa cha Manase, ingawa Manase alikuwa ndiye mzaliwa wa kwanza.

    15 48:15Ndipo akambariki Yosefu akisema,

    “Mungu ambaye baba zangu Abrahamu na Isaki walimtii, Mungu ambaye amekuwa mchungaji wa maisha yangu yote mpaka leo hii, 16 48:16Malaika ambaye aliniokoa kutoka madhara yote, yeye na awabariki vijana hawa. Na waitwe kwa jina langu na kwa majina ya baba zangu Abrahamu na Isaki, wao na waongezeke kwa wingi katika dunia.”

    17 48:17Yosefu alipoona baba yake akiweka mkono wa kuume juu ya kichwa cha Efraimu, hakupendezwa, kwa hiyo akauchukua mkono wa baba yake kutoka kichwa cha Efraimu na kuuweka juu ya kichwa cha Manase. 18 48:18Yosefu akamwambia, “Hapana, baba yangu, huyu ndiye mzaliwa wa kwanza; uweke mkono wako wa kuume juu ya kichwa chake.”

    19 48:19Lakini baba yake akakataa, akasema, “Ninajua, mwanangu, ninajua. Yeye pia atakuwa taifa, naye pia atakuwa mkuu. Hata hivyo, ndugu yake mdogo atakuwa mkuu kuliko yeye, nao wazao wake watakuwa kundi la mataifa.” 20 48:20Akawabarikia siku ile na kusema,

    “Kwa jina lenu Israeli watatamka baraka hii: ‘Mungu na awafanye kama Efraimu na Manase.’ ” Kwa hiyo akamtanguliza Efraimu mbele ya Manase.

    21 48:21Ndipo Israeli akamwambia Yosefu, “Mimi ninakaribia kufa, lakini Mungu atakuwa pamoja nanyi, na atawarudisha katika nchi ya baba zenu. 22 48:22Kwako wewe, kama aliye juu ya ndugu zako, ninakupa sehemu moja zaidi ya ndugu zako, lile eneo nililoteka kwa Waamori kwa upanga wangu na upinde wangu.”

    49Yakobo Abariki Wanawe

    1 49:1Ndipo Yakobo akawaita wanawe na kusema: “Kusanyikeni kunizunguka ili niweze kuwaambia lile litakalowatokea siku zijazo.

    2 49:2“Kusanyikeni na msikilize, enyi wana wa Yakobo, msikilizeni baba yenu Israeli. 3 49:3“Reubeni, wewe ni mzaliwa wangu wa kwanza, nguvu zangu, tunda la kwanza la nguvu zangu, umepita kwa heshima, umepita kwa uwezo. 4 49:4Usiyezuiwa kama maji, basi hutakuwa mkuu tena, kwa kuwa ulipanda kwenye kitanda cha baba yako, kwenye kitanda changu na kukinajisi. 5 49:5“Simeoni na Lawi ni wana ndugu: panga zao ni silaha za jeuri. 6 49:6Mimi na nisiingie katika baraza lao, nami nisiunganike katika kusanyiko lao, kwa kuwa wamewaua watu katika hasira yao, walikata mishipa ya miguu ya mafahali kama walivyopenda. 7 49:7Hasira yao na ilaaniwe, kwa kuwa ni kali mno, nayo ghadhabu yao ni ya ukatili! Nitawatawanya katika Yakobo Na kuwasambaza katika Israeli. 8 49:8“Yuda, ndugu zako watakusifu; mkono wako utakuwa shingoni mwa adui zako; wana wa baba yako watakusujudia. 9 49:9Ee Yuda, wewe ni mwana simba; unarudi toka mawindoni, mwanangu. Kama simba hunyemelea na kulala chini, kama simba jike: nani athubutuye kumwamsha? 10 49:10Fimbo ya ufalme haitaondoka kwa Yuda, wala fimbo ya mtawala kati ya miguu yake, hadi aje yeye ambaye milki ni yake, ambaye utii wa mataifa ni wake. 11 49:11Atamfunga punda wake katika mzabibu, naye mwana-punda wake kwenye tawi lililo bora zaidi; atafua mavazi yake katika divai, majoho yake katika damu ya mizabibu. 12 49:12Macho yake yatakuwa mekundu kwa divai, meno yake yatakuwa meupe kwa maziwa. 13 49:13“Zabuloni ataishi pwani ya bahari na kuwa bandari za kuegesha meli; mpaka wake utapanuka kuelekea Sidoni. 14 49:14“Isakari ni punda mwenye nguvu ambaye amelala kati ya mizigo yake. 15 49:15Aonapo palivyo pazuri mahali pake pa kupumzika na jinsi nchi yake inavyopendeza, atainamisha bega lake kwenye mzigo na kujitolea kwa ajili ya kazi ngumu. 16 49:16“Dani atahukumu watu wake kwa haki kama mmoja wa makabila ya Israeli. 17 49:17Dani atakuwa nyoka kando ya barabara, nyoka mwenye sumu kando ya njia, yule aumaye visigino vya farasi ili yule ampandaye aanguke chali. 18 49:18“Ee Bwana, nautafuta wokovu wako. 19 49:19“Gadi atashambuliwa ghafula na kundi la washambuliaji, lakini yeye atawageukia na kuwashinda kabisa. 20 49:20“Chakula cha Asheri kitakuwa kinono, naye atatoa chakula kitamu kimfaacho mfalme. 21 49:21“Naftali ni kulungu jike aliyeachiwa huru azaaye watoto wazuri. 22 49:22“Yosefu ni mzabibu uzaao, mzabibu uzaao ulio kando ya chemchemi, ambao matawi yake hutanda ukutani. 23 49:23Kwa uchungu wapiga mshale walimshambulia, wakampiga mshale kwa ukatili. 24 49:24Lakini upinde wake ulibaki imara, mikono yake ikatiwa nguvu, na mkono wa Mwenye Nguvu wa Yakobo, kwa sababu ya Mchungaji, Mwamba wa Israeli, 25 49:25kwa sababu ya Mungu wa baba yako, anayekusaidia, kwa sababu ya Mwenyezi, 49:25 Mwenyezi hapa ina maana ya Shaddai kwa Kiebrania. yeye anayekubariki kwa baraka za mbinguni juu, baraka za kilindi kilichoko chini, baraka za matitini na za tumbo la uzazi. 26 49:26Baraka za baba yako ni kubwa kuliko baraka za milima ya kale, nyingi kuliko vilima vya kale. Baraka hizo zote na zikae juu ya kichwa cha Yosefu, juu ya paji la yule mkuu miongoni mwa ndugu zake. 27 49:27“Benyamini ni mbwa mwitu mlafi mwenye njaa kuu; asubuhi hurarua mawindo yake, jioni hugawa nyara.”

    28 49:28Haya yote ndiyo makabila kumi na mawili ya Israeli, na hivi ndivyo baba yao alivyowaambia alipowabariki, akimpa kila mmoja baraka inayomfaa.

    Kifo Cha Yakobo

    29 49:29Ndipo alipowapa maelekezo haya: “Mimi niko karibu kukusanywa kwa watu wangu. Mnizike pamoja na baba zangu kwenye pango katika shamba la Efroni, Mhiti, 30 49:30pango lililoko katika shamba la Makpela, karibu na Mamre huko Kanaani, ambalo Abrahamu alinunua kwa ajili ya mahali pa kuzikia kutoka kwa Efroni, Mhiti, pamoja na shamba. 31 49:31Huko ndiko Abrahamu na Sara mkewe walikozikwa, huko akazikwa Isaki na Rebeka mkewe, na huko nilimzika Lea. 32 49:32Shamba hilo na pango lililoko ndani yake lilinunuliwa kutoka kwa Wahiti.”

    33 49:33Baada ya Yakobo kumaliza kutoa maelekezo hayo kwa wanawe, akarudisha miguu yake kitandani, akapumua pumzi ya mwisho, na akakusanywa kwa watu wake.

    501 50:1Basi Yosefu akamwangukia baba yake, akalilia juu yake na akambusu. 2 50:2Ndipo Yosefu akawaagiza matabibu waliokuwa wakimhudumia, wamtie baba yake Israeli dawa ili asioze. Hivyo matabibu wakamtia dawa asioze, 3 50:3wakatumia siku arobaini, kwa maana ndio muda uliotakiwa wa kutia dawa ili asioze. Nao Wamisri wakamwombolezea Yakobo kwa siku sabini.

    4 50:4Siku za kumwombolezea zilipokwisha, Yosefu akawaambia washauri wa Farao, “Kama nimepata kibali machoni penu semeni na Farao kwa ajili yangu. Mwambieni, 5 50:5‘Baba yangu aliniapisha na kuniambia, “Mimi niko karibu kufa; unizike katika kaburi lile nililochimba kwa ajili yangu mwenyewe katika nchi ya Kanaani.” Sasa nakuomba uniruhusu niende kumzika baba yangu, nami nitarudi.’ ”

    6 50:6Farao akasema, “Panda, uende kumzika baba yako, kama alivyokuapiza kufanya.”

    7 50:7Hivyo Yosefu akapanda kwenda kumzika baba yake. Maafisa wote wa Farao wakaenda pamoja naye, watu mashuhuri wa baraza lake na watu mashuhuri wote wa Misri. 8 50:8Hawa ni mbali na watu wote wa nyumbani kwa Yosefu, na ndugu zake, na wale wote wa nyumbani mwa baba yake. Ni watoto wao, makundi yao ya kondoo, mbuzi na ngʼombe tu waliobakia katika nchi ya Gosheni. 9 50:9Magari makubwa na wapanda farasi pia walipanda pamoja naye. Likawa kundi kubwa sana.

    10 50:10Walipofika kwenye sakafu ya kupuria nafaka ya Atadi, karibu na Yordani, wakalia kwa sauti na kwa uchungu; Yosefu akapumzika huko kwa siku saba kumwombolezea baba yake. 11 50:11Wakanaani walioishi huko walipoona maombolezo yaliyofanyika katika sakafu ile ya kupuria ya Atadi, wakasema, “Wamisri wanafanya maombolezo makubwa.” Kwa hiyo mahali pale karibu na Yordani pakaitwa Abel-Mizraimu. 50:11 Abel-Mizraimu maana yake Maombolezo ya Wamisri.

    12 50:12Hivyo wana wa Yakobo wakafanya kama baba yao alivyowaagiza: 13 50:13Wakamchukua mpaka nchi ya Kanaani, wakamzika kwenye pango katika shamba la Makpela, karibu na Mamre, ambalo Abrahamu alilinunua kutoka kwa Efroni, Mhiti, pamoja na shamba liwe mahali pa kuzikia. 14 50:14Baada ya Yosefu kumzika baba yake, akarudi Misri pamoja na ndugu zake na wale wote waliokuwa wamekwenda naye kumzika baba yake.

    Yosefu Awaondolea Ndugu Zake Mashaka

    15 50:15Ndugu zake Yosefu walipoona kwamba baba yao amekufa, wakasema, “Itakuwaje kama Yosefu ataweka kinyongo dhidi yetu na kutulipa mabaya yote tuliyomtendea?” 16 50:16Kwa hiyo wakampelekea Yosefu ujumbe, wakasema, “Kabla baba yako hajafa aliacha maagizo haya: 17 50:17‘Hili ndilo mtakalomwambia Yosefu: Ninakuomba uwasamehe ndugu zako dhambi na mabaya kwa vile walivyokutenda vibaya.’ Sasa tafadhali samehe dhambi za watumishi wa Mungu wa baba yako.” Ujumbe huu ulipomfikia, Yosefu akalia.

    18 50:18Ndipo ndugu zake wakaja na kujitupa chini mbele yake. Wakasema, “Sisi ni watumwa wako.”

    19 50:19Lakini Yosefu akawaambia, “Msiogope. Je, mimi ni badala ya Mungu? 20 50:20Mlikusudia kunidhuru, lakini Mungu alikusudia mema, ili litimie hili linalofanyika sasa, kuokoa maisha ya watu wengi. 21 50:21Hivyo basi, msiogope. Mimi nitawatunza ninyi nyote pamoja na watoto wenu.” Akawahakikishia na kusema nao kwa wema.

    Kifo Cha Yosefu

    22 50:22Yosefu akakaa katika nchi ya Misri, yeye pamoja na jamaa yote ya baba yake. Akaishi miaka 110, 23 50:23naye akaona kizazi cha tatu cha watoto wa Efraimu. Pia akaona watoto wa Makiri mwana wa Manase, wakawekwa magotini mwa Yosefu walipozaliwa.

    24 50:24Ndipo Yosefu akawaambia ndugu zake, “Mimi ninakaribia kufa. Lakini kwa hakika Mungu atawasaidia na kuwachukueni kutoka nchi hii na kuwapeleka katika nchi aliyomwahidi kwa kiapo Abrahamu, Isaki na Yakobo.” 25 50:25Naye Yosefu akawaapisha wana wa Israeli na kuwaambia, “Hakika Mungu atawasaidia, nanyi ni lazima mhakikishe mmepandisha mifupa yangu kutoka mahali hapa.”

    26 50:26Kwa hiyo Yosefu akafa akiwa na umri wa miaka 110. Baada ya kumtia dawa ili asioze, akawekwa kwenye jeneza huko Misri.